ZIKIWA zimebakia siku mbili kabla ya serikali kuanza kuwatoza
kodi ya laini (sim card) watumiaji wa simu, Taasisi ya Watumiaji wa
Bidhaa na Huduma imefungua kesi Mahakama Kuu kupinga sheria hiyo.
Taasisi hiyo ya Consumers of Goods and Services Across the Country
ilifungua kesi hiyo juzi Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam chini ya
hati ya dharura na kuanza kusikilizwa jana mbele ya jopo la majaji
watatu.
Majaji waliosikiliza kesi hiyo ni Lawrence Kaduri, Aloysius Mujuluzi na Salvatory Bongole.
Katika kesi hiyo walalamikaji wanaiomba mahakama itangaze kwamba
sheria iliyopitishwa na Bunge inayotaka kila mtumiaji wa simu ya
mkononi kukatwa sh 1,000 kila mwezi ni kandamizi.
Walidai kwamba watumiaji wengi wa simu za mkononi hawana uwezo wa
kukatwa fedha hiyo kwa mwezi, huku wakisisitiza kuwa itawaathiri
watumiaji wa huduma hiyo.
Kwa mujibu wa madai ya walalamikaji hao, sheria hiyo inakiuka matakwa
ya katiba ya nchi ya uhuru wa kupashana habari na kuiomba mahakama
kuifuta sheria hiyo waliyoiita kuwa kandamizi.
Mawakili wa walalamikaji kutoka Kampuni ya uwakili ya Rex, Lugano
Mwandamo na Merkizedeki Lutema walidai kuwa wateja wao wanataka
mahakama imzuie Waziri wa Fedha kupitia Mamlaka ya Mapato (TRA) kutoza
kodi hiyo hadi hapo maombi yao yatakapotolewa uamuzi.
“Kuanzia sasa hivi mahakama itoe amri ya muda kuzuia utekelezaji wa sheria hiyo usitendeke,” alidai Mwandamo.
Kutokana na maombi hayo, jopo la majaji liliahirisha kesi hiyo hadi
Oktoba 3 mwaka huu, likimtaka wakili wa serikali, Kelley Mwitasi
kuwasilisha maelezo yake kwa njia ya maandishi.
Wakati huo huo, majaji hao waliutaka upande wa walalamikaji kujibu
maelezo ya upande wa serikali kwa njia ya maandishi na kuyawasilisha
mahakamani hapo kabla ya Oktoba 7, ambapo kesi hiyo itaanza kusikilizwa
saa saba mchana siku hiyo.
Kufunguliwa kwa kesi hiyo kutasitisha utekelezaji wa utozaji wa kodi
hiyo unaotakiwa kuanza Septemba 30 mwaka huu, baada ya TRA kuziandikia
kampuni za simu waraka wa kuzitaka zianze utekelezaji wa sheria hiyo.
Sheria hiyo iliyopingwa na wanasiasa wengi bila kujali itikadi za
vyama vyao, ilipitishwa kwa nguvu ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) wakati wa Bunge la Bajeti na kutaka utekelezaji wake uanze Julai
30.
Bunge kupitia Kamati ya Bajeti inayoongozwa na Mbunge wa Bariadi
Magharibi, Andrew Chenge (CCM) lilitaka kuwapo kwa kodi hiyo ili
kusaidia shughuli za bajeti ya serikali kuu.
Kupitishwa kwa kodi hiyo kuliibua malalamiko ya wanasiasa hata wa CCM
dhidi ya Chenge anayelazimisha kuwapo kwa kodi hiyo, huku akishindwa
kuamini kwamba kuna Mtanzania anayekosa sh 1,000 kwa mwezi kwa ajili ya
laini ya simu.
Malalamiko hayo, yalimlazimu Rais Jakaya Kikwete kukutana na wadau wa
mawasiliano ambao ni wamiliki wa kampuni za simu Tanzania (MOAT),
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na
Waziri wa Fedha, William Mgimwa, kisha kuwaagiza waiondoe kodi hiyo.
“Nakuombeni kaeni pamoja, wekeni bongo zenu pamoja, wekeni akili yenu
pamoja tutafute namna gani tutajaza pengo hili la sh bilioni 178
endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha wananchi mzigo mzito na
kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni ngumu,” alisema rais
kwenye kikao hicho.
Licha ya agizo la rais kutekelezwa kwa MOAT kutakiwa kuongeza kodi
nyingine iitwayo ‘Excise duty’ kutoka asilimia 14 hadi 17 bila kujali
kwamba katika Bunge la bajeti kodi hiyo iliongezwa kutoka asilimia 12
hadi asilimia 14, kodi ya laini za simu haijaondolewa.
Wachambuzi wa masuala ya siasa na mawasiliano walisema kutojadiliwa
kwa mabadiliko ya kodi hiyo ya simu ni dalili kwamba Waziri wa Fedha
amezidiwa nguvu na kiti cha spika kinachounga mkono hoja hiyo ya Chenge
na kushindwa kutekeleza agizo la rais.
Takwimu zilizotolewa na kampuni za simu zinaonyesha kuwa miongoni mwa
wamiliki wa laini za simu milioni 22; milioni nane wanatumia chini ya
sh 1,000 kwa mwezi.
0 comments:
Post a Comment