Na Azimio Sote

Serikali imesema msimamo wa serikali kuanzisha  tozo ya kodi katika laini za simu hautabadilika kutokana na ulazima wa kupata fedha kwa ajili ya kuunganisha umeme maeneo ya vijijini ambako bado watu wengi wanaishi bila umeme.

Hayo yalisemwa jana na Waziri Mkuu wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda alipokuwa akihutubia wananchi na viongozi mbalimbali kwenye mkutano uliofanyika katika viunga vya Halmashauri ya Manispaa ya Songea.

Mizengo Pinda alisema kuwa kodi ya laini imewekwa mahususi ili kukusanya fedha ambazo zitatumika katika kuunganisha umeme kwenye maeneo mengi hususani ya vijijini ambayo kwa sasa hayana umeme jambo ambalo alisema linakwamisha jitihada za wananchi kujiletea maendeleo ambapo alisema kila mtumia laini ya simu atapaswa kulipa kodi ya shilingi elfu moja kwa mwezi.

Aidha, Pinda aliwashangaa watu wanaopinga tozo hii akidai kuwa ni ndogo kwa kuwa ni sawa na kutoza shilingi therathini kwa siku kiasi ambacho kiko chini sana ikilinganishwa na matumizi ya kawaida kama kuvuta sigara ambapo alisema kuwa suala la tozo katika laini linatokana na shinikizo la wabunge kuitaka serikali itafute vyanzo vya mapato vitakavyotumika kusambazia umeme maeneo ya vijijini.

“Serikali ilielekezwa bungeni kuwa itafute vyanzo vyoyote vile kupata umeme vijijini…tukakaa tukaangalia tukaona ni vema wananchi wachangie shilingi 1000 katika kila laini kiasi ambacho kitaiwezesha serikali kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 160 kwa ajili ya umeme vijijini”, alisema Pinda.

Hivyo, waziri Pinda akasisitiza kuwa serikali itaendelea kukusanya kodi katika laini za simu hata kama wananchi watalalamika lakini mwishoni lazima watalazimika kuelewa tu.

Awali Naibu waziri wa Nishati na Madini Steven Maselle alipata wakati mgumu alipojaribu kuwaeleza wananchi haja ya kukusanya kodi kwa kila laini ya simu ambapo wananchi waliguna kwa nguvu kuashiria kuwa hawakubaliani na kauli hiyo jambo lililomfanya Waziri Pinda alitolee ufafanuzi zaidi.


Uhusiano wa Tanzania na Malawi.
Akizungumzia suala la uhusiano wa Tanzania na Malawi Waziri Mkuu Pinda alisema kuwa kimsingi serikali ya Tanzania haina nia wala sababu ya kuingia vitani na Serikali ya Malawi kwa kuwa suala lililopo linaweza kupata ufumbuzi bila ya kuingia vitani ambapo alisema kuwa kwa sasa suala hili limepelekwa katika Jumuiya ya Nchi za Kusini Mwa Afrika (SADC) kwa usuluhishi ambako Marais wawili wastaafu wamepewa jukumu la usuluhishi wa tatizo hili.

Kwa upande mwingine Waziri Pinda alisema ikiwa SADC hawatafanikiwa kupata suluhisho na serikali ya Malawi ikaamua kwenda katika mahakama za kimataifa Tanzania iko tayari kwenda kujitetea kwa vile haioni wapi ilipoteleza.

“Hata wakipeleka suala hili katika mahakama ya Kimataifa tuko tayari kupeleka wanasheria wetu waliobobea tutakwenda kujieleza vizuri kwani hatuoni tulipokosea,” alisema Pinda.

Hata hivyo alionya kuwa ikiwa atatokea mtu, kwa sababu zake mwenyewe, akaamua kuivamia Tanzania nchi haitakuwa na budi kujitetea kwa kupambana naye kwa vile uwezo wa kupambana upo ambapo alitolea mfano wa kilichomkuta Idd Amin wa Uganda.

Vilevile Mizengo Pinda alisema kuwa kuna tatizo la miundombinu ya mawasiliano eneo la mwambao mwa ziwa Nyasa ambako wananchi wanakosa taarifa za vyombo vya habari vya Tanzania na badala yake wanapata kiurahisi zaidi taarifa za Malawi fursa ambayo Pinda  alisema inaweza ikawa inatumika vibaya kwa kuwapotosha wananchi wanaoishi pembezoni mwa ziwa Nyasa ambapo aliahidi kulipatia ufumbuzi tatizo hili kwa kufunga mitambo itakayowezesha wananchi hawa kupata taarifa za habari kama kawaida.

Suala la Ujangili
Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema kuwa serikali inasikitishwa na tabia ya watu kujihusisha na ujangili katika mbuga za taifa ambapo alisema hayo yanafanyika zaidi mkoani Ruvuma katika mbuga ya wanyama ya Selous ambapo aliwashangaa watu wanaojua uwepo wa ujangili na wanawajua watu wanaofanya ujangili lakini wanasema hakuna ujangili wakati wanyama wanazidi kuangamia.

Ndipo Pinda akasema kuwa serikali imejipanga kuhakikisha kuwa majangili yanasakwa popote yalipo, kunakamata na kufikishwa katika vyombo vya sheria ambapo alisema kuwa kwa sasa serikali imeanzisha oparesheni uhai inayolenga kunusuru viumbe hai vyote na inakusudia pia kupambana na majangili na ujangili nchini ingawa alikiri kuwa hadi sasa oparesheni hii bado haijaanza kufanya kazi.

Vilevile Waziri Pinda alikemea tabia ya vyombo vinavyohusika na kutoa silaha kwa wamiliki binafsi ambapo alivitaka kuhakikisha kuwa silaha zinatolewa kwa sababu na idadi maalumu ili kupunguza idadi ya watu wenye kumiliki silaha ambazo baadhi huishia kutumika katika ujangili.


TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top