
WAKATI shinikizo la kumtaka Waziri Mkuu Mizengo Pinda kujiuzulu ama
awajibishwe kutokana na kashfa ya ukatili mauaji dhidi ya wananchi
wakati wa Operesheni Tokomeza Ujangili likizidi kushika kasi, vumbi
jipya la maofisa wa juu wa serikali wanaotakiwa kuwajibika limewaangukia
Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Said Mwema na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi
na Usalama, Jenerali Davis Mwamunyange.
Shinikizo hilo jipya limetoka kwa madiwani wa Halmashauri ya Jiji la
Dar es Salaam jana, ambao wamesema Mwema na Mwamunyange hawawezi
kujinusuru katika kadhia hiyo.
Katibu wa madiwani wa jiji hilo, Julian Bujugo, alisema wakuu hao wa
vyombo vya dola wanapaswa kujiuzulu kwa kuwa ndio wanaotoa amri kwa
askari walio chini yao.
“Pamoja na mawaziri, viongozi hao wanatakiwa kujiuzulu kama hatua ya
kuonyesha uwajibikaji kwani askari wao wamefanya maovu makubwa,”
alisema.
Madiwani hao wengi wao wakitoka Chama Cha Mapinduzi, walisema ripoti
ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Mazingira na Maliasili ilibainisha uozo
katika Operesheni Tokomeza Ujangili ambayo ilisimamiwa na askari wa
vyombo vyao.
Walisema kubainika kwa ukiukwaji wa haki za binadamu katika
operesheni hiyo, ndiko kulimsukuma Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi
wa mawaziri wanne ambao ni Shamsi Vuai Nahodha (Ulinzi na Jeshi la
Kujenga Taifa), Balozi Khamisi Kagasheki (Malisili na Utalii), Dk.
Emmanuel Nchimbi (Mambo ya Ndani) na Mathayo David (Maendeleo ya Mifugo
na Uvuvi).
Hivyo, kwa kuwa mawaziri hao waliwajibika, Mwema na Mwamunyange
hawana sababu ya kuendelea kushikilia nafasi zao zaidi ya kuwajibika
wenyewe ama wawajibishwe kwa mujibu wa sheria.
Pamoja na wakuu hao wa polisi na JWTZ, madiwani hao wametaka pia
wakuu wote wa wilaya waliohusika kusimamia operesheni hiyo nao
wawajibike kwa kuwa walijua na waliona vitendo walivyofanyiwa wananchi,
lakini hawakuchukua hatua yoyote.
Bujugo alisema kama viongozi hao watakaidi agizo la madiwani kuwataka wajiuzulu, watalipeleka suala hilo kwa Rais Kikwete.
Pinda ang’ang’aniwa
Nalo shinikizo la kumtaka Rais Kikwete kumng’oa Waziri Mkuu Mizengo
Pinda katika nafasi yake limezidi kuongezeka licha ya hatua ya kiongozi
huyo mkuu wa serikali bungeni kupuuza maoni ya wabunge.
Akizungumza kwa njia ya simu na Tanzania Daima Jumatano, Mwenyekiti
wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, alisema kuwa ili
serikali ionekane inaheshimu misingi ya haki za binadamu lazima Pinda
awajibike.
“Pinda lazima awajibike bila kujali kiasi cha gharama ambazo
zitapotea kwa kuwatunza wastaafu kwani tukio la kuuawa kwa Watanzania
ni kubwa kuliko la kuwahudumia wastaafu,” alisema Lipumba.
Alisema kuwa kama tunajipambanua kwa kufuata misingi ya kulinda haki
za binadamu, ni lazima Pinda aachie ngazi kutokana na namna
alivyolishughulikia suala hilo kimzaha kwa mara ya kwanza lilipoingia
bungeni.
Mkurugenzi Mtendaji wa TGNP, Usu Mallya alisema kuwa lazima Pinda
awajibishwe kwa sababu hata mwenyewe alikiri kwamba kazi ya uwaziri mkuu
ni mzigo kwake.
“Kwa maneno yake mwenyewe anaonyesha huo ni mzigo mzito aliobebeshwa
na hauwezi. Hivi Rais Kikwete kwanini asimuache mtoto wa mwenzake asije
kuvunjika kwa ajili ya mzigo huo,” alisema Mallya.
Akizungumza wale wanaofikiria kwamba iwapo atawajibishwa atasababisha
kuwepo kwa gharama kubwa serikalini, Usu alisema hakuna gharama kwa
sababu kwa mujibu wa sheria atapoteza haki zake na hivyo serikali haina
haki ya kuingia gharama za kumtunza.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Tanzania Labour Party (TLP), Augustine
Mrema alipingana na wanaoshinikiza kujiuzulu kwa Pinda, akiwataka
Watanzania kuridhika na hatua ya kung’oka mawaziri wanne.
“Iwapo tutamng’oa Waziri Mkuu, tutakuwa na mlundikano wa mawaziri
wastaafu hali itakayosababisha kuwepo kwa ongezeko la gharama za
kuwatunza. Kumbuka hata mimi nilikuwa Naibu Waziri Mkuu mstaafu mpaka
sasa sijalipwa fedha zangu, sasa tuongeze tena Pinda.
“Sisi tumeongoza nchi, hivyo tunatakiwa kuondokana na ushabiki ingawa
hata mimi napenda kuondolewa kwa Mizengo Pinda, lakini kwa wakati huu
ambao tunataka kuisafisha serikali niko tayari hata kumuongezea Rais
Kikwete watu wengine ambao hata yeye hawajui,” alisema.
Mrema aliongeza kuwa wapo baadhi ya mawaziri wabovu ambao Rais
Kikwete hawajui na ndio wamekuwa wakihusika kuvuruga utendaji wake.
Kamati hiyo iliyoongoza na James Lembeli iliwasilisha taarifa yake bungeni mwishoni mwa wiki iliyopita.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
0 comments:
Post a Comment