IMANI za kishirikina zimegubika kijiji cha Iyela, Kata ya Mkwamba, wilayani Nkasi, Rukwa, na kusababisha walimu sita kati ya 10 wa Shule ya Msingi Mkwamba kukimbia shule hiyo na kuomba wapangiwe shule nyingine, ili kuokoa maisha yao.

Wakizumgumza na Tanzania Daima kwa niaba ya walimu wenzao katika shule hiyo, Josephat Kapandila na Jelazi Kakusa, walisema walimu hao wakiwamo wa kike wamekimbia baada ya kudai kuingiliwa kimwili na wanaume kwa imani za kishirikina Walisema sakata hilo limedumu kwa muda mrefu sasa na wametoa taarifa ofisi ya kijiji, ili kupata msaada lakini wamekosa ushirikiano.

Kutokana na hali hiyo, waliiomba Ofisi ya Elimu Wilaya kuwasaidia na ndipo walimu wawili kati ya wahanga wa tukio hilo walipopewa uhamisho.

Walisema kuwa walifikiri baada ya walimu hao wa kike kuondoka shule ingerudi katika utulivu, lakini vitendo hivyo vimeendelea na walimu wengine kulazimika kuondoka.

Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Michael Kapela, alisema licha ya shule hiyo kukumbwa na matatizo hayo ameshangazwa na ofisi ya elimu wilaya kukubali kuwahamisha walimu bila yeye kujua.

Alisema kwa kawaida kama mwalimu anaomba uhamisho ni lazima maombi yaanzie kwake, mratibu kata na kisha ngazi ya wilaya, lakini ofisi ya wilaya imekuwa ikitoa barua za uhamisho bila wao kushirikishwa na kutaka kujua tatizo hasa ni nini katika shule hiyo kwa lengo la kulitafutia ufumbuzi.

Afisa mtendaji wa kata hiyo Ghambi Idon alikiri kuwapo kwa tatizo kati ya wananchi na walimu wa shule hiyo wakituhumiana walimu wa kike kuingiliwa kimwili kiushirikina.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top