Sir Alex Ferguson 
Uongozi wa Old Trafford umetangaza rasmi na kuthibitisha kuwa David Moyes atakuwa meneja mpya wa timu hiyo kuchukua nafasi ya Sir Alex Ferguson atakayestaafu mwishoni mwa msimu huu.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Old Trafford mchana wa leo, David Moyes amepewa mkataba wa miaka sita wa kuifundisha Manchester United kuanzia msimu ujao.

David Moyes mwenye umri wa miaka 50,ametangazwa kuwa mrithi wa Ferguson ambaye alitangaza kustaafu kuifundisha Manchester United mwishoni mwa msimu huu baada ya kuifundisha United kwa karibu miaka 27.

"Tumekubaliana kwa pamoja bila kipingamizi kupitisha jina la David Moyes" alisema Ferguson.

"David ni mtu ambaye ana uadilifu wa hali ya juu na mwenye maadili makubwa ya kazi. Nimeipenda kazi yake kwa muda mrefu tangu mwaka 1998 wakati tulipomjadili kama kocha msaidizi.
"Hakuna maswali juu yake na ana viwango ambavyo tulikuwa tunavihitaji kwa meneja wa klabu hii." aliongeza Ferguson.

Naye David Moyes amesema " Najua ni vigumu kurithi na kufikia mafanikio kama ya kocha bora zaidi duniani, lakini nafasi ya kuifundisha Manchester United sio jambo ambalo linakuja mara mbili hivyo nina matumani mazuri nikiwa kocha wa klabu hii msimu ujao."

David Moyes amekaa Goodison Park kwa miaka 11 na hajawahi kushinda taji la ligi kuu lakini ameweza kuifanya Everton kuwa miongoni mwa klabu zenye mafanikio ya wastani kwenye ligi kuu soka nchini England.

Akiwa na Everton, Moyes ameifikisha fainali ya kombe la FA mwaka 2009 katika mechi waliyofungwa na Chelsea 2-1, na pia mwaka 2005 aliweza kumaliza nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi kuu ya England lakini waliondolewa kwenye hatua za mwanzo za kusaka nafasi ya kushiriki michuano ya klabu bingwa barani Ulaya.

Licha ya kuwa na bajeti ndogo ya usajili, Moyes aliiwezesha Everton kuonekana miongoni mwa timu zenye kiwango bora cha soka ambapo mara kadhaa amekuwa akitoa upinzani mkubwa kwa Manchester United ambapo katika mechi ya kwanza ya ligi kuu msimu huu, Everton waliifunga United kwa bao moja kwa bila.

Kibarua kikubwa ambacho anatarajia kukikabili kama meneja mpya wa United msimu ujao itakuwa ni kuhakikisha mchezaji wake wa zamani aliyemuibua Wayne Rooney anasalia kwenye klabu hiyo baada ya kutangaza kuwa anataka kuondoka.

Meneja wa Wigan, Roberto Martinez na bosi wa Swansea, Michael Laudrup wanatajwa kama warithi wa Moyes kwenye klabu ya Everton.

Mechi ya kwanza ya David Moyes kama kocha mpya wa Manchester United inatarajia kuwa ya ngao ya jamii watakapo pambana na watani zao Manchester City ama Wigan hapo tarehe 11 mwezi wa nane kwenye uwanja wa Wembley.

MAN.UNITED YASEMA  ROONEY HAUZWI
Rooney akiwa na Kocha David Moyes aliyemtoa kisoka.

Klabu ya Manchester United imepuuzilia mbali uvumi uliozagaa ya kwamba Mshambuliaji wa Kimataifa wa Uingereza anayekipiga katika timu hiyo Wayne Rooney atauzwa mwishoni mwa msimu huu.

Manchester United imekanusha uvumi huo kupitia Msemaji wa Klabu hiyo umesema hakuna mpango wowote wa kuuzwa kwa Mshambuliaji huyo aliyetumikia timu hiyo kwa miaka tisa sasa.

Msemaji wa Manchester United amesisitiza Rooney mwenye umri wa miaka 27 ataendelea kuwepo katika klabu hiyo na hawezi kuondoka eti kwa kuwa Kocha Mkuu Sir Alex Ferguson ametangaza kustaafu mwishoni mwa msimu huu.

Tamko la Manchester United limekujwa baada ya kuwepo taarifa Rooney ameomba kuondoka kwa mara ya pili katika kipindi cha miaka mitatu sasa taarifa ambazo zimetajwa kuwa ni uzushi mtupu.

Taarifa hizi zinakuja na kuongezewa nguvu ya kwamba Rooney alishamuomba Sir Ferguson kuondoka Manchester United kipindi cha majuma mawili yaliyopita lakini ombi lililokataliwa na Kocha huyo.
Rooney anatajwa kuwa aliomba kuondoka Manchester United na kumueleza Sir Ferguson ya kwamba huu ni wakati wake muafaka kuondoka baada ya kuitumikia Klabu hiyo kwa kipindi cha miaka tisa akitokea Everton.

Uvumi wa kuondoka kwa Rooney unakuja ikiwa ni siku moja baada ya Sir Ferguson kutangaza kustaafu wadhifa wake na wengi walianza kutoa taarifa hizo punde tu baada ya mchezaji huyo kuonekana akikosa namba ya kudumu kwenye kikosi cha kwanza.

Mshambuliaji huyo anaelezwa alikuwa na hasira baada ya kuwekwa benchi katika mchezo dhidi ya Real Madrid ambapo Danny Welbeck alianza kwenye mchezo huo ambao Manchester United haikufanya vizuri.

Rooney msimu huu amekuwa akibadilishwa mara kadhaa tangu Manchester United imsajili Robin Van Persie ambaye alipewa jukumu la kuwa mshambuliaji kinara na kuweza kuisaidia kutwaa taji la 20.

Tangu Rooney ajiunge na Manchester United mwezi Agosti mwaka 2004 amecheza michezo 402 na kufunga magoli 197 huku msimu huu akifunga magoli 16 katika michezo 37 aliyoshuka dimbani.

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

1 comments:

Aizea said... May 11, 2013 at 12:06 PM

Moyes nadhani ana changamoto kubwa. Hii itamuwezesha kukua na hata kuwa moja ya makocha bora duniani.

 
Top