Mwanasheria wa Kenya, Dola Indidis  
Mwanasheria wa Kenya ameanzisha mchakato wa kupinga mateso na hukumu ya kifo kwa Yesu Kristo, akisema kwamba ilikuwa kinyume cha sheria na kwamba Israel na baadhi ya mataifa yanatakiwa kuwajibika.
Mwanasheria huyo, Dola Indidis (pichani) ambaye aliwahi kuwa msemaji wa Mahakama nchini Kenya amesema kwamba amefikisha shauri hilo kwenye Mahakama ya Kimataifa ya Haki (ICJ), International Court of Justice, iliyopo The Hague, Uholanzi.
Indidis katika mashtaka yake anahoji kesi isiyo ya haki dhidi ya Yesu, kifungo, adhabu na kifo chake.
Agosti 2007 alifungua kesi hiyo kwenye Mahakama Kuu ya Nairobi kwa niaba ya ‘Marafiki wa Yesu.’ Hata hivyo mahakama mwaka 2011 ilitoa uamuzi kwa kusema haina mamlaka na kumwomba mtoa maombi kwenda ICJ.
Indidis anataka ifahamike ni uhalifu gani alifanya Yesu hadi kufikia hatua ya kushtakiwa, na anaitaka mahakama itamke kuwa ‘mwenendo wa mashtaka dhidi ya Yesu haukufuata taratibu za kisheria kwa wakati huo na hata sasa.’
“Mahakama (ICJ) imewasiliana na mimi. Sasa nasubiri tarehe ya kwenda Uholanzi kusikiliza kesi hiyo,” alisema Indidis.
Indidis aliendelea kusema: “Nimefungua kesi hii kwa sababu ni jukumu langu kuenzi heshima ya Yesu na nimekwenda ICJ kutafuta haki kwa ajili ya mtu kutoka Nazareth. “Kesi hii siyo kwa masuala ya kilokole. Ni kuhusu sheria na ni jukumu la mahakama kusadia maendeleo ya sheria,” alisema Indidis.
Alisema amekwenda ICJ kuhoji hukumu aliyopewa Yesu, kwamba alihukumiwa kwa makosa na alituhumiwa bila kufanya kosa lolote.
Indidis alisema japokuwa walalamikiwa wengi kwa sasa ni marehemu, bado anaona uzito wa kesi na kwamba itaweka utaratubu kwa siku za baadaye.
Kesi hiyo kwa mara ya kwanza ilifikishwa Mahakama Kuu ya Kenya chini ya kifungu namba 65 na 67 cha Katiba ya Kenya (ambayo sasa imerekebishwa).
Walalamikaji katika kesi hiyo ni Marafiki wa Yesu kupitia kwa Dola Indidis, ambao wanawashtaki mtawala wa Roma Tiberius, Pontius Pilate (Pilato) ambaye ni Gavana wa Judea, Annas, Padri Mkuu wa Wayahudi, kiongozi wa Wayahudi, Walimu wa sheria wa Kiyahudi, Mfalme Herod, Jamhuri ya Italia na Taifa la Israel.
Kwenye kesi hiyo taasisi ya kiraia ya kutetea haki ya Kenya na Humprey Odanga Achala, wameorodheshwa katika sehemu ya watu wenye masilahi na kesi hiyo. Alisema ametumia kifungu cha Marafiki wa Yesu kwenye Agano Jipya kufungua kesi hiyo.

Walalamikaji wamezitaja nchi za Italia na Israel kwakuwa nchi hizo hata baada ya uhuru zimeendelea kutumia sheria za Utawala wa Roma na zile zilitotumika kumsulubu msalabani Yesu.
Padri Mkuu wa Wayahudi Caiaphas anatuhumiwa kumkamata Yesu, kumshtaki kwenye mahakama isiyo halali (Kangaroo Court), na kumtia hatiani kwa mashtaka ya kidini yaliyoangukia kwenye adhabu ya kifo na hakutaka Yesu ahoji mamlaka yake.
Alidai Pilato hakumtia hatiani Yesu, lakini alitoa hukumu ya kumuua ili kuleta amani.
“Haikuwa sahihi Pilato kushuhudia mtuhumiwa akipigwa,” alisema Indidis na kuongeza kuwa, “Jaji lazima alisimamie haki za watu wote na aina zote za ukiukwaji wa sheria.”
“Miongoni mwa waliokuwepo walimshambulia usoni, walimtemea mate, walimzaba vibao, walimdhihaki, na kumwona kuwa mtu anayestahili kifo,” alisema.
Mlalamikaji pia alihoji mfumo wa maswali yaliyotumika wakati wa kesi, uchunguzi, wakati kesi ikisilikizwa na hukumu kwa Yesu Kristo, adhabu alizokuwa akipewa wakati kesi ikiendelea na ukweli wa taarifa zilizotumika kumtia hatiani. Alisema kilichofanyika ni uvunjaji wa haki za binadamu. “Yesu alikuja duniani kama binadamu. Sasa hakupewa fursa ya kusikilizwa na hakuna aliyezungumza kwa niaba yake.”
Indidis alisema ametumia miaka 10 kuifanyia kazi kesi hiyo, ikiwamo kukusanya ushahidi kutoka kwenye Biblia. “Ushahidi wote umo kwenye kumbukumbu za Biblia, huwezi kuidharau Biblia,” aliongeza Indidis.
Alisisitiza kwamba hata baada ya Yesu kufa, haikutolewa nafasi yoyote kusikilizwa kwa rufaa ya aina yoyote, hivyo yeye ameamua kufanya hivyo akiwa kama ‘rafiki’.
Alizungumza kuhusu kesi hiyo, mmoja wa maofisa wa ICJ alisema mahakama hiyo haina mamlaka kuhusiana na kesi ya aina hiyo kwa sasa kwa kuwa inajihusisha zaidi na kesi baina ya nchi na nchi, hivyo ni vigumu kuishughulikia kesi ya aina hiyo.
Mwananchi 
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top