NA RAMADHANI ALI/MAELEZO                     19/12/2012
 
Wizara ya Afya Zanzibar kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Chanjo GAVI, Shirika la kuhudumia watoto UNICEF  na WHO itaanzisha chanjo mbili mpya zinazokinga maradhi ya Kuharisha na Nyumonia kuanzia mwezi Februari mwakani
 
Akitoa taarifa ya kuanzishwa chanjo hizo kwenye Mkutano wa wadau katika Hoteli ya Bwawani, Naibu Waziri wa Afya Dk. Sira Ubwa Mwamboya amesema lengo  ni kupunguza idadi kubwa ya vifo vya watoto vinavyosababishwa na maradhi hayo.
 
Amesema watoto wenye umri wa miaka miwili wako katika hatari kubwa zaidi ya kupata maambukizi ya ugonjwa wa nyumonia na kuharisha na hatimae kufariki na ndio iliyopelekea  Mashirika ya Kimataifa kuanzisha chanjo hiyo ili kuwanusuru watoto na maradhi hayo.
 
Ameongeza kuwa lengo la Wizara ni kuwachanja watoto kufikia kiwango cha zaidi ya asilimia 95 katika kila Wilaya, hivyo amewataka wazazi na walezi pamoja na wananchi wote  kuchukua juhudi na kushiriki kikamilifu kuhakikisha watoto wote wanafikiwa na huduma za chanjo.
 
Dk Mwamboya amesema chanjo ni haki ya kila mtoto na kwa kutambua hilo mwaka 19981 Mradi wa chanjo Zanzibar ulianzishwa rasmi na chanjo dhidi ya Kifua kikuu, Kifaduro, Dondakoo. Polio na surua zilianza kutolewa.
 
“Chanjo nyengine  ya homa ya ini iliongezeka katika miaka 2002 na chango dhidi ya  ugonjwa wa homa ya uti wa mgongo na kichomi zilizinduliwa mwaka 2009”, aliongeza Dk. Mwamboya.
 
Naibu Waziri amesema huduma za chanjo zimechangia kwa kiasi kikubwa kufikia malengo ya Melenia katika kupunguza vifo na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo miongoni mwa watoto chini ya miaka mitano.
 
Amesema Wizara ya Afya inathamini juhudi zinazochukuliwa na wadau mbali mbali pamoja na viongozi katika  kuimarisha huduma za chanjo Zanzibar hata hivyo amesisitiza juhudi zaidi zinahitajika ili kuhakikisha watoto wote wanapatiwa huduma hiyo ambayo itatolewa bila malipo.
 
Amewahakikishia wananchi kuwa chanjo hizo ni salama na hazina madhara yoyote na baadhi ya nchi  duniani   zinaendelea kuzitumia na zimepata mafanikio makubwa ya kuwaepusha watoto na maradhi hayo.
 
Naibu Waziri amewakumbusha washiriki wa mkutano huo kwamba kiwango cha chango zilizopita kitaifa kimeonyesha kuongezeka lakini  zipo baadhi ya Wilaya kiwango chake cha uchanjaji kipo chini ya asilimia 80 .
 
Amezitaja Wilaya zilizofanya vibaya  kuwa ni Mkoani na Micheweni kwa miaka miwili mfululizo, Kaskazini A na Kaskazini B pamoja na Wilaya ya Chake Chake.
 
Mkuu wa Kitengo cha chango Katika Wizara ya Afya Dk Yussuf Makame amewaeleza washiriki wa Mkutano huo kwamba magonjwa ya nyumoni yanaathiri mapafu, uti wa mgongo na ubongo na husababishwa na bacteria aina ya Streptococcus.
 
“Magonjwa ya nyumonia huenezwa kwa njia ya hewa wakati mtu mwenye vimelea vya ugonjwa huo anapopiga chafya au kukohoa”, amesema Dk. Yussuf Makame.
 
Ameeleza chanjo hiyo itatolewa kwa watoto ambao hawajapatiwa chanjo ya aina yoyote na watoto wachanga watakaozaliwa .
 
Akizungumzia ugonjwa wa kuharisha , Msaidizi Mkuu wa Kitengo cha chanjo Dk. Abdulhamid Ameir Saleh amesema maradhi hayo yanasababishwa na virusi vya Rota na huenezwa kwa njia ya kula ama kunywa maji yaliyochafuliwa na kinyesi chenye virusi hivyo.
 
Katika michango yao washiriki wa mkutano huo wamesema takwimu zisizo sahihi zinazofuatwa na mafiasa wa Wizara  ya afya zimepelekea kuonekana baadhi ya Wilaya kutofikia viwango vya chanjo zilizowahi kutolewa miaka iliyopita.
 
Wameshauri kutumika takwimu walizonazo  masheha katika chanjo za nyumonia na kuharisha kwani ziko sahihi na zinakwenda na wakati.
 
                                   Mwisho
 
IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO ZANZIBAR
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top