Bunge maalumu la katiba linaloendelea mjini DodomaChama cha Demokrasia  na Maendeleo- CHADEMA kimesisitiza kwamba bunge maalum la katiba linaloendelea na vikao vyake mjini dodoma si halali ingawa lipo kisheria kutokana na kukosa maridhiano na muafaka wa watanzania  wanaohitaji katika mpya.
Akizungumza jijini Dar Es Salaam, Jumanne Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA bara, bwana John Mnyika amesema bunge hilo maalum la katiba limekuwa likiendeshwa kwa kukiuka sheria huku mwenyekiti wake akiliongoza kwa kuweka suala la kukusanya maoni tena kinyume na maoni ya wananchi yaliyokusanywa na tume ya mabadiliko ya katiba  na wakichakachua pia baadhi ya kanuni zilizowekwa awali



Amewataka watanzania na Umoja wa katiba ya Wananchi-UKAWA kuendelea kupinga bunge maalum la katiba lisifike kwenye hatua ya upigaji wa kura ili kuepuka kupata katiba iliyo kinyume na maoni ya wananchi na kwamba mikutano, migomo na maandamnao bado inaratibiwa katika sehemu mbalimbali nchini  ambapo kila mkoa unatarajiwa kufanya kwa utaratibu wake.

Jumatatu Bunge maalum la katiba lilipitisha azimio la kufanyia marekebisho kanuni za upigaji kura  ambapo sasa kanuni hizo zitaruhusu wajumbe kupiga kura hata wakiwa nje ya ukumbi wa bunge hilo maalum.

Kupitishwa kwa mabadiliko hayo ya kanuni kumekuja baada ya kamati ya kanuni na haki za bunge kuwasilisha mapendekezo hayo pamoja na ufafanuzi wa mwenyekiti wa bunge maalum la katiba bwana Samwel Sitta, kuwa lengo ni kuwawezesha wajumbe walio nje ya ukumbi kupata haki ya kupiga kura na kazi ya kutunga katiba iliyopendekezwa iweze kukamilika ndani ya muda uliopangwa kisheria.
VoaSwahili
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top