MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (CHADEMA), amesema kitendo cha wabunge kufungwa mdomo kujadili ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kitaligeuza Bunge hilo kuwa kibogoyo.

Kauli ya Zitto imekuja muda mfupi baada ya Ofisi ya Bunge mjini Dodoma kutoa ratiba ya vikao vyake ambavyo vinaanza leo, ikionyesha ripoti ya CAG itawasilishwa bungeni, lakini haitajadiliwa kama ilivyozoeleka.

Alisema kutojadiliwa kwa ripoti hiyo, kutaendelea kutoa mianya ya ulaji ambayo tayari ilikuwa imeanza kuzibwa kutokana na ripoti hiyo kujadiliwa kwa kina na wabunge kama ilivyokuwa mwaka jana.

“Nina jibu moja tu, kutojadili ripoti ya CAG, sasa Bunge limekuwa kibogoyo. Kila siku nguvu za Bunge zinazidi kupungua.

“Ulaji utaendelea kwa kutojadili kwa uwazi taarifa ya CAG, wananchi wakatae Bunge kibogoyo,” alisema Zitto.

Lakini habari za kuaminika zilizopatikana mjini Dodoma jana na kuthibitishwa na Ofisi ya Bunge, zinasema ripoti ya CAG ambayo huwasha moto mkali katika utendaji kazi hasa wa mawaziri, itawasilishwa bungeni Ijumaa ya wiki hii.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Habari, Deogratius Igidio, alisema ripoti hiyo haitajadiliwa kutokana na mabadiliko ya ratiba ya vikao vya Bunge.

Alisema Bunge, linatimiza sheria inayotaka ripoti hiyo kuwasilishwa bungeni kila Aprili ya kila mwaka na kwamba kutojadiliwa kwake kunatokana na mabadiliko ya ratiba ya Bunge na kuwataka Watanzania waelewe hivyo.

“Sheria inataka taarifa ya CAG iwasilishwe Aprili, kutokana na mabadiliko ya ratiba ya Bunge ambapo mfumo mzima wa bajeti umebadilika, inatuwia vigumu kuijadili taarifa hii.

“Taarifa ya CAG, ikishawasilishwa kwa Rais, anatoa idhini iletwe bungeni, lakini mabadiliko ya bajeti ya Serikali, haitajadiliwa, bali itawasilishwa tu kama ambavyo ripoti nyingine za mwaka huu, zinavyowasilishwa bila kujadiliwa.

“Siwezi kusema lini itajadiliwa, ila hapa katikati baada ya kumalizika kwa mkutano huu, lazima kutakuwa na mikutano miwili kabla ya Bunge la Katiba, watakaopanga ratiba watazingatia hilo,” alisema Igidio. Kwa mujibu wa ratiba hiyo, leo Bunge linatarajia kupitisha Azimio la Marekebisho ya Kanuni za Kudumu.

Siku ambayo ripoti hiyo itawasilishwa itakuwa ni siku ambayo mjadala wa hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, utakuwa ukiendelea kujadiliwa.

Kesho Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, atasoma hotuba ya ofisi yake, itahusisha wizara tatu na itajadiliwa kwa siku tano.

Wizara ambazo zimo ndani ya hotuba hiyo, ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, Ofisi ya Waziri Mkuu, Uwekezaji na Uwezeshaji na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Baada ya wizara hiyo, hotuba za wizara nyingine zitafuatia na Bajeti ya Serikali itakayosomwa Juni 13, mwaka huu saa 10 jioni, siku ambayo nchi zote za Jumuiya ya Afrika Mashariki zatasoma bajeti zao.

Baada ya kusomwa kwa bajeti hiyo, kutakuwa na siku ya mapumziko kabla ya wabunge kuijadili kwa siku saba. Bunge linatarajiwa kuahirishwa Juni 28, mwaka huu.

Itakumbukwa mwaka jana, moto uliowashwa bungeni na wabunge kuibana Serikali, baada ya kuwasilishwa kwa ripoti ya CAG, uliwalazimu mawaziri wanane kutakiwa kupima uzito wa makosa yao na kufanya maamuzi, ikiwa ni pamoja na kutakiwa kujiuzulu.

Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, alitoa wito kwa wabunge wote kujiorodhesha kwa nia ya kupata saini za wabunge 71 ambao wangewasilisha kutimiza matakwa ya kisheria kupata asilimia 20 ya wabunge kwa ajili ya kumuondoa Waziri Mkuu.

Kutokana na hali hiyo, mawaziri kadhaa walimwandikia Rais Jakaya Kikwete, kwa ushauri wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ili kuiokoa Serikali ya chama hicho isianguke kutokana na mpango wa wabunge kujiorodhesha kutaka kumuondoa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.

Waliotakiwa kuondoka, ni Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami, Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu, Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, Waziri Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI0), George Mkuchika, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Jumanne Maghembe na Waziri wa Afya, Dk. Hadji Mponda.

Lakini baadhi ya walisakamwa na walijitetea hawahusiki kwa lolote na mambo wanayotuhumiwa nayo, huku baadhi wakiona mambo ni mazito na kusubiri panga la Rais.
Chanzo: Mtanzania

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top