Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) wa zamani, Yusuf Makamba
*Apinga mawaziri kushambuliwa hadharani
KATIBU Mkuu Mstaafu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Yusuf Makamba, amekosoa mwenendo wa chama chake na kueleza kuwa kwa namna kinavyoendeshwa kinajipa wakati mgumu.

Akizungumza juzi na MTANZANIA Jumamosi, Makamba alisema kitendo cha viongozi wa chama hicho kuwataja hadharani baadhi ya mawaziri kwamba ni mizigo, si kizuri kwa maslahi ya chama hicho.

Makamba alifanya mahojiano maalumu na gazeti hili nyumbani kwake Wazo Tegeta, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam, ambapo pamoja na mambo mengine alizungumzia nafasi ya CCM kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

Akizungumzia hoja hiyo, Makamba alisema hatua ya chama hicho kuwataja hadharani baadhi ya mawaziri wasiowajibika ni kuvipa ajenda vyama vya upinzani na kwamba hiyo ni sawa na kujimaliza mbele ya wananchi.

Kauli ya Makamba inaonekana wazi kumpinga Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana na Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye ambao hivi karibuni walitaja hadharani majina ya mawaziri watatu kwamba ni mizigo.

Wakiwa katika ziara za kichama katika mikoa ya Mbeya, Ruvuma na Songea, Kinana na Nape waliwashukia mawaziri hao ambao ni Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chizza na Naibu wake, Adamu Malima.

Wengine waliotajwa na viongozi hao ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, kwamba kwa pamoja wameshindwa kutatua matatizo ya wananchi.

Makamba alisema, CCM itajijengea heshima iwapo itaendelea kuwa na utaratibu wa kutumia vikao vya chama kuwashughulikia mawaziri wasiotimiza wajibu wao badala ya kuwaumbua hadharani.

Kwa mujibu wa Makamba, hatua ya kuwaita mawaziri mizigo hadharani ilikuwa ni sawa na kujiumbua wenyewe na kukivunjia heshima chama hicho.

“Ndio maana chama kina vikao, kama waziri ni mzigo mwiteni katika vikao, kumsema hadharani ndio sipendi hata kidogo na tusemane kwenye vikao na si mahala pengine.

“Kumsema mwenzako hadharani siyo vizuri yule ana mke, anao watoto, anao ndugu zake, hawa wote hawapendi na hawataki, sifurahishwi kuwapigia kelele hadharani mnajiumbua wenyewe. Lazima tukijengee heshima chama.

“Haya ya kusemana hadharani si mazuri, chama kinakwenda kwenye uchaguzi 2015 mtawaeleza nini wananchi, hamuoni kwamba mtaonekana hamfanyi kazi?” Alihoji Makamba.

Katika mazungumzo hayo, Makamba aligusia uhusiano wake wa kikazi na baadhi ya wenzake katika chama na kusema mara nyingi alikuwa akisumbuliwa kutokana na kusema ukweli.

Bila kufafanua Makamba kwa sauti ya chini na ya huzuni, alisema ukweli umekuwa ukimsumbua kati yake na wenzake lakini amekuwa akiweka ushahidi kwa kila analolitamka au kulitenda.

“Nimekuwa nikipata shida kutokana na kusema ukweli. Ukweli unanisumbua sana kwa wenzangu, lakini inanibidi nikisema niweke ushahidi,” alisema Makamba bila kufafanua.

Makamba alisema CCM inaendelea kufanya kazi kubwa na nzuri ndani ya chama. “Kazi ya chama ndani ya chama ni vikao, wanachama kukutana na kushiriki katika vikao na viongozi pamoja na kulipa ada.

“Mimi ni mwanachama wa Tawi la Tegeta Kisanga, naalikwa katika vikao vya chama na vijana, hivi vinafanyika.

“Kazi ya chama ndani ya umma ndio hizi kazi zinazofanyika kujenga shule za msingi na sekondari, kupeleka maji kwa wananchi, barabara na uchukuzi na sisi ndio chama tawala tuliahidi katika manifesto,” alisema Makamba.

Ziara za akina Kinana

Hivi karibuni, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahaman Kinana aliripotiwa akiwa Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya akisema kuwa CCM imepoteza imani kwa wananchi kutokana na kukorogana kwa viongozi wenyewe kwa wenyewe.

Katika kikao na wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, Wilaya ya Rungwe, Kinana alisema CCM itachukua hatua za kuwawajibisha viongozi wakiwamo wa Serikali walioshindwa kuwajibika.

Akiwa Songea, Kinana alinukuliwa akimtaja hata aliyekuwa Waziri wa Fedha marehemu, Dk. William Mgimwa kuwa ni miongoni mwa mawaziri ‘mizigo’ na kuahidi kuwashughulikia katika Kamati Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akiwa Namtumbo mkoani Ruvuma, Kinana aliwataja Chizza na Malima kuwa tangu wateuliwe wameshindwa kutekeleza wajibu wao wa kuongoza wizara hiyo na hakuna hata siku moja waliyofika Ruvuma kushughulikia matatizo ya wakulima wa mazao ya tumbaku, mahindi na mpunga.

Nape pia alinukuliwa akimtaja, Dk. Shukuru Kawambwa akisema kuwa licha ya kushindwa kuongoza Wizara ya Elimu, lakini pia anatakiwa kuchukuliwa hatua kutokana na mkataba alioingia na wakandarasi wa ujenzi wa barabara ya kutoka Namtumbo hadi Tunduru mkoani Ruvuma.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula, amekuwa akinukuliwa na vyombo vya habari akikemea tabia ya baadhi ya viongozi serikalini kutowajibika.

Mbali na suala hilo, Mangula pia hivi karibuni alikemea tabia ya baadhi ya wanachama wa chama hicho ambao wameanza kutangaza nia ya kuwania nafasi mbalimbali ikiwamo urais, ubunge na udiwani kabla ya muda.

“Kuna baadhi ya wanachama wetu wanapita mitaani na kujifanya wanatoa misaada kama vile wafadhili, huku wakitangaza nia ya kuwania uongozi, hao ni waasi chama hakitawavumilia,” alinukuliwa Mangula.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top