HARAKATI za Jeshi la Polisi kuishinikiza CHADEMA kuwasilisha ushahidi unaolituhumu jeshi hilo kuhusika na mlipuko wa bomu mkoani Arusha hivi karibuni na kuua watu wanne zimechukua sura mpya.

Jeshi hilo limemuamuru Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kuwasilisha ushahidi unaohusu bomu lililolipuka katika mkutano wa chama hicho uliofanyika viwanja vya Soweto, jijini Arusha Juni 15, mwaka huu.

Ingawa polisi imeendelea na harakati hizo, tayari CHADEMA walishakataa kuutoa ushahidi huo kwa polisi bali wanataka Rais Jakaya Kikwete aunde tume huru ya kijaji itakayosikiliza shauri hilo.

Tanzania Daima Jumapili limefanikiwa kupata nakala yake yenye kumbukumbu ya jalada, AR/IR/6223/2013 ya tarehe 17, Julai 2013.
Barua hiyo inamtaka Mbowe apeleke vielelezo kwa mujibu wa kifungu namba 10 (2) na (2A) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai.

Barua hiyo imesainiwa na Kamishna Msaidizi wa Polisi, Hussein Laisseri, kwa niaba ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai.

“Kutokana na mahojiano uliyofanya na Polisi Mkoa wa Arusha mnamo Juni 20, 2013 kuhusu mauaji yaliyotokana na ulipuaji wa bomu huko Soweto, Arusha ulidai kuwa unao ushihidi unaobainisha wahusika wa tukio hilo.

“Kwa mujibu wa kifungu cha 10 (2) na (2A) cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai nchini, sura 20 kama ilivyorekebishwa mwaka 202, unaamriwa kufika Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai tarehe 23 Julai, 2013 saa 8 mchana bila kukosa na ulete ushahidi huo, unatahadharishwa kuwa kushindwa au kukataa kufika na kuleta ushahidi huo ni kosa la jinai chini ya sheria iliyotajwa,” inaeleza sehemu ya barua hiyo.

Tanzania Daima Jumapili liliwasiliana na baadhi ya wanasheria wa CHADEMA ambao hawakutaka kutajwa majina yao, wamesema kitendo cha polisi kumshinikiza Mbowe kupeleka ushahidi huo ni kuingilia mchakato mwingie wa kisheria.

Walisema kuwa tayari CHADEMA wamepeleka maombi kwa Rais Jakaya Kikwete ili aunde tume huru ya kijaji ambayo mpaka leo hajajibu ombi hilo.

Walibainisha kuwa jeshi hilo wamekosea utaratibu kisheria na kuingilia suala ambalo tayari lipo katika mchakato.

“Haiwezekani kuingilia mchakato mmoja wa kisheria kwa kutumia mchakato mwingine wa kisheria, hii ni sub judice,” alisema mmoja wa mawakili.

Wakili huyo alisema hatua ya Jeshi la Polisi nchini kudai ushahidi wa bomu la Arusha kwa nguvu ni ya kushangaza na hawajapata kuitumia kushinikiza masuala mengine.

“Jeshi hilo halijawahi kumlazimisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwataja wauza dawa za kulevya, licha ya kusema majina anayo, hadi sasa hajayaweka hadharani,” alisema. 

Kauli ya Slaa
Barua hiyo inakuja siku chache baada ya Jeshi la Polisi kumuita na kumhoji kwa maelezo ya onyo kuhusiana na uchochezi Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe.

Hata hivyo Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alipinga hatua ya polisi kumhoji Mbowe kuhusu ushahidi wa Arusha kwa madai kuwa alichokifanya mwenyekiti wao, huo si msimamo wake bali wa chama.

Dk. Slaa aliweka wazi kuwa kamati kuu ya chama hicho iliamua kuwa ushahidi huo usiwasilishwe polisi kwa sababu ni watuhumiwa katika suala hilo.

“Mbowe hajasema hatatoa ushahidi, atatoa lakini si kwa polisi, tunataka tume huru ya kimahakama ya kijaji, ambayo inapaswa kuundwa na rais, sasa rais hajasema hataunda, Jeshi la Polisi linapoanza kulazimisha ninashindwa kuelewa uwezo wa polisi katika uelewa wa sheria.

“Tumewaeleza polisi kuwa hatutawasilisha ushahidi wetu kwao kwakuwa kwanza sisi tunaamini kuwa wao ni watuhumiwa namba moja,” alikaririwa Dk. Slaa.

Dk. Slaa aliongeza kuwa polisi hawakupaswa kumshika Mbowe bali kamati kuu iliyoamua kutoutoa ushahidi huo kwa polisi.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top