MIILI 25 imepatikana Ziwa Albert baada ya boti iliyokuwa imebeba wakimbizi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuzama.

Wakimbizi hao walikuwa wakitoroka kutoka kambi ya wakimbizi ya Kyangwali wilayani Hoima magharibi mwa Uganda, wakirejea kwao.

Kwa sasa Jeshi la polisi linaendelea na jitihada za kutafuta miili zaidi. Kamanda wa polisi wa eneo hilo John Ojukuna amesema watu 43 wameokolewa. Boti iliyozama inadhaniwa kuwa ilikuwa imebeba zaidi ya wakimbizi 100.

Wengi wa wakimbizi hao ni wale waliokimbia mapigano mashariki mwa Kongo mwaka jana.

Mwendeshaji wa boti hiyo amekamatwa na jeshi la polisi na inadaiwa kuwa alikuwa amelewa. Wakimbizi waliookolewa wamewaambia polisi kuwa alikuwa mlevi na alikuwa akiendesha boti hiyo kwa kasi.

Hii siyo mara ya kwanza ajali ya boti kuua watu katika Ziwa Albert kutokana na kujaza abiria na mizigo kupita kiasi. Miaka minne iliyopia boti nyingine ilizama na kusababisha vifo vya watu 70.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top