Latest News

Ezekiel Maige na James Lembeli 
SIKU chache baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James Lembeli kutoa taarifa yake bungeni iliyowang’oa mawaziri wanne, vita kali imeibuka kati yake na mbunge wa Msalala, Ezekiel Maige (CCM).
 
Itakumbukwa kuwa kamati hiyo ya Lembeli ndiyo ilishinikiza kung’olewa kwa Maige katika nafasi ya Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na mawaziri wengine mwaka jana kwa kashfa ya utoroshwaji wa wanyamapori hai nje ya nchi.

Kufuatia hatua hiyo, wakazi wa Msalala wilayani Kahama, Mkoa wa Shinyanga, wamemtaka Lembeli ambaye pia ni mbunge wa Kahama, amuombe radhi mbunge wao, Maige kutokana na walichodai ni fitina alizomzushia hadi akapoteza wadhifa wa uwaziri mwaka jana.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti juzi mjini Kahama, wakazi hao walisema wamelazimika kumtaka Lembeli amuombe radhi Maige kufuatia kitendo chake cha kutaka kumsafisha aliyekuwa waziri wa wizara hiyo, Balozi Khamis Kagasheki.

Lembeli katika kuhitimisha hoja ya taarifa ya kamati yake bungeni hivi karibuni, alimtetea Waziri Kagasheki aliyeamua kujiuzulu akidai hakuhusika moja kwa moja katika kashfa ya Operesheni Tokomeza Ujangili.

Wakazi hao walisema wanamtaka Lembeli aombe radhi ili amsafishe Maige kutokana na tuhuma kali alizomzushia wakati akiwa waziri kwa kumtuhumu kwamba alihusika na utoroshaji wanyamapori hai kwenda nje ya nchi.

Walisema kama Lembeli alikiri bungeni kuwa Waziri Kagasheki hakuhusika moja kwa moja na vitendo viovu vilivyotendwa na askari wakati wa kutekeleza operesheni hiyo, anapaswa kumwomba radhi na Maige ambaye pia hakuhusika moja kwa moja.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Masanja Joseph alifafanua kuwa katika taarifa yake bungeni, Lembeli alionyesha wazi dhamira ya kutaka kumsafisha Kagasheki akidai hakuhusika moja kwa moja licha ya unyama uliofanyika katika operesheni hiyo.

Joseph alisema Lembeli katika taarifa yake alidai watendaji ndani ya wizara hiyo wakiongozwa na Katibu Mkuu wao, Maimuna Tarishi ndio wanaostahili kubeba lawama na kuwajibishwa kwa vile Kagasheki hakuwa mtendaji wa moja kwa moja.

“Kauli hii ilitutia wasiwasi maana katika uamuzi wa kamati hiyo dhidi ya Maige, kuhusiana na kashfa ya utoroshwaji wa wanyama hai, huyo alibebeshwa msalaba peke yake ambapo hata maofisa usalama wa taifa hawakuguswa kabisa tofauti na ilivyokuwa kwa taarifa ya Operesheni Tokomeza Ujangili.

“Hii ni ajabu sana, wakati wa tuhuma za kutoroshwa wanyama hai, Lembeli alimbebesha moja kwa moja tuhuma Maige kuwa alizembea na kusababisha wanyama watoroshwe, leo katika kashfa ya Operesheni Tokemeza Ujangili anadai Kagasheki hakuhusika moja kwa moja, hapa hajatenda haki,” alieleza Joseph.

Wananchi hao walisema ni jambo la kushangaza kuona mtu ambaye tuhuma zake hazikuhusisha kupoteza maisha ya Watanzania alihukumiwa peke yake bila watendaji wengine.

Kwamba huyu ambaye ameguswa na tuhuma za mauaji ya binadamu na mifugo kuibwa na mingine kuuawa, anatetewa na kamati ikitaka mzigo wake ubebwe na watendaji ndani ya wizara.

“Kwa hali hii kuna kila sababu sasa Lembeli akamsafisha mbunge wetu kwamba hakumtendea haki, na ikibidi ifike wakati na yeye mwenyewe ajipime katika uhakimu wake anaoufanya mara kwa mara kama kweli huwa anatenda haki.

“Kwa taarifa hii aliyoitoa bungeni juzi ilionyesha wazi huenda alitofautiana na katibu mkuu wa wizara au watendaji wengine walioonyesha nia ya kutaka kupingana naye na hivyo kutaka awabebeshe zigo lote peke yao,” alisema.

Waliongeza kuwa kitendo cha Lembeli kuwawajibisha mawaziri wawili ndani ya wizara moja kimewashtua, huku tukio la mbunge wao Maige likibakia gumzo kwani hakupewa nafasi yoyote ya kutoa utetezi wake bungeni.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top