Majeneza yaliyowekwa miili ya marehemu waliokufa katika shambulio la
bomu Jumapili iliyopita kwenye misa ya uzinduzi wa Kanisa Katoliki la
Mtakatifu Joseph Mfanyakazi la Parokia ya Olasiti, Jimbo Kuu la Arusha,
majeneza hayo yalikuwa ndani ya Kanisa hilo wakati wa misa ya kuwaombea
kabla ya kuzikwa.
Watu watatu, waliofariki katika shambulio la bomu katika Kanisa
Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, mkoani
Arusha wamezikwa jana na mamia ya watu, huku ulinzi ukiwa umeimarishwa
kuliko kawaida na viongozi wa dini na Serikali kutoa kauli nzito.
Marehemu hao, ni Regina Loning’o Laizer (45),
James Gabriel(16) na Patricia Joachim Assey(9) walizikwa katika eneo la
kanisa hilo Katoliki, mazishi yaliyohudhuriwa na maaskofu wanane wa
majimbo tofauti ya Kanisa Katoliki, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la
Kilutheri Tanzania(KKKT), Askofu Alex Malasusa, Waziri Mkuu Mizengo
Pinda na viongozi mbalimbali wa dini, Serikali na kisiasa.
Kauli za viongozi
Katika ibada hiyo ya viongozi mbalimbali wa
kidini, walitoa salamu zao akiwamo Rais wa Baraza la Maaskofu wa Kanisa
Katoliki Tanzania (TEC), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa aliyeitaka
Serikali kutumia msamiati wa mwenye macho haambiwi tazama na kukomesha
mpasuko wa kidini aliosema unalitafuna taifa.
Askofu huyo alisema kuwa miongo mitatu sasa,
Serikali imekaa kimya, ikishuhudia mafundisho na mihadhara ya kidini
inayochochea na kuhamasisha uhasama kati ya Ukristo na Uislamu, bila
kuchukua hatua kukomesha hali hiyo.
“Matukio mbalimbali yanayoashiria uhasama wa
kidini yanatokea nchini. Kuna mihadhara, CD, DVD, machapisho na
mafundisho yanayotishia maisha na usalama wa viongozi wa kanisa na
waumini wao, ambayo yamefuatiwa na uchomaji wa makanisa,” alisema
Askofu Ngalalekumtwa.
Alitaja mfano wa kongamano la Januari 15, mwaka
juzi iliyofanyika Ukumbi wa Diamond Jubillee jijini Dar es Salaam kuwa
moja ya mikutano iliyojaribu kuchochea chuki ya kidini kati ya Waislamu
na Wakristo kwa kudai kuwa Serikali ya Tanzania inaongozwa kwa mfumo wa
Kikristo ulioasisiwa na Hayati Mwalimu Julius Nyerere.
Askofu huyo alisema kwamba katika kongamano hilo,
washiriki waliaminishwa kuwa Serikali inatoa fedha za ruzuku kujenga
shule na taasisi za kanisa kutokana na kuwapo mkataba maalumu kati ya
kanisa na Serikali, jambo ambalo siyo kweli.
“Kinachosikitisha zaidi ni kwamba Serikali
haikukanusha madai na uchochezi huo, licha ya mambo hayo kufanyika na
kusemwa hadharani kwa wahusika kuzunguka nchi nzima kueneza chuki na
uchochezi huo,” alisema Askofu Ngalalekumtwa.
Mkuu wa Kanisa la KKKT, Askofu Dk Alex Malasusa
alisema kuwa tukio la Arusha ni la kikatili na aibu kwa taifa akiwataka
wenye dhamana ya ulinzi na usalama kuchukua hatua kudhibiti hali hiyo
akionya kuwa wasipofanya hivyo watahukumiwa kwa kosa la kukaa kimya
mambo yakiharibika mikononi mwao.
“Wote wenye jukumu la kulinda na kuitunza amani
waifanye kazi hiyo bila uoga. Wasipofanya hivyo iko siku watahukumiwa,”
alisema Dk Malasusa.
Mwakilishi wa Muungano wa Madhehebu ya Kikristo
mkoani Arusha, Askofu Stanley Hotay aliwataka viongozi wa kisiasa
kuepuka kutumia jukwaa la dini kutimiza malengo ya kisiasa, akionya kuwa
makanisa hayana itikadi, bali waumini ndiyo wenye itikadi mbalimbali.
Mwananchi
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment