Ally Mohamed Kileo (kushoto) akiwasilisha utafiti wake ambao umebaini kuwa mawasiliano hafifu baina ya bodi ya mikopo elimu ya juu na wanafunzi ni chanzo cha migomo na migogoro isiyokwisha vyuoni. Upande wa kulia ni Mwalimu  Dominicus Makukula kutoka UDSM,Shule ya Uandishi wa Habari na Mawasiliano ya Umma SJMC aliyeambatana naye wakati wa uwasilishaji.
Mwalimu  Dominicus Makukula(kulia)  kutoka UDSM,Shule ya Uandishi wa Habari na Hawasiliano ya Umma SJMC  akifafanua jambo wakati wa uwasilishaji,kushoto ni Mtafiti Ally Mohamed Kileo

  1. Utangulizi
Utafiti huu ulifanyika kama sehemu muhimu ya kukamilisha masomo yangu ya stashahada ya juu katika kozi ya mawasiliano ya umma inayotolewa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Nilipanga kuhitimisha masomo yangu kwa kufanya kitu ambacho kingejenga na kuimarisha wasifu wangu nikiwa msomi katika fani ya mawasiliano lakini pia kufanya kitu ambacho kinatoa mchango wa moja kwa moja katika maendeleo ya nchi yangu.

Katika miaka ya hivi karibuni, kuanzia mwaka 2000 na kuendelea jamii yetu ya Watanzania imeshuhudia migogoro mingi kati ya wanafunzi wa elimu ya juu hasa vyuo vikuu na serikali katika upatikanaji wa mikopo ya kugharamia masomo. Upatikanaji wa mikopo umekuwa kero kubwa na lawama nyingi zikielekezwa katika ufanisi mdogo au mapungufu ya kiutendaji ya Bodi ya Mikopo. Wanafunzi ambao daima waliona au kuhisi kutotendewa haki na serikali katika upatikanaji wa mikopo, kwa kupitia vyama na serikali zao vyuoni wamekuwa wakifanya migomo na maandamano ya mara kwa mara ambayo yameleta hasara na madhara makubwa katika kufanyika kwa shughuli za kimasomo vyuoni. Wakati mwingine vurugu hizi zilizusha vitendo vya uvunjifu wa amani na uharibifu wa miundombinu na samani za taasisi walizosajiliwa kufanya masomo. Tumeshuhudia mara kadhaa kati ya mwaka 2005 hadi 2011 wanafunzi katika Chuo Kikuu kikongwe cha Dar es salaam wakifanya migomo iliyosababisha vurugu na hatimaye chuo kufungwa huku wanafunzi wakisimamishwa kwa muda na kurudishwa baadae kumalizia masomo yao. Wengine walifikishwa mbele za vyombo vya dola kwa makosa yatokanayo na madai ya mikopo kupitia migomo hiyo pamoja na wale waliofukuzwa kutoka chuoni moja kwa moja. Migogoro kati ya Bodi ya Mikopo na Wanafunzi wa Elimu ya Juu imechangia kwa kiasi kikubwa kudumaa kwa maendeleo ya elimu ya juu hasa katika utekelezaji wa shughuli za kimasomo. Mihula ya masomo huvurugika na kuwanyima walimu na wanafunzi muda wa kutosha kufanya shughuli za kujifunza na ufundishanaji na zaidi kuyafanya mazingira ya vyuo kukosa utulivu na amani kwa shughuli za kimasomo. Bodi kuna wakati imetumia gharama kubwa na nguvu nyingi kukabiliana na matokeo ya madai ya wanafunzi badala ya kuchunguza kiini cha tatizo na kulimaliza kwa usahihi na wakati.

Utafiti huu maalum ulilenga katika kuchunguza matatizo ya msingi yanayoikabili Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu hasa katika eneo la mawasiliano kupitia teknolojia ya intaneti katika kuwahudumia wadau wake wakuu yaani wanafunzi (wakopaji), na mwishowe kutoa mapendekezo ya kitaalamu ili kuiwezesha Bodi kutoa huduma bora zaidi. Matatizo yaliyochunguzwa zaidi katika utafiti yalikuwa katika mawasiliano wakati wa maombi ya mikopo ya karo na gharama za shughuli za kimasomo hasa fedha kwa ajili ya kufanyia utafiti na mafunzo kwa vitendo.

Baada ya kuzichunguza na kuzichambua taratibu na shughuli za kiutendaji za kila siku za Bodi ya Mikopo, utafiti huu uligundua kuwa matatizo ni mengi na yote yalianza katika mfumo mbovu wa mawasiliano ambao daima ulisababisha kuibuka kwa migogoro mikubwa kati ya Bodi, Taasisi za Elimu ya juu (vyuo vikuu) na wakopaji, yaani wanafunzi wa vyuo vikuu na hatimaye kufanyika migomo na maandamano ya mara kwa mara.

1.      A.  Dhana au Kanuni Zilizotumika Katika Utafiti

Utafiti huu uliongozwa na kanuni mbili za utafiti ambazo ni:

1.                          Njia au chombo cha kutolea habari huathiri maana na jinsi ujumbe wa mawasiliano unaotolewa na muwasilishaji
(Medium Theory ya McLuhan, 1967) na;
2.                          Kanuni au modeli ya mawasiliano ya Shannon na Weaver ya mwka 1949.

Dhana zote mbili zilitumiwa kwa kusudio la kumwezesha mtafiti kuchunguza jinsi na namna mawasiliano yalivyofanywa na pande zote mbili (1. Bodi ya mikopo- Mtoaji taarifa na mpokeaji na 2. Wanafunzi – watoaji taarifa na wapokeaji pia) katika mfumo wa mawasiliano wa Bodi ya Mikopo. Dhana ya kwanza ilitumika kama darubini katika kuhizihakiki njia au vyombo vya habari vinavyotumiwa na Bodi ya Mikopo kama vinafaa kubeba ujumbe unaokusudiwa na kuwawezesha walengwa wa mawasiliano kuelewana. Mtafiti alizitumia kanuni hizi kuangalia usahihi wa ujumbe, njia ya mawasiliano (chombo cha habari, kwa mfano : intaneti,  gazeti, radio, t.v n.k), changamoto katika kufanyika kwa mawasiliano     (“ noise”- visababishi vya kutokamilika kwa mawasiliano) na matokeo ya mawasiliano ( communication impact). Iwapo shughuli ya mawasiliano ilifanyika kwa kuzingatia kanuni na dhana sahihi za kitaalamu ilitarajiwa kuwa ni rahisi kwa pande hizi mbili za mawasiliano kufikia mwafaka kwa kila mmoja kujua nafasi yake na hata kuona na kuelewa kwa urahisi matatizo ya kimawasiliano yaliyojitokeza na kwa jinsi gani yangeliweza kutatuliwa au kusahihishwa kwa maelewano kati ya pande zote mbili bila mvutano usio wa lazima.

B. Methodolojia

1.         Muundo wa Utafiti

Utafiti huu ulifanyika katika misingi ya tafiti za taaluma ya sayansi ya jamii, na kuakisi methodolojia isiyo ya kitakwimu. Katika metholojia hii matokeo ya utafiti yametokana na ubunifu wa uchambuzi na tafsiri za mtafiti kutokana na data iliyokusanywa na sio taarifa ya kitakwimu iliyotokana na data moja kwa moja.


2.      Sampuli ya Washiriki Katika Utafiti.

Utafiti huu ulitumika sampuli wakilishi ya washiriki 45 ikiwa ni jumla ya wanafunzi 25 wa elimu ya juu, wafanyakazi 10 kutoka taasisi ya elimu ya juu na wafanyakazi 10 kutoka Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu nchini. Sampuli ya washiriki ilichaguliwa kwa kutumia mbinu inayojulikana kama “uchaguzi wa kupangwa au kwa upendeleo” (purposive sampling). Kati ya washiriki wote 45, washiriki 35 walichaguliwa kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam na 10 waliobakia walitokea Bodi ya Mikopo. Mtafiti aliona sampuli hii kwa tabia na idadi yake ilijitosheleza kutoa picha halisi ya malengo ya utafiti.

3.      Mbinu ya Ukusanyaji Data Katika Utafiti

Utafiti huu ulitumia mbinu mbili za ukusanyaji wa data, nazo zilikuwa ni;
  • Mahojiano ya uso kwa uso baina ya mtafiti na washiriki (moja baada ya mwingine kwa siri).
  • Washiriki wa utafiti kujaza hojaji au dodoso la utafiti lenye maswali ya wazi kumwongoza mshiriki kutoa mawazo, mtazamo na uelewa wake katika tatizo la utafiti kama alivyohojiwa.

4.      Uchambuzi wa Matokeo ya Utafiti

Taarifa za utafiti au matokeo ya utafiti yaliainishwa kwa kutumia maswali mawili ya utafiti yaliyohoji: 1. Ni aina gani ya mfumo wa mawasiliano unatumiwa na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu? 2. Kwa jinsi gani mfumo wa mawasiliano wa Bodi ya Mikopo unasaidia au kuathiri huduma za Bodi kwa wadau wake?. Maswali haya yalifafanuliwa na kurahisishwa katika maswali madogo manne ili kuwawezesha washiriki kuyajibu kwa ufasaha kupitia dodoso la utafiti. Katika hatua iliyofuata, majibu ya washiriki katika madodoso yote 45 yaliyochambuliwa, kuainishwa na kupangiliwa katika maudhui yaliyofafanuliwa na kuelezea tatizo la utafiti na kuwasilishwa katika mjadala na majedwali yenye kutoa takwimu fupi za matokeo ya utafiti.

  1. Matokeo ya Utafiti

Utafiti uligundua kuwa tatizo kuu ni mfumo wa mawasiliano wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya juu ya Tanzania. Japokuwa, Bodi ya Mikopo imejiwekea utaratibu wa kutumia njia au vyombo mchanganyiko katika kufanya mawasiliano na wadau wake, bado matatizo ya kimawasiliano yamekuwa makubwa na kusababisha shida nyingi baina ya wadau wa Bodi.

Asilimia 55 (washiriki 25) ya washiriki wote 45 (100%) katika utafiti walisema kuwa, matumizi ya intaneti, vipeperushi, matangazo ya kubandikwa, matangazo ya redioni na katika televisheni kama njia za mawasiliano bado hazijaiwezesha Bodi kutoa au kufanya shughuli za mawasiliano vizuri na kwa wakati baina yake na wadau wake katika kutoa huduma sahihi na kwa haraka. Katika kuchunguza matumizi ya mtandao wa intaneti kama chombo kikuu cha mawasiliano (jambo ambalo limechukua nafasi kubwa katika utafiti huu), mtafiti aligundua mapungufu makubwa zaidi kama inavyoainishwa hapo chini:

  1. Kukosekana  kwa ubunifu na matumizi madogo  ya njia ya mawasiliano ya intaneti
Washiriki 13 wote kutoka  Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambapo 3 ni  wanafunzi  wanaoendelea na masomo, 9  wanafunzi wapya na kiongozi  mmoja kutoka umoja wa  wanafunzi DARUSO (Dar es Salaam Students Organization ) walisema, kuna  matatizo  katika matumizi ya njia  ya mtandao wa intaneti kwani hawakuona  tofauti kati ya  tovuti ya Bodi  na bango au tangazo la kubandikwa. Washiriki walisema walitarajia  tovuti hiyo kusheheni  taarifa nyingi, sahihi na za kina katika kumwezesha mdau (mwombaji)  wa Bodi  ya Mikopo kupata taarifa zote na kukidhi mahitaji yake awapo  mtandaoni bila kulazimika kwenda  Bodi ya Mikopo kwa  ajili ya shughuli hiyo hiyo.

  1. Urasimu usio wa lazima

Vilevile, washiriki 25 wote wanafunzi wa Chuo Kikuu   cha Dar es salaam, kati yao wakiwemo viongozi 5 wa DARUSO, wanafunzi  10 wanaoendelea  na masomo ya juu na 10 wapya (waliotarajia kujiunga na Chuo kikuu  cha Dar es salaam) walilalamikia mlolongo  wa taratibu  zilizowekwa ili mwombaji wa mkopo kufanikisha usajili wake katika Bodi. Kutokana na utaratibu  mbovu wa utunzaji wa kumbukumbu za watu katika mfumo  mzima wa elimu wa Tanzania, Bodi imeweka  urasimu mgumu wakati wa kuzipata  taarifa  za mwombaji mpya. Utaratibu wa Bodi  unahusisha  vyombo au taasisi zisizosaidia kwa  namna  yoyote  ile  kumtambulisha mwombaji  kwa usahihi; Kwa mfano, katika hili  unatolewa  katika  kipengele cha ithibati ya serikali  ya mtaa anaoishi mwombaji inayohitajika ili kumtambulisha mwombaji  kwa Bodi.

  1. Kuchelewa  kwa majibu ya maswali au maelezo yatokanayo na zoezi la usajili

Katika hili, washiriki 25 wote wanafunzi  wa chuo kikuu cha Dar es Salaam, kati yao  wakiwemo, viongozi 5 wa DARUSO, wanafunzi 10 wanaoendelea  na masomo na  10 wapya waliotarajia kujiunga  na Chuo Kikuu cha Dare s salaam  walisema, walitegemea mtandao  wa intaneti ungelirahisisha upatikanaji  wa huduma za Bodi ya Mikopo na badala yake hawaoni tofauti  yoyote kati ya matumizi ya matumizi ya mtandao wa intaneti  na mfumo  wa zamani  wa taarifa /mawasiliano  kufanyika kupitia mbao za  matangazo za Bodi na chache zilizopo  katka Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Viongozi wa DARUSO walibainisha kuwa maswali yao kuhusu taratibu za utoaji wa mikopo panapotokea ucheleweshwaji, Bodi huchukua muda mrefu kujibu toka muda ule mdau anapouliza. Vilevile, hata taarifa muhimu juu ya upatikanaji wa mikopo hazipatikani kwa wakati zinapohitajika kulingana shughuli za kimasomo chuoni. Wanafunzi 7 wanaoendelea na masomo walisema hawakuwahi kujibiwa maswali yao waliyouliza kupitia anuani ya baruapepe iliyowekwa mtandaoni wala kupatiwa au kutumiwa taarifa walizoomba kupitia tovuti ya Bodi ya Mikopo.

  1. Kukosekana kwa uwazi na ukweli katika  mchakato wa kupanga mikopo

Utafiti ulionyesha katika tatizo hili tovuti ya Bodi ya Mikopo imepoteza maana zaidi kwa kushindwa kutumika kwa ufanisi uliotarajiwa. Washiriki wote 25 wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika utafiti huu walisema kuwa, hili ni moja katika matatizo makubwa yanayoonyesha utendaji wa Bodi unayokosa haki, ukweli na uwazi kwa waombaji. Washiriki wa utafiti walisema ingekuwa rahisi sana Bodi kuonyesha matokeo ya mwombaji na madaraja ya mikopo wanayopangiwa wadau kupitia mtandao wa intaneti kuliko ilivyokuwa siku za nyuma. Teknolojia ya intaneti ingeiwezesha bodi kuainisha mchakato wote wa upangaji na utoaji wa mikopo kwa uwazi mkubwa huku kila mwombaji na  sifa zake zikionekana na kupatikana kwa urahisi mtandaoni, lakini jambo hilo halifanyiki kwa kuzingatia teknolojia tuliyonayo na ubabaishaji bado unandelea kujitokeza. Hapa mtafiti alitia shaka (observe) kuwa, inawezekana bado Bodi ya Mikopo inakosa wataalamu wa teknolojia ya mtandao katika mawasiliano ya Umma pamoja na vyombo vyake.

5. Kukosekana kwa ushirikiano katika mawasiliano kati ya Bodi ya Mikopo na wadau wake

Mwishowe, washiriki wote 45 (100%) walikubali kuwa Bodi ya Mikopo haitumii mtandao wa mawasiliano katika njia inayowakutanisha na wadau wake kwa wakati (interactivity). Mtafiti aliona tatizo hili kuwa ni la kiufundi zaidi na hivyo kubainisha mawazo ya washiriki walioona kuwa bado Bodi ya Mikopo inaendelea kutumia njia moja ya mtiririko wa mawasiliano (Linear communication) isiyoshirikisha (kinyume na matarajio ya matumizi ya mtandao wa intaneti) walengwa katika mchakato wa mawasiliano pindi taarifa/mawasiliano yanapofanyika, na hivyo kufanya yasitimie kwani panakosekana mrejesho (Feedback) baina ya wanamawasiliano kwa wakati. Mrejesho katika mawasiliano ungelikamilisha shughuli ya mawasiliano mara moja iwapo pande mbili za mawasiliano zingeshirikishwa kupitia mtandao kama vile kuchati (instant messaging) au kuwapo kwa kitengo cha mawasiliano ya simu cha huduma kwa wateja (Student Call Centre) kama ilivyo katika huduma za makampuni ya simu za kiganjani.

Hitimisho
 Kwa ufupi sana utafiti huu umegundua kukosekana kwa taaluma, wataalam na maana sahihi ya matumizi ya mtandao wa intaneti katika shughuli za Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Katika nchi zilizoendelea na zinazoendelea kwenye teknolojia ya utoaji wa mikopo ya elimu kwa kutumia mtandao wa inteneti kama Afrika ya Kusini na Botswana shughuli zinazotuchukua muda wa siku mbili sisi Watanzania, wao huwachukua masaa machahe kuzikamilisha. Utafiti huu pia ulibaini sio tu uzembe wa watendaji katika vitengo mbalimbali vya Bodi vimefanya huduma za Bodi hiyo kuwa duni na mbaya, lakini pia kukosekana kwa nia ya dhati ya kuboresha huduma za Bodi ya Mikopo kunafanya zoezi zima la matumizi ya mtandao wa intaneti kutoa huduma kuwa kama mchezo wa kuigiza usio na waigizaji wala watazamaji sahihi. Ni changamoto kubwa kwetu wasomi wa fani mbalimbali zenye mahusiano na shughuli za Bodi ya Mikopo kutoa michango endelevu na kuikosoa Bodi ili  kuiwezesha kuona kwa sawasawa nafasi na wajibu wake katika kufanya kazi zake muhimu sana kwa Tanzania yetu ya leo.


Mapendekezo

Kutokana na matokeo ya utafiti kama ulivyofanyika na kutoa matokeo yake, mtafiti aliona ni vyema kupendekeza yafuatayo ili utafiti huu usiwe ni sehemu ya kubomoa bali ni mchango mkubwa katika kujenga na kuimarisha shughuli za Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Tanzania hususani katika kipengele cha mawasiliano ya intaneti kama yalivyoorodheshwa hapo chini;

  • Bodi ya Mikopo iimarishe na kuboresha huduma za mtandao wa intaneti kwa kuongeza taaluma ya mawasiliano ya umma kwa watendaji wake katika zama hizi za utandawazi.
  • Bodi ya Mikopo ijenge kituo cha mawasiliano ya huduma kwa wateja kwa njia ya simu na intaneti itakayopatikana kwa masaa ishirini na nne kwa gharama za mtumiaji wa huduma hiyo. (A Student call centre- for receiving and transmitting a large volume of requests by telephone/online).
  • Bodi ianzishe akaunti za wateja mtandaoni ambazo zitaruhusu wadau wote wa eneo la mikopo ya elimu ya juu kuweka na kutoa taarifa na data nyingine muhimu zinazohitajika bila urasimu wowote kwa Bodi na wakopaji.
  • Bodi ipunguze idadi ya washiriki katika mchakato wa usajili wa waombaji kwa kuwasiliana na Mwombaji, Tanzania Commission for Universities (TCU), Vyuo husika vya waombaji na Baraza la Mitihani tu kwa kutumia mtandao wa intaneti.

Ahsanteni sana kwa kunisikiliza

MUNGU IBARIKI TANZANIA, MUNGU IBARIKI AFRIKA!

Ally Mohamed Kileo
Post Graduate Diploma in Mass Communication, 2011 (SJMC-UDSM).
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top