Tanzania imelitaka Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa kuendelea kuunga mkono mikakati na juhudi mbalimbali zinazolenga katika kurejesha amani ya kudumu katika eneo la Mashariki ya Jamhuri ya  Kidemokrasia ya Kongo. Wito huo umetolewa na Balozi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa
Mataifa Tuvako Manongi, wakati akichangia majadiliano ya wazi kuhusu operesheni za kulinda amani na ujenzi wa amani na maendeleo.
 

Majadaliano hayo yaliyofunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, yameandaliwa na Pakistani, nchi ambayo ni Rais wa Baraza hilo kwa mwezi huu wa Januari. Katika mchango wake, Tanzania imeeleza bayana kuwa, hali iliyojitokeza mwezi Novemba mwaka jana huko Goma DRC, ni kielelezo na ushuhuda wa dhahiri kwamba juhudi na mikakati mbadala ya ulinzi wa amani inahitajika katika kuwakabili wavurugaji wa amani katika eneo hilo.
 

Balozi  Manongi amesisitiza kuwa ili amani ya kudumu iwepo nchini DRC, na hususani eneo hilo la Mashariki, panahitajika pia uwepo wa vikosi vya ulinzi wa amani vitakavyokuwa na uwezo wa kuchukua maamuzi ya haraka na wakati mwingine katika mazingira magumu kama sehemu muhimu ya kuchagiza ufanisi na mafanikio.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top