Dk. Salim Ahmed Salim
WAZIRI Mkuu mstaafu Dk. Salim Ahmed Salim, amevionya vyombo vya dola kuwa matumizi ya nguvu dhidi ya wananchi ni kiashiria cha uvunjifu wa amani.

Dk. Salim ameeleza masikitiko yake kuhusu uwepo wa viashiria vya uvunjifu wa amani, zikiwemo kauli za viongozi na kuitaka jamii kupambana navyo kwa kudumisha misingi ya amani ambayo ni upendo, kuheshimiana na kuvumiliana.

Mwanadiplomasia huyo wa kimataifa alisema hayo Dar es Salaam jana alipozungumza na Tanzania Daima Jumatano wakati wa kongamano la kutafakari amani ya nchi lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD).

Kauli ya kiongozi huyo mashuhuri Afrika ilikuja baada ya kutakiwa kutoa maoni yake kuhusu kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda aliyoitoa hivi karibuni bungeni, akiwaruhusu askari polisi kuwapiga wananchi aliodai wanavunja sheria.

Pinda alitoa kauli hiyo siku chache baada ya bomu kutupwa kwenye mkutano wa CHADEMA wa kumalizia kampeni za uchaguzi mdogo wa madiwani mjini Arusha kwenye Uwanja wa Soweto.

“Mimi nadhani nguvu ya dola siku zote itumike kwa maslahi ya wananchi… wakati mwingine mazingira yanakuwa magumu mtu anaudhika, lakini kitu muhimu popote pale duniani nguvu ya dola isipotumika kwa maslahi ya wananchi itavuruga amani.

“Tujifunze kwamba bila amani, bila utulivu hakuna kinachofanyika. Vurugu katika jamii ni mbaya, hebu tujifunze kwa nchi za wenzetu zinavyovurugana… amani ni kitu muhimu kwa familia zetu, watoto wetu na jamii nzima.

“Lazima tuheshimiane, tumefika kama kisiwa cha amani kwa kuheshimiana, tusibaguane, tupambane na viashiria vya uvunjifu wa amani,” alisisitiza Dk. Salim aliyepata kuwa balozi wa Tanzania kwenye nchi mbalimbali.

Aidha, alionya matumizi ya nyumba za ibada yanayofanywa na baadhi ya wanasiasa nchini na kusema si vema kupeleka siasa, huku akitaka viongozi wa dini na wanasiasa watimize wajibu wao kila mmoja kwa nafasi yake bila kuingiliana.

Naye Mkurugenzi wa Maendeleo ya Vijana wa Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, Profesa Elisante ole Gabriel aliwataka viongozi wa dini kutoshabikia siasa na kuwaonya viongozi wanaopeleka siasa kwenye nyumba za ibada.

“Viongozi wa dini watambue nafasi yao katika kudumisha amani bila kushabikia,” alisema mkurugenzi huyo na kuongeza kwamba wanapofanya hivyo wanaashiria uvunjifu wa amani kwa sababu dini na siasa ni mambo tofauti.

Gabriel alishauri kuwepo na mafunzo maalumu kwa wanasiasa ya jinsi ya kuzungumza jukwaani huku akisisitiza kwamba yanayotokea Tanzania na Afrika nzima ni matokeo ya kuingia kwenye mfumo wa vyama vingi bila kujiandaa kisaikolojia.

Alivitaja viashiria vya uvunjifu wa amani kuwa ni kutoaminiana kwa viongozi, wananchi na wanasiasa jambo linalowafanya kila mmoja kumlalamikia mwenzake.

“Tusibaguane ingawa kwa sasa ubaguzi upo kwenye siasa. Ipo siku tutabaguana dhahiri, naamini tofauti za kisiasa ni njia rahisi ya kupoteza amani yetu. Ubaguzi wa kidini na kikabila utatupeleka pabaya,” alisema.

Alishauri TCD iendelee kuwezeshwa kwa gharama yeyote ili kiwe chombo cha kuwakutanisha wanasiasa na serikali katika kuimarisha umoja, mshikamano na kuaminiana kwa mustakabali wa amani ya Tanzania.

Alichagiza kwamba upo uwezekano wa chama kingine kuingia madarakani, lakini sio kwa kukidharau chama kinachotawala huku akisisitiza kwamba uwezekano wa chama kimoja kukaa madarakani muda mrefu upo ila sio kutawala milele.

Naye Mwenyekiti wa TCD, James Mbatia, aliwataka wanasiasa wasijione muhimu zaidi kuliko Watanzania wengine, hivyo kila wanachokifanya lazima kiwe kwa maslahi ya wote.

Mbatia alisisitiza kwamba viongozi wa dini hawapendi kuona polisi wakiwalinda wakati wanawafundisha neno la Mungu waamini wao, hivyo kuwataka wanasiasa wasiwe chanzo cha vurugu nchini.

Naibu Katibu Mkuu Bara wa Chama cha Wananchi (CUF), Julius Mtatiro, alisema iwapo mifumo thabiti ya utoaji haki haijengwa na haki ikaonekana kutendeka, bado amani ya nchi itaendelea kuwa shakani.

“Hata TCD wakiitisha makongamano kama haya mara 10,000 wakajadili amani, kama viongozi wa serikali hawapo tayari kuiweka mifumo thabiti ya kuifanya haki itendeke na ionekane, hayo makongamano hayatafanikiwa.

“Watawala wanataka kuiendesha nchi kwa kubahatisha, jambo ambalo ni hatari kwa amani ya nchi badala yake wawe radhi kuweka mifumo imara ya kumwezesha kila mmoja kupata haki kwa wakati,” alisisitiza Mtatiro.

Kongamano hilo la siku mbili litamalizika leo. 
Chanzo: Tanzania Daima
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top