Waziri Mkuu wa sasa, Mizengo Pinda akizungumza na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa.

RIPOTI ya tume iliyoundwa na Waziri Mkuu aliyejiuzulu, Edward Lowassa mwaka 2006 kuchunguza ujenzi wa maghorofa katika Jiji la Dar es Salaam, imemweka mahala pabaya na inaweza kumtoa kafara, Waziri Mkuu wa sasa, Mizengo Pinda, Tanzania Daima Jumatano limedokezwa.

Pinda anatolewa kafara katika sakata la jengo la ghorofa 16 lililoporomoka katikati ya Jiji la Dar es Salaam wiki iliyopita na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 40.

Kutokana na janga hilo, Pinda analalamikiwa kukalia ripoti ya Tume ya Lowassa ambayo ilikuja na mapendekezo ya kukabiliana na maghorofa yaliyojengwa chini ya kiwango.

Duru za siasa kutoka ndani ya Bunge zinasema kuwa tayari kuna baadhi ya wabunge bila kujali itikadi zao, wameunganisha nguvu kutaka kumsulubu Waziri Pinda katika mkutano ujao wa Bunge kupitia hoja binafsi au maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu.

Mmoja wa mawaziri waandamizi wa serikali ambaye aliomba jina lake lihifadhiwe, alisema: “Pinda anastahili kubeba mzigo, kwani baada ya kukabidhiwa ripoti hiyo alimwajibisha nani tangu 2008 hadi sasa?

“Kwa uzembe huu, Pinda ameshiriki kwa kuwa hakuwawajibisha waliojenga kinyume na utaratibu hadi Watanzania wengine wakafa. 

Zamu hii hata akilia anahusika.” Mbunge wa Vunjo Augustino Mrema (TLP) alimshangaa Waziri Pinda kwa kushindwa kuchukua hatua zilizopendekezwa na tume ya Lowassa kwani ilipendekeza baadhi ya majengo yabomolewe na wahusika wachukuliwe hatua.

Alisema athari ya ukimya huo ni kuendelea kuangamia kwa Watanzania kunakosababishwa na uzembe wa viongozi wa serikali.

“Hili tatizo la kushindwa kuchukua uamuzi mgumu litaendelea kutugharimu kila siku, yale maghorofa yaliyotakiwa kubomolewa kipindi kile hayajaguswa na hayataguswa kwa sababu ya kubebana, hili hatuwezi kulinyamazia, lazima tukawashe moto bungeni,” alisema Mrema.

Alisema Watanzania hawapo tayari kuletewa danganya toto ya tume nyingine ikalete majibu ambayo tayari yako mezani kwa Pinda.

Mbunge wa CCM aliyeomba jina lake lihifadhiwe, alisema kitendo cha Jeshi la Polisi kuwakamata watendaji wa Manispaa ya Ilala hakitoshi kama Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ataendelea kubaki ofisini.

Mrema ambaye amepata kuwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Ndani kwa nyakati tofauti, alisisitiza kuwa Waziri Tibaijuka anapaswa aige mfano wa Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi na Lowassa walioamua kuachia ngazi kutokana na uzembe wa watendaji wao.

“Kwa wenzetu leo inapotokea boti ikazama kwa uzembe na kupoteza maisha ya watu watatu waziri mwenye dhamana anawajibika, iweje sisi leo tuwachekee mawaziri wetu?” alihoji mbunge huyo.

Mbunge wa kuteuliwa na rais, James Mbatia, ameapa kuwasha moto katika Bunge lijalo hadi kieleweke.

Mbatia ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, alisema lazima Waziri Mkuu atoe majibu ya msingi kwa Watanzania kwanini hakutekeleza maazimio ya tume ya Lowassa.

Alienda mbali na kuhoji utendaji wa kitengo cha maafa cha Waziri Mkuu kwani kimekuwa kikishughulika kutoa vyakula vya misaada kwenye maafa badala ya kudhibiti yasitokee.

“Tangu tume zianze kuundwa kuhusu maafa ni akina nani walichukuliwa hatua? Kuanzia tume ya MV Bukoba hadi tume ya matokeo ya kidato cha nne, Watanzania tumechoka kuneemesha mifuko ya wajumbe wa tume na kufilisi rasilimali zetu, hivyo Pinda, Tibaijuka lazima wajiuzulu,” alisema.

Wakati wabunge hao wakitaka Pinda na Tibaijuka waachie ngazi, habari zaidi ndani ya serikali zinasema kuwa ripoti ya Tume ya Lowassa haikufanyiwa kazi kwani baadhi ya majengo yaliyopendekezwa kubomolewa, yanawahusu viongozi wa juu serikalini.

“Ile ripoti iliwasilishwa wakati Lowassa bado yuko madarakani. Alishindwa kuifanyia kazi na haiwezi kufanyiwa kazi kwani baadhi ya majengo yanawahusu viongozi au yanamilikiwa na watu wa karibu wa viongozi, na ndio wachangiaji wakubwa wa fedha wakati wa kampeni,” kilisema chanzo chetu cha habari.

Akifanya majumuisho katika hotuba ya matumizi ya ofisi yake bungeni kwa mwaka 2008/09, Pinda alizungumzia jinsi Tume ya Lowassa ilivyofanya kazi katika sakata la ghorofa kuanguka jijini Dar es Salaam.

Pinda alilithibitishia Bunge kuwa zaidi ya maghorofa 100 jijini Dar es Salaam yalibainika kuwa yalijengwa kinyume na taratibu za ujenzi.

Kwa mujibu wa ripoti iliyoundwa na Lowassa, kati ya maghorofa 505 ambayo waliyakagua, 147 yalikutwa hayana nyaraka za ujenzi.
Lowassa aliunda tume baada ya jengo la hoteli ya Chang’ombe Village Inn, Keko, Dar es Salaam kuanguka mwaka 2006 na kuua mtu mmoja na kujeruhi wengine kadhaa. Ilidaiwa kwamba ulikuwapo ukiukwaji katika ujenzi wake.

Pinda aliliambia Bunge kuwa tume hiyo ya Lowassa ilibaini pia maghorofa 81 yalikutwa yamekiuka masharti ya ujenzi huku mengine 22 wenyewe hawakupatikana na yalikuwa yamejengwa bila kuzingatia sheria za ujenzi pamoja na uzembe wa baadhi ya watendaji wakiwamo wahandisi wa manispaa husika. 

NHC yatoa kauli
SHIRIKA la Nyumba la Taifa (NHC) limesema kuwa mbia wao alikuwa na vibali vya mamlaka zinazohusika kusimamia ujenzi wa majengo makubwa vya kumruhusu kuongeza ghorofa 16 kutoka kumi za awali.

Kauli hiyo inakuja kukiwepo na mvutano kutoka mamlaka mbalimbali ikiwemo Manispaa ya Ilala kwamba mbia wao huyo ambaye ni M/s Ladha Construction alipewa kibali cha kujenga ghorofa kumi, lakini cha kushangaza aliongeza nyingine sita bila taarifa na hivyo kusadikiwa kuwa huenda ndiyo chanzo cha kuanguka kwa jengo hilo.

Mkurugenzi Mtendaji wa NHC, Nehemiah Mchechu akizungumza jana na waandishi wa habari jijini Dar es Salaa, alisema Agosti 22 mwaka jana mbia wao huyo aliwataarifu kuwa ameshapata vibali kutoka mamlaka husika, na kwamba angependa aingie nao mkataba mdogo kutambua ongezeko la ghorofa hizo na mabadiliko ya tarehe ya kumaliza mradi.

“Shirika lilimjibu kuwa hakuna pingamizi kama mbia ataleta nakala ya vibali kutoka mamlaka husika kwa ajili ya kumbukumbu za shirika na pia ili kufikia hatua za maamuzi ya ndani na mawasiliano yote hayo yapo kwenye rekodi zetu na endapo mamlaka husika itazihitaji tuzazipatia,” alisema.

Kutokana na hali hiyo, aliutaka umma kutoliingiza shirika hilo katika sakata hilo kwa madai kuwa zipo taasisi na vyombo vinavyokasimiwa mamlaka ya kusimamia ubora wa ujenzi wa nyumba nchini, na NHC nayo husimamiwa na taasisi na vyombo hivyo.
Chanzo: Tanzania Daima
 Picha kwa hisani ya mtandao.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top