Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimeibana serikali kikitaka  viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) walionaswa wakifanya mawasiliano na watuhumiwa wa ugaidi wa kubambikizwa waunganishwe kwenye kesi hiyo.

Kauli hiyo ilitolewa jana bungeni na Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe, wakati akiwasilisha hotuba mbadala ya makadirio ya   mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2013/2014 katika Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa CHADEMA taifa na Mbunge wa Hai, alisema vitendo vya viongozi wa dini kujeruhiwa na kuuawa kwa kupigwa risasi, kuchoma moto nyumba za ibada huko Zanzibar na Dar es Salaam ni ugaidi kwa mujibu wa tafsiri ya Sheria ya Ugaidi ya Tanzania.

“Kambi Rasmi ya Upinzani inashangazwa sana kuona kwamba serikali haikuyachukulia matukio haya ya wazi ya kigaidi kama ni ugaidi ila imekuwa hodari sana kuchukua suala la mtu aliyebambikiwa kesi ya ugaidi kwa ushahidi wa kughushi kuwa yeye ndiye gaidi.

“Pili, kwa mujibu wa Sheria ya Ugaidi, mtu yeyote anayefanya mawasiliano na gaidi au magaidi, yeye pia anahamasisha ugaidi, hivyo naye anastahili kuunganishwa katika tuhuma hizo za mashtaka ya ugaidi,” alisema Mbowe.

Ingawa Mbowe hakutaja jina la mtu, lakini ni dhahiri alikuwa akimzungumzia Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA, Willfred Lwakatare na kijana Ludovick Joseph, ambao wamefunguliwa mashtaka ya ugaidi kwa madai ya kupanga njama za kutaka kumdhuru Mhariri wa gazeti la Mwananchi, Dennis Msacky.

Kufunguliwa kwa kesi hiyo kumeibua mjadala mkali miongoni mwa wananchi wakihoji ni kwanini Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Mwigulu Nchemba, ambaye amekiri kuwa na video hiyo inayoonesha mipango ya kigaidi hakushtakiwa.

Mwigulu pia amedaiwa kuwa na mawasiliano ya karibu na Ludovick kabla na baada ya video hiyo kurekodiwa ikiwa ni pamoja na kumtumia fedha kwa njia ya M-pesa kupitia namba yake ya simu.
Hivyo kauli ya Mbowe ni kama alimlenga Nchemba ambaye anadaiwa kufanya mawasiliano na watuhumiwa hao wa ugaidi na bado yupo nje wala hajahojiwa na polisi.

Alisema kuwa  hivi sasa taifa linashuhudia kuibuka kwa uchochezi mpya wa kisiasa tena wenye ubia kati ya CCM na vyombo vya dola na kinachoitwa ‘ugaidi’.

“Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inasikitika sana kuona wale wote waliokuwa wakiwasiliana na hao wanaoitwa magaidi, ambao pia ni viongozi wa CCM na washirika wao hawajachukuliwa hatua yoyote,” alisema.

Aliongeza kuwa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaulaani mkakati huu wenye nia ovu ya kufifisha demokrasia hapa nchini.

Mbowe alifafanua kuwa Kambi Rasmi ya Upinzani inaamini kwamba,  kamwe mpango huu haramu hautafanikiwa na alitumia nafasi hiyo kuonya kuwa vyama vya siasa vifanye siasa zake kwa ushindani wa sera na isiwe kwa mikakati ya kiharamia ya kudhuru, kubambikiza na kisha kutengeneza ushahidi kwa kutumia vyombo vya ulinzi na usalama.

“Hili nalo likiachiwa likakomaa litaliingiza taifa letu katika hatari nyingine ya machafuko,” alisisitiza.

Akieleza chanzo cha chuki hiyo, Mbowe alisema  ilipaliliwa kisiasa na sasa ndiyo inayoitesa nchi na kwamba  linastahili kuwa somo kwa wanasiasa wote walioasisi uhalifu huu dhidi ya mustakabali mwema wa taifa.

“Mheshimiwa Spika, uchochezi na propaganda za kidini na kikabila vilichagizwa kasi na CCM mara baada ya kuanza mfumo wa vyama vingi vya siasa kama mojawapo ya turufu yake ya kukabiliana na vyama vya upinzani.

“Uchochezi huu ulishika kasi katika uchaguzi wa mwaka 2005 na mwaka 2010. Vikundi kadhaa vya kidini vilifadhiliwa kuhubiri chuki dhidi ya dini nyingine waziwazi na kwa muda mrefu katika maeneo kadhaa ya nchi,” alisema.

Mbowe alifafanua kuwa mihadhara, mahubiri na hata matamko ya hatari na uchochezi yalitolewa waziwazi hata kupitia vyombo kadhaa vya habari vya kidini na mitandao ya kijamii.

“Malalamiko mengi yalitolewa lakini serikali ilifumbia macho tatizo hili, kwani ilionekana kuwa mpasuko na hofu iliyo matokeo ya propaganda hizo ulikinufaisha zaidi chama tawala na baadhi ya viongozi wake,” alisema.

Mabadiliko ya Katiba
Kuhusu mabadiliko ya Katiba, Mbowe aliweka msimamo wa chama chake kuwa   kitajitoa kushiriki katika mchakato wa Katiba Mpya endapo mambo yafuatayo hayatapatiwa ufumbuzi hadi kufikia mwisho wa mwezi huu.

Aliyataja mambo hayo kuwa ni pamoja na kufutwa kwa uteuzi/ uchaguzi wa wajumbe wa mabaraza ya wilaya ya Katiba uliofanywa na Kamati za Maendeleo za Kata, na badala yake wajumbe wa mabaraza ya katiba ya wilaya wachaguliwe moja kwa moja na wananchi wa kata husika bila kuchujwa na WDC.

Kwa mujibu wa Mbowe, aliitaka serikali ilete mbele ya Bunge Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba yatakayofanyika maeneo yafuatayo.

Moja, ni vifungu vyote vinavyohusu uwakilishi katika Bunge Maalumu la Katiba na taasisi zilizoainishwa katika Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.

Pili, alisema ni vifungu vyote vinavyohusu ushirikishi wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutoka Zanzibar katika mijadala inayohusu mambo yasiyokuwa ya muungano ya Tanzania Bara.

Tatu, pia alitaja vifungu vyote vinavyohusu mamlaka ya rais kuitisha tena Bunge Maalumu la Katiba baada ya Bunge hilo kuwa limeshapitisha Rasimu ya Katiba Mpya kwa lengo la kufanya marekebisho katika rasimu kabla haijapelekwa kwenye kura ya maoni.

Nnne, ni vifungu vyote vinavyohusu mamlaka ya kikatiba na ya kisheria yatakayoiwezesha Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuendesha na kusimamia kura ya maoni.

Mbowe alisema kuwa kwa mujibu wa Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji Joseph  Warioba, hadi awamu nne za kukusanya maoni ya wananchi zinakamilika Desemba 19 mwaka jana, tume ilikwisha kufanya mikutano 1,776 nchi nzima.

Kwamba kufikia kipindi hicho wananchi wapatao 64,737 walikwishatoa maoni yao kwa kuzungumza wakati 253,486 walitoa maoni kwa njia ya maandishi, na wengine 16,261 walitumia njia ya posta, tovuti ya tume, mitandao ya kijamii na ujumbe mfupi wa simu za mkononi.

“Kwa hiyo, kwa mujibu wa taarifa hizi za tume, kati ya Watanzania takriban milioni 45, ni Watanzania 334,484 ndio waliotoa maoni juu ya Katiba Mpya hadi kufikia Januari 4, mwaka huu. Idadi hii ni sawa na asilimia 0.7 ya Watanzania wote.

“Na hao ndio waliotoa maoni yao kwa muda wa dakika tano kila mmoja, wakiwamo waheshimiwa wabunge wa Bunge hili tukufu. Mheshimiwa Spika, ni wazi kwa takwimu hizi za Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kwa vyovyote vile, Katiba Mpya itakayotokana na maoni haya haiwezi kuwa Katiba Mpya ya Watanzania wote,” alisema.

Mbowe alisema kuwa utaratibu wa hovyo namna hiyo utazaa Katiba Mpya ya hovyo, kwamba Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini utaratibu huu wa hovyo hauwezi kutupatia Katiba Mpya yenye maridhiano ya kitaifa kwa ajili ya kutatua migogoro mingi ya kisiasa, kijamii na kidini ambayo inaikabili nchi yetu kwa sasa.

Alisema CHADEMA haiwezi kuendelea kushiriki na kubariki mchakato huu kama ulivyo sasa kwani ishara zote ziko wazi kuwa Katiba inayokusudiwa ni ile tu itakayokidhi matakwa ya Wana CCM na washirika wake, hivyo kutokutimiza azima ya kuwa na Katiba itakayoponya majeraha mbalimbali na kurejesha uzalendo, mshikamano na upendo wa dhati miongoni mwa Watanzania. 

Hatima ya waliofeli
Kuhusu waliofeli elimu ya msingi na sekondari, Mbowe alisema vijana hao kwa sasa ni wastani wa watoto 800,000.

Alisema wengi wao wanatoka familia maskini, hawana uwezo wa kujiendeleza na hawana sifa za kuajiriwa ikiwa ni pamoja na umri mdogo.

Mbowe aliongeza kuwa kwa kipindi cha miaka 51 ya Uhuru, serikali haijatengeneza sera yoyote au sheria ya kusaidia kundi hili kubwa ili liweze kushiriki  katika shughuli za kiuchumi ili liweze kujikimu na kuchangia katika pato la taifa.

“Mheshimiwa Spika, Kambi Rasmi ya Upinzani inaitaka serikali kueleza mbele ya Bunge hili kwamba ina mpango gani wa kupunguza idadi hii ya watoto wanaobaki mitaani bila shughuli rasmi ya kufanya,” alisema.
Chanzo:  Tanzania Daima
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top