Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Dkt Hussein Mwinyi

 Waziri wa afya na Ustawi wa Jamii Dkt. Hussein Mwinyi  ameitaka bodi ya maabara binafsi za afya kuchukua hatua  kwa wale wanaokwenda kinyume na sheria ikiwepo  kusimamisha huduma na kuwapeleka mahakamani  wale watakaokaidi  sheria ya kuratibu huduma za maabara binafsi  za afya.
Dkt. Mwinyi ameyasema hayo leo alipokuwa akizindua bodi mpya ya maabara binafsi za afya .Alisema sheria hiyo iliyopitishwa na Bunge la Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania na kuanza kutumika mwaka 1998 ilikuwa na lengo la  kuboresha huduma za maabara  pamoja na kufanikisha utoaji wa huduma bora za afya nchini.
“Uboreshaji wa mabadiliko ya sekta ya afya ni vema ufanyike sambamba na uboreshaji wa huduma za maabara ikiwemo uzingatiwaji wa maadili ya utoaji wa huduma za maabara ili kuepuka athari zinazoweza kutokea kwa mtoa huduma au anayehudumiwa yaani mgonjwa”alisema
Aidha, aliitaka bodi hiyo kuratibu na kukagua majengo,vifaa,vitendanishi na kuhakikisha usahihi wa majibu ya vipimo ili kuleta ubora wa matokeo ya uchunguzi wa magonjwa pamoja na kutoa nafasi kwa wataalamu wa maabara kuanzisha huduma hiyo hapa nchini.
“Kazi ya bodi hii ni ya muhimu sana kwani utoaji wa huduma ya tiba haukamiliki iwapo hakuna huduma ya uchunguzi wa magonjwa,ikiwemo maabara,hivyo maabara inapofanya kazi zake kwa usahii,inampa nafasi nzuri mganga kuwa na usahii wa tatizo la mgonjwa na kutoa dawa inayostahili na kutuonesha umuhimu wa kuwa na wataalamu wazuri wa maabara”.
Hata hivyo Waziri huyo  ameitaka bodi hiyo kupitia na kufanya maboresho mapya ya sheria, kanuni na miongozo iliyopo ili iandane na mabadiliko yanayojitokeza na kuweza kusimamia na kusajili maabara zote nchini.
Awali akisoma  hotuba yake Mwenyekiti wa bodi hiyo Dkt. Magraret Mhando alisema bodi yake inatarajia kuhakikisha kuwa vifaa na vitendanishi vyote vinavyotumika nchini vina ubora unaokubalika na vimeorodheshwa katika orodha ya vifaa na vitendanishi vya maabara ya afya pamoja na kusajili na kuandikishwa maabara na maduka yote kwa mujibu wa sheria.
Bodi mpya ya maabara binafsi za afya inaundwa na wajumbe wapatao kumi inatarajia kumaliza muda wa utendaji wake kwa  miaka mitatu mwaka 2015.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top