Waziri wa Madini na Nishati, Profesa Muhongo

Wasomi kutoka vyuo vikuu mbalimbali duniani wameilaumu Serikali ya Tanzania kwa kushindwa kulinda rasilimali zake kwa manufaa ya Watanzania na badala yake imekalia sera za kikoloni zinazochochea uporaji wa rasilimali hizo.

Wakizungumza katika tamasha la tano lililoandaliwa na Kigoda cha kitaaluma cha Mwalimu Nyerere katika Ukumbi wa Nkrumah wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam jana, wasomi hao walisema Serikali imekumbatia sera mbovu zinazoruhusu uporaji huo.

Akichambua ripoti za ‘A golden Opportunity; How Tanzania is failing to benefit from gold mining ya mwaka 2008 na The One Billion Dollar Question; How can Tanzania stop losing so much tax revenue’ ya mwaka 2012, Profesa John Saul kutoka Chuo Kikuu cha York cha Toronto, Canada ameitaja Kampuni ya African Barrick Gold kuipunja Tanzania katika mgawo wa madini.

“Kampuni ya African Barrick Gold ni adui wa Tanzania, ripoti hizi ukizisoma zinaonyesha uporaji wa rasilimali ya madini. Hata viongozi wa dini walishatembelea migodi hiyo wakajionea,” alisema Profesa Saul akiwa na nyaraka za ripoti hizo.

Profesa Saul aliyewahi kufundisha UDSM kati ya mwaka 1965 hadi mwaka 1972, aliilaumu Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wawekezaji wanaopora rasilimali za Tanzania.

“Tuliwahi kumtuma mtu wetu kuchunguza uporaji wa rasilimali, Serikali ikamfutia kibali cha kuishi nchini,” alidai Profesa Saul na kuongeza: “Kushindwa kukusanya kodi maana yake fedha kidogo ndiyo inakwenda kwenye shughuli za maendeleo. Inakadiriwa kuwa Tanzania hupoteza mapato yatokanayo na kodi kati ya Sh1.35 hadi 2.05 trilioni kwa mwaka.”

Akijibu tuhuma hizo, Waziri wa Madini na Nishati, Profesa Muhongo alisema Tanzania haiwezi kubakia kuwa taifa la kulaumiana bali watu wanatakiwa kufanya vitendo. “Profesa wa fani ipi? Sidhani kama analo jipya lolote kwani huo ndiyo wimbo wake. Sijui kama hapo ndiyo tamati yake?”
Mkurugenzi wa African Barrick Gold, Deo Mwanyika alizipinga ripoti hizo... “Huo siyo ukweli.

Ni upotoshaji mkubwa. Huyo Profesa anatumia ripoti ya kiharakati ambayo siyo sahihi. Mbaya zaidi hiyo ripoti kwenye mambo ya kodi iliegemea zaidi kwenye kazi ya Alex Stewart Asseyar Report (ASA).”

Alisema kampuni hiyo (ASA), haikuaminika na Serikali kutokana na kutokuwa wazi kiasi cha kufikishwa mahakamani huku Bunge likikataa mkataba wake usirudiwe.
“Kama mtu anasema tumeipunja Serikali, kuna mamlaka moja tu ya kuyasema hayo, nayo ni TRA (Mamlaka ya Mapato Tanzania) yenye mamlaka kisheria,” alisema Mwanyika.

Malalamiko haya yamekuja siku chache baada ya Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe kudai kuwa Serikali inakosa Dola 885 milioni (Sh1.5 trilioni) kutokana na kampuni za madini kukwepa kodi. Akihutubia mkutano wa hadhara huko Shelui mkoani Singida, Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu ya Bunge, alizituhumu kampuni hizo kuwa zinatumia mwanya wa kutoa mchanganuo wa ununuzi, ambayo siyo wa kweli ili kukwepa kodi.

Awali, akitoa mada ya Miaka 50 ya Uhuru wa Afrika, Profesa wa Maendeleo ya Afrika katika Shule ya Uchumi ya Uingereza, Thandika Mkandawire alisema Afrika bado haijajikomboa katika miaka yote hiyo.

Alitaja changamoto nne zilizoikabili Afrika baada ya kupata uhuru kuwa ni ubinafsi uliosababisha vita vya wenyewe kwa wenyewe, ukoloni mamboleo, umaskini na mgawanyiko wa matabaka ya walionacho na wasionacho.

Chanzo:Mwananchi
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top