MAKAMU wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mohammed Gharib Bilal |
MAKAMU wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Mohammed Gharib Bilal, amewataka maofisa wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar kuwashirikisha kikamilifu wananchi ili waweze kuendeleza sekta ya utalii nchini na kufaidika nayo.
Hayo
ameyasema leo huko Nungwi Mkoa wa Kaskazini Unguja wakati wa ufunguzi
wa hoteli yenye hadhi ya nyota tano, iitwayo Gold Hotel.
Amesema njia ya kuwashirikisha wananchi itawafanya waweze kufaidika na matunda ya utalii hasa kupata ajira na kuongeza kipato.
“Mjiulize mnafaidika kwa kiasi gani katika utalii, vipi unachangia uchumi wa Serikali ya Zanzibar na Tanzania kwa jumla, lakini pia ni lazima utalii huu uchangie moja kwa moja kwa wananchi”, alisema.
Alisema
njia za kuwafaidisha wananchi ni kuwaajiri na kuwasomesha vijana elimu
ya utalii itakayowawezesha kuifanyia kazi katika mchanganyiko wa watalii
na wageni kiujumla.
Aidha
Dkt. Bilal alifahamisha njia za kulikuza soko la utalii nchini, akisema
kuna umuhimu mkubwa kuwasomesha watu wanaowatembeza wageni ili waijue
vyema historia ya Zanzibar na mazingira, na kwa hivyo waweze
kuwashawishi wageni kubakia nchini kwa muda mrefu.
Njia
nyengine, alisema ni pamoja na kuwafundisha namna ya kuwapokea wageni,
kuwashawishi kutumia pesa zao na kutoa miongozo ya kuleta sifa katika
mazingira ya visiwa vya Zanzibar na fukwe zake.
Dkt
Bilal alisema miongozo hiyo na mengine mingi, ni muhimu sana na endapo
itafuatwa, ni wazi kuwa soko la utalii litakua kwa kasi kubwa.
Aidha aliwaeleza viongozi wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA), wazingatie na kufikiria kwa makini kuwavutia
wengi wakiwemo wawekezaji wa ndani ili kuijengea sura nzuri Zanzibar
kwa kuchangia miji na vijji, na kuwataka katika uwekezaji huo waangalie
njia za kutunza silka na utamaduni wa Mzanzibari.
Makamu
wa Rais alifahamisha kuwa sekta ya utalii inakua kwa kasi kubwa duniani
na zaidi ya dola trilioni mbili za Kimarekani zinazopatikana katika
nchi nyingi hutokana na mchango wa utalii, ambao pia umeajiri watu
milioni 98 duniani kote.
Nae
Mkurugenzi Mtendaji wa ZIPA Salum Nassor, alisema mpaka sasa jumla ya
miradi 511 imeidhinishwa na mamlaka yake katika sekta mbalimbali, ambapo
wawekezaji wageni ni 340 na wenyeji 171.
Amesema
sekta ya utalii peke yake ina miradi 328 sawa na asilimia 64.19 ambapo
kati ya hiyo, wenyeji wanamiliki miradi 214 na wageni 114.
Mkurugenzi huyo alisema kufunguliwa kwa hoteli hiyo ni ishara ya mafanikio, kwani itaweza kuhamasisha sekta nyengine kama vile biashara, kilimo na uvuvi ambavyo vitapelekea kukua kwa uchumi wa nchi. Hoteli hiyo mpya yenye vyumba 66 inatarajia kuajiri wafanyakazi 200.
Mbali
na idadi hiyo ya vyumba vya wageni vya daraja mbalimbali, hoteli hiyo
ina kumbi kadhaa za mikutano, nyumba tatu zinazojitegemea (villa) ambapo
kila moja ina nyumba mbili.
0 comments:
Post a Comment