Mwanablog amefika msibani kwa ajili ya kushiriki mazishi ya ndugu yake (Mbwiga Yabhamba) kijijini Jojo kata ya Santilya Mbeya Vijijini. Hata hivyo, kuna jambo linamvutia kiasi cha kumfanya aanze kuliangalia kwa jicho la pekee. Si jingine zaidi ya utekelezaji wa wosia ulioachwa na marehemu kwa watoto wake. Alisema mambo mawili: kwanza, nataka mnizike jirani na nyumba yangu na mwanandani (ngwenya) uwe katika nyumba yangu. Pili, msinizike katikati kama mnavyozika siku hizi badala yake mnizike kama zamani; mtanichimbia mwanandani na huko kunikalisha katika kiti changu. Hivyo, Kabla ya kufariki, marehemu alinunuliwa kiti chake na kukikagua.

 Zifuatazo ni picha na maelezo ya maziko ya marehemu yaliyofanyika siku ya Jumatatu ya tarehe 10.12.2012 na kushuhudiwa na mwanablog. Nakusihi ufuatilie kisha uone falsafa iliyokuwa katika mazishi ya kabila hili na hata Waafrika kwa ujumla hasa kabla ya ujio wa wageni. Kumbuka kuwa mazishi ya aina hii hupatikana mara chache siku hizi katika kabila hili.
Enzi za uhai wake marehemu aliagiza kuwa kaburi lake lichimbwe pembezoni mwa nyumba yake. Zoezi la kuchimba linaendelea pembezoni mwa nyumba ya marehemu. Kwa kawaida shimo huwa na urefu wa futi zaidi ya saba. Uchunguzi unaonesha kuwa urefu wa shimo waweza kwenda mbali zaidi kama marehemu alikuwa anapendwa sana na jamii au kama jamii ilikuwa na mtazamo hasi dhidi ya marehemu. Kwa wanaompenda hufanya hivyo kuchelewesha mazishi yake kwa imani kuwa wanendelea kuongea naye. kama wana mtazamo hasi na marehemu huamini kuwa wakichimba shimo fupi atafufuka, kufukua udongo kiurahisi na kisha kutoka.

Marehemu enzi za uhai wake aliagiza pia kuwa awekewe mwanandani na mwili wake kuwekwa huko. Vijana wanachimba mwanandani kama walivyoelekezwa.
Wachimbaji wa kaburi wakiwa eneo la mwanandani. Kwa kawaida eneo la mwanandani lilikuwa na uwezo wa kuchukua wachimbaji zaidi ya sita. Huko, walitengeneza kutegemeana na masharti  ya mila na desturi za ukoo wa marehemu, mapenzi ya wachimbaji kwa marehemu na marehemu alikuwa anapenda nini (mfano; uwindaji, pombe, nk). Hivi viliathiri ukubwa na upambaji wa mwanandani. Walipoulizwa kuwa wanaepukaje kudondokewa na vifusi, walidai kuwa wakati wa kuchimba mwanandani kuna ishara zinazowasaidia kujua kuwa udongo unataka kudondoka. Mfano, mizizi kuanza kudondosha matone ya maji ni ishara kuwa watoke haraka shimoni.
Muombolezaji aliyevaa kofia amebeba baragumu. Hili hutumika kwa ajili ya kuujulisha umma wa watu kuwa kuna mtu amefariki. Hivyo, kila mtu lazima ajiridhishe juu ya wapi na ni nani amefariki. Kuna mlio maalumu unaoashiria kuwa kuna msiba kwa vile kuna milio mingine inayoashiria matukio mengine mfano ngoma. Baragumu la msiba hupigwa kwa watu wazima tu. Watoto wadogo hawapigiwi baragumu.
Mwili wa marehemu unashushwa kaburini tayari kwa mazishi. Wametanguliza miguu.
Ni mwiko katika kabila hili kumtaguliza miguu marehemu wakati wa kumwingiza eneo la mwanandani. Hivyo, wamelazimika kumgeuza ili atangulie kichwa kama inavyotakiwa, zoezi limefanikiwa, wanamwingiza.
Mwili wa marehemu umewekwa sehemu ya mwanandani kama yeye (marehemu) mwenyewe alivyoagiza. Vijana wanamuweka vizuri.
Zoezi la kuuweka vyema mwili wa marehemu ikiwa ni pamoja na kumkalisha kwenye kiti chake kama ilivyoagizwa na yeye mwenyewe (Marehemu)linaendelea.
Waombolezaji kwa majonzi makubwa wakifuatilia tukio la mazishi ya ndugu yao kwa vile hawatakuwa naye tena.
Ulitoka kwa udongo utarudi kwa udongo. Andiko linatimia. Vijana wanaanza kufukia. Mfukiaji wa kushoto kwako ana jembe kubwa lakini lenye mpini mfupi. Katika kabila hili huamini kuwa mtu mzima hana budi kuwa na jembe lake. Hili hukatwa mpini na ndilo linalotumika kuchimbia kaburi kwa mara ya kwanza kabisa (kukhomela) katika kaburi lake. Majembe mengine hufuata.
Ili kuhakikisha kuwa udongo hauingii eneo la mwanandani mkeka huwekwa kwa utaratibu maalumu ikiwa ni pamoja na kuweka miti kwanza kisha mkeka. Zoezi la kufukia hufanyika kwa uangalifu mkubwa na kwa  kupokezana jambo linalofanya tukio kuchukua muda mfupi zaidi.
Vijana wanaendelea na zoezi la kufukia ingawa baridi ni kali pia.
Kwa heri ya kuonana
Hii ni nyumba ya milele.
 Kushoto ni nyumba ya marehemu
 ambako kuna mwanandani.
Apumnzike kwa amani.



Mpaka hapo umeweza kupata kitu. 
Unaweza kuona kufanana au kutofanana kwa namna ya maziko ya kabila hili  na maziko asilia ya kabila lako. Kama hujui, mlizikaje, kaulize wazee wachache waliobaki kule mlikotoka. Unaweza kusema pia ni yapi mazuri, yanayofaa kuendelezwa, na yepi yamepitwa na wakati yanayopaswa kuachwa na utakuwa na sababu za uamuzi wako. Lengo la habari hii ni kutaka kukuonesha kuwa Waafrika na Uafrika wetu tumetoka wapi, tuko wapi na pengine tunakwenda wapi. 

Kuna mambo mengi yanayotuunganisha na kututambulisha kwa Uafrika wetu.Tatizo letu ni kuona kila kinachofanywa na Mwafrika kimepitwa na wakati hivyo ni kikwazo cha maendeleo ya sayansi na teknolojia hata kama ni mtaji mkubwa kwa maendeleo ya sayansi na teknolojia hiyo. Tunapenda vya Magharibi zaidi hata kama ni mwiba kuliko vya kwetu. Sasa vinakuja vya Mashariki, naongelea China kwa mfano. Tutavutwa kushoto kulia mpaka lini? 

 Ifike wakati, kwa dhati kabisa, tuwe jamii huru kifikra inayoweza kuamua na kuyasimamia maamuzi yake. Tusiwe sehemu ya kujaribia mawazo ya watu ambayo yamepitwa na wakati au hayawezi kuishi kwao. Vilevile tusiwe sehemu ya kutupia visivyohitajika kwao nasi kuona ni lulu wakati tukiwaachia vyetu wakijitwalia watakavyo. Wanachota utamaduni wetu wanatuuzia matokeo yake, nasi tunabaki kugombania vivuli vya utajiri wetu. Wao wanabaki kuwa matajiri sisi maskini na umaskini wetu katika nchi zinazonuka utajiri wa kila aina.  

Haya yote ni matokeo ya matatizo ya kifkra.  Wananchi tubadilike  viongozi wabadilike. Kila mtu abadilike. Kama upande mmoja utabadilika basi wananchi wawe wa kwanza. Maana kiongozi ni mwananchi hivyo ni lazima watabadilika. Wewe unasemaje?

Picha na Mwanablog TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top