Chama cha Walimu Tanzania (CWT), kimetangaza mgogoro na Serikali
kwa kile walichodai kutofanyiwa kazi madai yao mbalimbali yakiwamo
malimbikizo ya mishahara na likizo ya walimu zaidi ya Sh61 bilioni.
Madai mengine ni Serikali kutofanya maandalizi mazuri ya mfumo wa kutathmini utendaji kwa kuwapandisha walimu madaraja.
Rais wa Chama cha Walimu Tanzania Gratian Mukoba
alisema jana kuwa, katika madai hayo matatu, hakuna lililofanyiwa kazi
hivyo wamechoka kupewa ahadi hewa na Serikali ndiyo maana wamefikia
hatua hiyo.
Mukoba aliiambia Mwananchi kwa simu jana kuwa
Baraza la Taifa la CWT lililokaa kuanzia Januari 27 hadi 29, mwaka huu
liliazimia kwamba kero za walimu ziwe zimepatiwa ufumbuzi hadi mwishoni
wa Februari vinginevyo chama kitangaze mgogoro na Serikari.
“Kwa kuwa hakuna dai hata moja lililofanyiwa kazi
na Serikali, hivyo kutokana na kero za walimu kutopatiwa ufumbuzi
kuanzia sasa, CWT kimetengaza mgogoro na Serikali,” alisema Mukoba.
Alisema Serikali iliiahidi CWT kuwa Februari mwaka
huu ingewalipa madai ya walimu yanayohusiana na malimbikizo ya mshahara
matokeo yake imebadili ahadi hiyo na italipa taratibu kwa sababu
yanahitaji kutumia mfumo mpya wa kielektroniki wa kuingiza madeni ili
yalipwe.
Alisema vikao mbalimbali vya majadiliano ya
mishahara ambavyo vimeshafanyika kutokana na maagizo ya Mahakama Kuu ya
Division ya Kazi ya mwaka 2012, hakuna chochote ambacho kimeshapatikana.
Mukoba alisema madai mengine kuwa Serikali
haikufanya maandalizi mazuri ya mfumo wa kutathmini utendaji kazi, kwani
iligawa fomu Septemba mwaka 2013 na imejikuta kazi ya kupandisha walimu
madaraja imefanywa kwa mikoa 12 na siyo kwa wilaya zote.
“Serikali imejikuta ikishindwa kupandisha walimu
madaraja kwa asilimia 100, na kwa bahati mbaya sana hadi kikao cha
Februari 4 mwaka huu, ni mikoa 12 tu ambayo nayo siyo wilaya zote ndiyo
walimu wamepandishwa madaraja na mikoa 13 iliyobaki tumeelezwa kuwa
zoezi la kuwapandisha madaraja linaendelea,” alisema Mukoba.
“Tungependa kuona mambo haya pia yanatekelezwa na Serikali kama ilivyoahidi kwa walimu,” alisema.
Mwananchi
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment