Hotuba ya Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati wa kufungua Mkutano Mkuu wa Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi Katika Ukumbi wa Bunge, Dodoma,  12 Februari 2013

Mheshimiwa Dkt. Emmanuel Nchimbi, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi;
Mheshimiwa Rehema Nchimbi, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma;
Ndugu Said Mwema, Inspekta Jenerali wa Polisi;
Makamishna na Naibu Makamishna wa Jeshi la Polisi;
Ndugu wajumbe;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Utangulizi
Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini kwa kunialika kuja kushiriki katika ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi wa mwaka 2013.  Nakupongeza sana Inspekta Jenerali kwa utaratibu huu mzuri mliojiwekea.   Hii ni fursa nzuri kwenu kupima maendeleo mliyopata katika utekelezaji wa majukumu yenu.  Mtajua mmefanikiwa kiasi gani na maeneo au mambo gani yamewatatiza. Kwa kufanya hivyo mnaweza kujua jinsi gani mtaimarisha mafanikio yenu, na mtatatuaje changamoto zinazowakabili ili mpate ufanisi mkubwa zaidi siku za usoni. 
Natumia neno “ufanisi mkubwa zaidi siku za usoni” kwa makusudi kabisa, kwani ni ukweli ulio wazi kuwa kila kukicha Jeshi la Polisi limekuwa linapata mafanikio.  Hata hivyo bado haitoshi lazima mlenge kupata mafanikio makubwa zaidi katika kupambana na uhalifu.  Nakupongeza kwa dhati kabisa Inspekta Jenerali, Makamu wa Polisi, Maafisa na askari wote wa Jeshi la Polisi kwa kazi kubwa na nzuri mnayoendelea kuifanya.  Ni ushahidi ulio wazi kuwa uhalifu unazidi kudhibitiwa na wahalifu wa aina mbalimbali wanazidi kubanwa.  Endeleeni na mwendo huo huo.


Kauli Mbiu ya Mwaka Huu
Mheshimiwa Waziri;
Inspekta Jenerali; na
Washiriki watu;

          Nimevutiwa sana na Kauli Mbiu ya mkutano wenu wa mwaka huu inayosema ‘Tujenge Uwezo wa Jamii na Polisi Kukabiliana na Vurugu, kwa kuimarisha Utii wa Sheria bila Shuruti”. Kauli Mbiu hii imebeba ujumbe muafaka katika mazingira tuliyonayo sasa katika nchi yetu.   Hivi sasa matukio ya vurugu yanaanza kuwa taarifa za kawaida.  Kila kukicha au kila baada ya muda mfupi kuna tukio la vurugu ya aina fulani mahali fulani na kwa sababu mbalimbali.  Kauli mbiu hii, inatukumbusha ukweli huo na umuhimu wa jamii na Polisi kushirikiana katika kukabiliana na vurugu nchini.  Aidha Kauli Mbiu yenu inasisitiza nafasi ya utii wa sheria bila shuruti katika kuzuia vurugu zisitokee au pale zinapotokea ziweze kumalizwa haraka bila ya madhara makubwa kwa pande husika.  Mimi naamini kama shabaha za Kauli Mbiu hii zitatimia, vurugu hazitakuwepo nchini na Tanzania patakuwa mahali salama kuishi kwa kila mtu. 
Mheshimiwa Waziri;
Ndugu Inspekta Jenerali;
Makamanda Waandamizi;

Vurugu ni changamoto mpya ya usalama wa raia, mali zao na nchi ambayo hatuna budi kukabiliana nayo.  Hatuna budi kukaa kitako na kutafakari kwa makini kiini cha vurugu na jinsi ya kukabiliana nazo kwa maana ya kuzuia zisitokee na zinapotokea zinamalizwa haraka bila ya kuwa na athari kubwa au kupunguza madhara kwa watakaoathirika.  Wapo wadau wengi ambao kila mmoja wao anao wajibu wake anaopaswa kuutekeleza. Kila mdau anatakiwa kuutambua wajibu huo na kuhakikisha kuwa anatimiza ipasavyo yale yanayomhusu.  Ninyi katika Jeshi la Polisi mnajua vyema wajibu wenu katika kudhibiti vurugu.  Bahati nzuri wajibu huo umetamkwa kisheria na una miongozo yake ambayo imeandikwa na hufundishwa katika vyuo na hufanyiwa mazoezi vikosini. 
Nawaomba suala la kuzuia na kudhibiti vurugu mlipe kipaumbele cha juu.  Najua siku za nyuma haikuwa lazima kufanya hivyo kwa sababu halikuwa tatizo kubwa.  Siku hizi sivyo.  Vurugu zinakuwa nyingi na za aina nyingi hivyo kugeuka kuwa shughuli kubwa ya jeshi letu.  Vurugu  zinasababishwa na mambo mengi.  Zipo zinazosababishwa na vyama vya siasa kwa kufanya mikutano na maandamano yasiyoruhusiwa.  Wakati mwingine hata pale yaliporuhusiwa wahusika hufanya mambo yasiyohusika ama wakati au baada ya mkutano.  Pia zipo vurugu zinazosababishwa na kauli za wanasiasa au wafuasi wa vyama vya siasa.  Vilevile zipo vurugu zinazosababishwa na watu kugombea rasilimali kama vile ardhi kwa wakulima na wafugaji na baina ya wananchi wasiokuwa na ardhi na wamiliki wa maeneo makubwa. Lakini, zipo pia vurugu zinazosababishwa na kauli na vitendo vya baadhi ya viongozi wa dini na waumini wao.  Kama yale yaliyotokea jana Buseresere, Geita.


Mheshimiwa Waziri;
Ndugu IGP;

Hatukuwa na  hali tuliyonayo sasa ya watu kutumia njia ya vurugu kuelezea hisia zao au kujaribu kutatua matatizo yanayowakabili.  Maadam sasa yameanza kujitokeza kwa nguvu hatuna budi kukabiliana kisawasawa na aina hii ya uhalifu.  Hatuna budi  kujifunza namna bora ya kukabiliana na vurugu. Hatuwezi kusema yatapita, lazima tukubali ukweli kuwa matukio haya yanaweza kuendelea kuwepo na hata kuongezeka siku za usoni.  Tunachotakiwa kufanya ni kuhakikisha kuwa tunajijengea uwezo wa kudhibiti vurugu na kufanya athari zake zinakuwa ndogo.
          Katika kukabiliana na vurugu kwanza kabisa ni muhimu kuelekeza nguvu zetu kwenye kuzuia zisitokee.  Kwa ajili hiyo ni muhimu kuyatambua maeneo na mazingira yanayoweza kuleta au kusababisha vurugu kutokea.  Kuwatambua wahusika wakuu na kuwasiliana nao ili kuelewana nao kuhusu namna ya kupata ufumbuzi wa tatizo lililopo ili kuzuia madhara yasitokee.  Natambua kuwa kazi hiyo mmekuwa mnaifanya kwa mafanikio makubwa.  Na mara zote pale ushauri wenu ulipopuuzwa madhara yalitokea.  Naomba muendelee na jitihada hizo.  Zitaliepusha taifa katika hatari nyingi. 
Mheshimiwa Waziri;
Ndugu IGP; na
Ndugu Makamanda;

Ninapoyasema haya kwenu natambua vilevile kwamba jukumu hilo si lenu peke yenu.  Shughuli za kuzuia vurugu zisitokee au kutuliza zinapotokea na kupata ufumbuzi wa migogoro  iliyozua vurugu inahusu wadau wengine pia.  Kwa mfano vurugu za wakulima na wafugaji kugombea ardhi zitapatiwa ufumbuzi wa uhakika na mamlaka zinazohusika na upangaji wa matumizi ya ardhi.  Wakitenga maeneo kwa ajili ya shughuli za kilimo na ufugaji inasaidia kutatua migogoro iliyopo na kuzuia isitokee siku za usoni.  Hali ni hiyo hiyo kwa migogoro mingine yote ambapo wapo wadau ambao wanaweza kufanya isitokee na kuipatia ufumbuzi inapotokea.  Naomba ninyi kwa upande wa polisi muwatambue watu hao na kushirikiana nao kwa karibu kwa ajili hiyo. 
Napenda kutumia nafasi hii kuwaasa viongozi na mamlaka husika kuwa wawe wepesi kutambua maeneo yenye migogoro inayoweza kusababisha vurugu na kuyatafutia ufumbuzi mapema masuala hayo.  Aidha migogoro na vurugu zinapotokea na wao wawe mstari wa mbele kushiriki katika jitihada za kutafuta suluhisho. Wasifanye ajizi bali watekeleze yanayowahusu kwa ukamilifu na kwa wakati.  Bila ya hivyo vurugu hazitaisha.  Halikadhalika, ushirikiano na uelewa wa wahusika wenyewe wa mgogoro au suala linaloweza kusababisha vurugu na utayari wao nao unaweza kuepusha shari na madhara.  Pale ambapo ushirikiano utakapokosekana na migongano kujitokeza, umahiri wa polisi kushirikisha wadau wote unahitajika kutuhakikishia ushindi.
Natambua kuwa katika kutimiza wajibu wenu kumekuwepo na lawama nyingi na madai dhidi ya Jeshi la Polisi.  Nawapongeza kwa jinsi mnavyoshughulikia tuhuma dhidi yenu.  Mmekuwa mnachukua hatua za kufanya uchunguzi na pale kosa lilipodhihirika hamkusita kuchukua hatua.  Naomba muendelee na utaratibu huo mzuri.  Unaliletea heshima Jeshi letu na kuwaziba midomo watu wasiowatakia mema.  Aidha, nawaomba mtambue maeneo ya udhaifu na kuyatafutia ufumbuzi kuanzia kwenye mafunzo ya vyuoni mpaka malezi ya askari wawapo kambini.
Hatua kadhaa zinachukuliwa kuzikabili changamoto
Makamanda na Maofisa Waandamizi
wa Jeshi la Polisi;

Nashukuru Ndugu IGP na Mheshimiwa Waziri kwa kuwa wawazi kuhusu changamoto zinazowakabili na jinsi mnavyoendelea kuzikabili na mlivyojipanga kuzikabili siku za usoni.  Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali itakuwa nanyi bega kwa bega kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakabili.  Natambua kuwa changamoto kubwa na ya msingi ni ile ya kutokutengewa fedha za kutosha.  Hili ni tatizo la kweli lakini tumekuwa tunalishughulikia na nawaahidi tutaendelea kufanya hivyo.  Jeshi la Polisi ni muhimu sana hatutaacha lidhoofike.
          Ndio maana tangu tulipoingia madarakani (mwaka 2005) tumeongeza sana bajeti ya Jeshi la Polisi na kuboresha mazingira ya kazi kwa kadri tulivyoweza. Kwa mfano mwaka 2005/06 bajeti ya Jeshi la Polisi ilikuwa shilingi bilioni 103.7 na  tumeiongeza mwaka hadi mwaka mpaka kufikia shilingi bilioni 334 mwaka 2012/13. Tutaendelea kuiongeza mwaka ujao wa fedha na miaka ijayo.  Tulipoingia madarakani tulianzisha program ya ujenzi nyumba bora za kuishi za askari, wakaguzi na maafisa wa Jeshi la Polisi.    Mpaka sasa ujenzi wa maghorofa 90 yanayochukua familia 360 umekamilika.  Programu hiyo ambayo inafanana na ile ya Jeshi la Ulinzi ilisimama kwa matatizo ya upatikanaji wa fedha ambayo tutayatafutia ufumbuzi. 
          Aidha, kuanzia mwaka huu tutaongeza uwekezaji kwenye kuboresha usafiri, zana na vitendea kazi katika Jeshi la Polisi.  Kazi itaenda sambamba na kuboresha maslahi na mazingira ya kuishi na kufanya kazi.
Ndugu wajumbe;
          Kwa maneno mengine napenda kuwaambia tutaendeleza na kazi kubwa tuliyoianza na tunayoendelea kuitekeleza ya kuboresha utendaji wa Jeshi la Polisi.  Kimsingi lengo ni kulifanya jeshi lila kisasa.  Hayo ndiyo maudhui na malengo ya Programu ya Maboresho ya Jeshi la Polisi ya Miaka Mitano (2010/2011-2014/2015). Programu hii mliibuni na kuitayarisha wenyewe.  Sisi Serikalini tulipoletewa mapendekezo yenu tuliyapokea kwa mikono miwili na Baraza la Mawaziri lililofanyika tarehe 31 Machi, 2011 liliupitisha Mpango huo. 
          Sote tuliunga mkono nia njema ya kutaka Jeshi la Polisi liwe la kisasa na lenye watendaji wenye weledi wa hali ya juu na walio tayari kushirikiana na jamii kuzuia uhalifu.  Hivyo nawapongeza kwa kuanza kutekeleza Programu hiyo japokuwa kuna changamoto za hapa na pale. Nawaahidi kuwa tutaendelea kutoa fedha zetu hata kuomba mikopo na misaada. 
          Pamoja na hayo, nawaomba mtupie macho kutoa mafunzo mahsusi kwa uendelezaji wa rasilimali watu hususan katika taaluma  ambazo mnao watu wachache au hawapo kabisa.  Mpango huo pia uwe na mapendekezo ya namna ya kuimarisha vyuo vyetu vya ndani ikiwa ni pamoja na kuboresha mitaala, vifaa vya kufundishia na uwezo wa wakufunzi. Tuvifanye vyuo vyetu kuwa vya kisasa ili vikidhi mahitaji ya sasa na ya baadae.
Mafunzo yanayotolewa yalenge kuwaanda maofisa na askari kutumia zaidi sayansi na teknolojia katika utendaji wao.  Lazima Jeshi la Polisi liende na wakati. Hakuna namna tunaweza kukwepa. Hivyo lazima mafunzo yaweke msisitizo kwenye matumizi ya sayansi na teknolojia. Matumizi hayo yanakuwa na maana zaidi katika kipindi hiki ambacho nchi yetu ina Mfumo wa Taifa wa Usajili na Utambuzi wa Watu niliouzindua tarehe 7 Februari 2013. Mfumo huu utarahisisha sana kazi ya Jeshi la Polisi kama mtautumia ipasavyo.   Mimi nina imani kuwa tukiimaarisha mafunzo, Jeshi la Polisi litafanya makubwa kuliko ilivyo sasa.
Malalamiko dhidi ya Jeshi la Polisi
Inspekta Jenerali wa Polisi;
          Naomba muongeze bidii kupambana na utovu wa maadili ili tupunguze kunyoshewa kidole kuhusu tuhuma za rushwa na kasi ndogo ya upelelezi wa makosa. Hili la rushwa nimelisema mara nyingi, lakini kutokana na umuhimu wake leo narudia tena kulisema. Tuhuma za rushwa zinachafua sifa nzuri ya Jeshi letu. Nafahamu kuwa sio wote katika Jeshi la Polisi wanaojihusisha na vitendo vya kuomba na kupokea rushwa. Jeshi lina maofisa na askari wengi ambao ni waadilifu na wachapa kazi wenye uzalendo wa kweli kwa nchi yetu. Lakini waswahili wana msemo usemao: “nazi mbovu harabu ya nzima”.
          Maana yake ni kuwa askari wachache wasiokuwa waadilifu wanaweza kuharibu sifa ya wengi walio wazuri.  Najua na ninyi jambo hili linawakera.  Hivyo naomba viongozi muweke uzito unaostahili kwa masuala ya uadilifu na uaminifu wa askari na maofisa wa Jeshi la Polisi. Wekeni utaratibu mzuri wa kupokea na kushughulikia maoni na malalamiko ya wananchi. Msiwaonee muhali wale wataobainika, miongoni mwenu, kujihusisha na vitendo vya rushwa.
          Pamoja na vitendo vya kuomba na kupokea rushwa, Jeshi la Polisi linalalamikiwa na wananchi kwa kuendesha upelelezi wa kesi za jinai kwa kasi ndogo.   Kwa sababu hiyo, kesi zilizoko mahakamani zinachukua muda mrefu kumalizika kuliko inavyostahili.  Nawaomba, mlitafutie ufumbuzi wa haraka suala hili.  Mimi nilidhani tulipotenganisha shughuli za upelelezi na uendesha mashtaka ingesaidia.  Inaelekea bado.  Nawasihi Maafisa, Wakaguzi na askari waliopangiwa kufanya kazi za upelelezi kuifanya kazi hiyo kwa ufanisi na kasi inayokubalika kisheria.  Mkifanya hivyo mtasaidia kupunguza moja ya kero kubwa na ya muda mrefu ya msongamano wa mahabusu magerezani.
Ushirikiano uimarishwe
Ndugu wajumbe;
          Nawapongeza sana kwa kuwashirikisha wananchi kwa karibu katika kupambana na uhalifu.  Tafadhali dumisheni na kuendeleza falsafa ya ulinzi shirikishi.  Ni muhimu sana na ni jawabu sahihi kwa uhaba wa polisi nchini. Uwiano wa askari polisi na raia ni 1:1,184 wakati ule unaokubalika kimataifa ni 1:450. Lakini hata kama tungekuwa na uwezo wa kuongeza ukubwa wa Jeshi la Polisi na kufikia au kukaribia uwiano unaofaa, lisingeweza kupambana na uhalifu bila kushirikiana na wananchi na vyombo vingine vya dola na jamii kwa ujumla. Hivyo ni vyema kuimarisha ushirikiano uliopo baina ya Jeshi la Polisi na wananchi na  vyombo vingine vya dola kwa ujumla. Aidha tujenge uwezo wa wadau wengine wanaosaidia kuelimisha jamii kutii sheria bila shuruti. Hawa tuwape muongozo sahihi wa namna ya kufanya nao kazi. Watakuwa mtaji mkubwa katika mapambano dhidi ya uhalifu nchini.
          Vilevile hatuna budi kuimarisha ushirikiano uliopo kati yetu na taasisi mbali mbali za kanda na za kimataifa zinazojihusisha na mapambano dhidi ya uhalifu kama vile Inter-pol, “East African Police Chiefs Cooperation Organisation (EAPCCO)” na “Southern African Regional Police Chiefs Cooperation Organisation (SARPCCO)”. Taasisi hizi zinasaidia sana na zitaendelea kufanya hivyo katika kupambana na uhalifu wa kimataifa kama vile biashara ya madawa ya kulevya na uharamia. Bila ya kuwa na ushirikiano mzuri, Jeshi letu peke yake haliwezi kupambana na kushinda uhalifu wa namna hiyo.




Mwisho
Mheshimiwa Waziri;
Inspekta Jenerali wa Polisi;
Makamanda na viongozi wakuu  wa Jeshi la Polisi;
Ndugu wajumbe;
Mabibi na Mabwana;

Kwa kumalizia napenda kuwapongeza wale wote walioshiriki kuandaa mkutano huu kwa kazi nzuri waliyofanya. Nawaomba wajumbe wote wa mkutano mkitoka hapa mkatekeleze kwa vitendo kwenye mikoa na maeneo yenu yale mtayokubaliana. Sisi tunawaombea kila la heri na mafanikio katika kutekeleza majukumu yenu mazito na muhimu kwa taifa letu na watu wake.
Baada ya kusema hayo  sasa ninayo furaha kutamka kuwa Mkutano Mkuu wa Maofisa Waandamizi wa Jeshi la Polisi wa mwaka 2013 nimeufungua rasmi. Nawatakia Mkutano mwema na wenye mafanikio.
Asanteni kwa kunisikiliza.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top