Frederick Sumaye 
Frederick Sumaye
WAZIRI Mkuu mstaafu Frederick Sumaye amewananga wanaomuita kuwa muasisi wa takrima akidai kuwa uelewa wao ni mdogo juu ya suala hilo.
 
Wiki iliyopita, Sumaye akiwa katika ibada ya harambee ya kuchangia ujenzi wa ukumbi wa Kanisa Katoliki Jimbo la Moshi katika Parokia ya Mawella, alidai kuwa uchaguzi wa sasa nchini umegubikwa na rushwa na vishawishi vingi badala ya kuzingatia ubora, uhodari na tabia ya anayesaka uongozi.

Kufuatia kauli hiyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamis Mgeja, alimjia juu Sumaye na kusema kuwa ni kama analamba matapishi yake mwenyewe kwa sababu ndiye aliasisi rushwa ya uchaguzi.

Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano jana kwa njia ya simu, Sumaye alisema kuwa ni upuuzi kwa wanaomuita muasisi wa sheria hiyo kwa kuwa Bunge ndilo lenye jukumu la kutunga sheria.

Sumaye alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Tatu sio muasisi wa sheria ya takrima kama inavyoelezwa, bali suala hilo lilianza miaka ya nyuma na ikalazimu kufanyiwa marekebisho na Bunge.

“Hii sheria ilitoka katika Local Government na kuja katika uchaguzi mkuu, na Bunge ndilo lililopitisha sheria hiyo, sasa kama kuna kikundi cha watu kinajitokeza na kuniita mimi muasisi, hao watakuwa hawana uelewa wa suala hilo,” alisema.

Alisema kuwa hata kupitia hotuba yake aliwahi kueleza kuwa sheria hiyo inapaswa isitumike vibaya, lakini hao wanaompinga juu ya rushwa ndio vinara wa kupindisha sheria hiyo.

Waziri Mkuu huyo mstaafu alisema kuwa nia ya Bunge kuweka sheria hiyo ilikuwa njema, lakini baadhi ya viongozi, hasa wanaowania nyadhifa mbalimbali ndio wanaoiharibu.

Sumaye alisema kuwa kutokana na sheria hiyo kuharibiwa, ni vyema Bunge likaangalia namna ya kuiondoa ili kuepusha chaguzi kutawaliwa na rushwa.

“Nafikiri uelewa wa wanaonipinga ni mdogo na hawana ufahamu kuhusiana na suala hilo, imefika wakati sasa kuona umuhimu wa kuiondoa sheria hiyo, hasa kwa Bunge ambao ni muhimili unaohusika na kutunga sheria kwani maana halisi ya takrima imeharibiwa,” alisema.

Alisema kuwa takrima ilikuwa ni lengo jema kwa kundi linaloshirikiana na mgombea kuweza kupewa chakula baada ya kumaliza kampeni na sio kumwaga fedha kama inavyojitokeza sasa.

Katika hotuba yake aliyotoa katika ibada hiyo, Sumaye alisema kiongozi hutafutwa na jamii husika kutokana na ubora wake na siyo vishawishi vyake.

“Kama nilivyokwishaeleza, uongozi hautafutwi kwa udi na uvumba wala kwa rushwa, bali anayefaa kuwa kiongozi hutafutwa na jamii husika kutokana na ubora wake na siyo vishawishi vyake.

Ni ukweli ulio wazi kuwa leo chaguzi zetu zimegubikwa na rushwa na vishawishi vingi na siyo ubora, uhodari wala tabia ya anayetaka nafasi hiyo ya uongozi,” alisema.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top