Mbunge wa Jimbo la Msalala (CCM), Ezekiel Maige
WAPENDWA, Watanzania wenzangu. Nimetazama kwa mshangao na kutoamini kuhusu kilichojiri bungeni juzi.

Kwa bahati mbaya, binafsi sikuwepo niko Arusha kwenye mkutano wa Ushirika wa Wabunge wa Kamati za Mahesabu ya Serikali kutoka nchi za SADC (SADCOPAC) na nchi kadhaa za Afrika nje ya SADC.

Sikuona sababu kabisa ya kufikia hapo kwani hali hiyo ingeweza kuepushwa. Ingewezekana kabisa kuahirisha muswada na kutoa nafasi kwa Kamati ya Katiba na Sheria kwenda Zanzibar kupata maoni ya wenzetu wa huko.

Najua kuna maelezo mazuri ya kushirikishwa kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Lakini kikanuni, baada ya muswada kusomwa mara ya kwanza, unakuwa mikononi mwa Bunge na kamati ndiyo inayokusanya maoni si serikali! 

Kwa kuwa hakuna ushahidi wa public hearing kufanyika Zanzibar na kuwasikia Wazanzibari wa kawaida (nje ya serikali), basi kulikuwa na hoja kabisa ya kurekebisha kasoro hiyo kwa kutoa nafasi kwa kamati kwenda Zanzibar.

Suala la Katiba ni kubwa hivyo ni vema zikafanyika jitihada za kutosha kuhakikisha tunakwenda pamoja (na wenzetu hasa wenye mtazamo tofauti na sisi) badala ya kutumia wingi wetu kwani mwisho wa safari tukienda hivi wapo watakaodai Katiba mpya si yao na hivyo kuikosesha social legitimacy!

Kwa kiti kutomsikiliza KUB nako kulitibua mambo bila sababu. Angepewa nafasi ya kusikilizwa hata kama hoja yake isipokubaliwa ingekuwa nafuu sana na shari na aibu ya jana ingeepukika!

Tumesameheana, lakini tujifunze na tujitahidi sana kwenda kwa maelewano.

Mungu ibariki Tanzania.

Ezekiel Maige ni
Mbunge wa Msalala (CCM).
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

1 comments:

Denny said... September 8, 2013 at 12:26 PM

Siipendi CCM ila kwa hili ulilolisema mh. Maige nimekukubali na umeonyesha ni kwa jinsi gani ulivyo na uelewa mpana wa mambo. Barikiwana uzidi kuwa kiongozi mtenda haki na usiyekuwa mbaguzi.

 
Top