Waziri Wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa


Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imelipa jumla ya madai ya walimu yenye thamani ya shilingi 554,390,879.67 kati ya tarehe 1 Julai na 30 Desemba, 2012. Malipo haya yamefanywa kwa walimu wa halmashauri za wilaya walio chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Wakufunzi, walimu, pamoja na wakaguzi wa shule wa Kanda na wilaya walio chini ya katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi. Malipo haya yamefanywa kwa kutumia hundi na si kwa kuingizwa moja kwa moja kwenye akaunti za wanaodai kama ilivyokuwa hapo awali. 

Ili kurahisisha zoezi la usambazaji/ugawaji wa hundi hizi kwa wahusika na kupata mrejesho wa haraka wa malipo hayo. Utaratibu ufuatao utafuatwa;

1.    Hundi za walimu walio katika Halmashauri za wilaya zitapelekwa kwa Katibu Tawala wa Mikoa husika ili Afisa Elimu wa Mkoa kusaidia kuzipeleka kwa wahusika;

2.   Hundi za wakufunzi na walimu walio katika Vyuo vya Ualimu zitapelekwa kwa wakuu wa vyuo vya ualimu husika;

3.   Hundi za wakaguzi wa shule wa kanda na wilaya zitapelekwa kwa Mkaguzi Mkuu wa Shule wa Kanda husika.

4.   Hundi za madai ya walimu ambayo kwa sasa ni mirathi zitapelekwa kwenye mahakama zilizofunguliwa mirathi hiyo.

Tunashauri wahusika wapewe hundi hizo ndani ya mwezi mmoja toka tarehe zilipopokelewa. Kwa hundi ambazo wahusika hawatakuwa wemejitokeza ndani ya mwezi mmoja ni vyema zikarejeshwa kwa katibu Mkuu, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

Kwa maelezo ya ziada, tafadhali wasiliana na Mhasibu Mkuu wa Wizara kwa namba za simu +255 22 2126828.



IMETOLEWA NA


KATIBU MKUU

WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI

10/01/2013

Chanzo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top