TANZANIA VETERANS WAZIDI KUIKOMALIA TFF KUHUSU KUENGULIWA KWA JAMAL MALINZI
Mchezaji wa zamani wa Yanga na Taifa Stars Bakari Malima Jembe Ulaya na Madaraka Suleimani mzee wa kiminyio wakiongea na waandishi wa habari kuhusiana na hali ya sekeseke la uchaguzi linalozidi kufukuta na kutishia soka la Tanzania kwenda halijojo.

Baadhi ya wadau wa michezo wamesema kitendo kumuengua JAMAL MALINZI aliyekuwa mgombea URAIS wa TFF kilichofanywa na kamati ya Rufaa ya shirikisho la kandanda Tanzania TFF ni kukandamiza na kurudisha nyuma maendeleo ya mchezo wa soka hapa nchini.

Wadau hao kwa kauli moja wamesema wako tayari kulipeleka suala hilo kwa mahakamani  ili kuhakikisha haki inatendeka.

Beki mahiri wa klabu ya Yanga na timu ya Taifa Stars Bakari Malima ni miongoni mwa wadau waliopendekeza kuwa jina la Jamal Malinzi linarejeshwa katika orodha ya wagombea ili kupambana na Athumani Nyamlani ambaye amebaki kama mgombea pekee.

Wadau wengine walioongea na vyombo vya habari walikuwa Mchezaji wa Zamani  Simba na Taifa Stars Madaraka Suleimani maarufu Mzee wa Kiminyio  wamedai maendeleo ya soka hayawezi kufikiwa kama mizengwe itaendelea katika mchezo huo.

Hassan Mbashiri ambaye ni miongoni wajumbe wa wanakamati wa kuhakikisha uchaguzi wa TFF unafanyika kwa mujibu wa sheria na si kuona mpira unaburuzwa huku wadau wakibaki watazamaji tuu.

Hata hivyo katibu mkuu wa Shirikisho Angetile Osiah amesema hawezi kuyatolea ufafanuzi malalamiko ya wadau kuwa baadhi ya majina yameondolewa kimizengwe wakati kuna sheria,kanuni na taratibu zilizotumika kuwaengua wagombea husika.

Baadhi ya wagombea ambao rufaa zao zimedunda ni Michael Richard Wambura aliyekuwa anawania nafasi ya makamu rais wa TFF Omari Nkurulo aliyekuwa akigombea nafasi ya Urais TFF.

AZAM  TAYARI KUKIPIGA NA AL NASRI JUBA
 Kikosi cha Timu ya Azam
Uongozi wa klabu ya Azam umesema umejipanga kuhakikksha inaibuka na ushindi katika mechi ya kombe la Shirikisho la kandanda barani Afrika dhidi ya Al Nasri Juba ya Sudan Kusini ikiwa ni mara ya kwanza kushiriki katika michuano hiyo mikubwa.

Afisa habari wa klabu ya Azam Jaffar Idd amesema licha ya kwamba wapinzani wao hawakutoa taarifa mapema ya Ujio wao lakini wanaisubiri kwa hamu,hapo Jumamosi Februari 16 katika uwanja wa Taifa.

SIMBA KUIVAA RECREATIVO LIBOLO JUMAPILI
Mabingwa wa ligi kuu ya kandanda Tanzania, Simba ya Dar es Salaam wanataraji kushuka dimbani Jumapili wiki hii dhidi ya Recreative de Libolo ya Angola katika ligi ya mabingwa barani Afrika.

Mechi hiyo itapigwa katika dimba la Taifa inataraji kuwa vuta nikuvute kutokana na uimara wa timu zote mbili.

Mwenyekiti wa klabu ya Simba Ismail Aden Rage amesema wamefanya maandalizi ya kutosha kutoka kwa kocha Patrick Liewig ambaye anaongoza jopo la ufundi la Wekundu wa Msimbazi.

Klabu ya Simba ilifanya vizuri kwa mara ya mwisho mwaka 2003 ambapo ilitinga hatua robo fainali.

Simba imewahi kutinga hatua nusu fainali ya michuano hiyo mwaka 1974 na kutolewa na Mehalla el Kubra  ya Misri hata hivyo mwaka 1993 imewahi kutinga hatua ya fainali ya michuano ya kombe la shirikisho maarufu kama michuano ya CAF dhidi ya Stella Abidjan ya Ivory Coast.


wakati huo huo Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linazitakia kila la kheri timu za Azam, Jamhuri na Simba ambazo zinaiwakilisha Tanzania katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho.

Azam inacheza na Al Nasir Juba ya Sudan Kusini katika mchezo wa Kombe la Shirikisho utakaofanyika Jumamosi (Februari 16 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Nayo Jamhuri ya Zanzibar kesho itacheza na St. Georges ya Ethiopia katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika utakaofanyika Uwanja wa Gombani kisiwani Pemba. Simba itacheza na Recreativo do Libolo ya Angola keshokutwa (Februari 17 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

 CAF YASITISHA UKAMISHNA WA HAFIDH ALI
 Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limesitisha ukamishna wa Hafidh Ali. Uamuzi huo umefanywa na Kamati ya Mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika iliyokutana Januari 17 mwaka huu jijini Johannesburg, Afrika Kusini.

Kwa mujibu wa barua ya Katibu Mkuu wa CAF, Hicham El Amrani kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), ukamishna huo umesitishwa kwa vile hadi sasa Shirikisho hilo halijapata ripoti ya mechi namba 78 kati ya Comoro na Libya ambayo Ali aliteuliwa kuisimamia.

YANGA, AFRICAN LYON ZAINGIZA MIL 68/-
Mechi namba 119 ya Ligi Kuu ya Vodacom iliyochezwa juzi (Februari 13 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa Yanga kuibuka ushindi wa mabao 4-0 imeingiza sh. 68,438,000.

Watazamaji 12,147 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo iliyochezwa kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 16,170,252.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 10,439,694.92.

Kiingilio cha sh. 5,000 ndicho kilichovutia watazamaji wengi ambapo 10,982 walikata tiketi hizo na kuingiza sh. 54,910,000.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 8,222,162.26, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 4,933,297.36, Kamati ya Ligi sh. 4,933,297.36, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 2,466,648.68 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,918,504.53.

PONGEZI KWA UONGOZI MPYA TASMA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa pongezi kwa uongozi mpya wa Chama cha Wataalamu wa Tiba ya Michezo Tanzania (TASMA) uliochaguliwa katika uchaguzi uliofanyika Februari 10 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Ushindi waliopata viongozi waliochaguliwa kuongoza chama hicho unaonesha jinsi wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TASMA walivyo na imani kubwa kwao katika kusimamia tiba ya wanasoka nchini.

TFF inaahidi kuendeleza ushirikiano wake kwa Kamati ya Utendaji ya TASMA chini ya uenyekiti wa Dk. Mwanandi Mwankemwa aliyeibuka mshindi katika uchaguzi huo kwa kura 18 dhidi ya 7 za aliyekuwa Mwenyekiti Biyondho Ngome

Uongozi huo mpya una changamoto nyingi, kubwa ikiwa ni kuhakikisha unaendesha shughuli za mpira wa miguu kwa kuzingatia katiba ya TASMA pamoja na vyombo vya mpira wa miguu vilivyo juu yake.

Pia tunatoa pongezi kwa Kamati ya Uchaguzi ya TASMA chini ya Dk. Paul Marealle na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kuhakikisha uchaguzi huo unaendeshwa kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi za Wanachama wa TFF.

Safu nzima ya uongozi wa TASMA iliyochaguliwa inaundwa na Dk. Mwanandi Mwankemwa (Mwenyekiti), Dk. Nassoro Matuzya (Katibu Mkuu), Sheky Mngazija (Katibu Msaidizi), Dk. Juma Mzimbiri (Mhazini), Joakim Mshanga (mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF) na Dk. Hemed Mziray (mjumbe wa Kamati ya Utendaji).

Ukiondoa nafasi ya Mwenyekiti, wagombea wengine wote hawakuwa na wapinzani. Nafasi ya Makamu Mwenyekiti haikupata mgombea, hivyo itajazwa katika uchaguzi mdogo utakaofanyika baadaye mwaka huu. TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top