Tume ya Warioba yavunjwa rasmi 
Jaji Joseph Sinde Warioba
HATIMAYE Rais Jakaya Kikwete ameivunja rasmi Tume ya Mabadiliko ya Katiba, iliyokuwa chini ya Mwenyekiti Jaji Joseph Warioba.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari jana jijini Dar es Salaam na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, imeeleza kuwa Machi 18, mwaka huu, Warioba aliwasilisha rasimu ya Katiba kwenye Bunge Maalumu na Machi 19 Rais Kikwete aliivunja tume hiyo.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa kutokana na hatua hiyo na kwa mujibu wa kifungu cha 31 cha sheria ya mabadiliko ya Katiba, rais alivunja rasmi tume hiyo  Machi 19 kwa  tangazo la Serikali namba 81 la Machi 21, mwaka huu.

Rais Kikwete aliunda tume hiyo kwa mujibu wa kifungu cha  5 na 6 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83 kwa tangazo la Serikali namba 110 la mwaka 2012.

Taarifa hiyo ilieleza kuwa tume ilikusanya maoni na kuandaa rasimu ambayo imewasilishwa kwenye Bunge Maalumu na kwamba kwa mujibu wa kifungu cha 31 cha sheria ya mabadiliko ya Katiba, Sura ya 3, rais amepewa mamlaka ya kuvunja Tume hiyo baada ya Rasimu ya Katiba kuwasilishwa bungeni.

Warioba aliwasilisha Rasimu ya Katiba kwenye Bunge Maalumu, M achi 18 ambapo katika hotuba yake alisema kuwa mfumo wa Serikali tatu unaopendekezwa na tume hauepukiki.

Alibainisha kuwa Serikali ya Muungano itakuwa na mambo saba ambayo ni Katiba na Mamlaka ya Jamhuri ya Muungano, Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano, Uraia na Uhamiaji, Sarafu na Benki Kuu, Mambo ya Nje, Usajili wa Vyama vya Siasa, Ushuru wa Bidhaa na Mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na Mambo ya Muungano.

Wakati akiwasilisha rasimu ya pili, Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, alisisitiza kuwa mapendekezo ya serikali tatu katika Muungano ni ya wananchi na taasisi mbalimbali, na wala si matakwa ya tume yake.

Jaji Warioba alieleza kuwa nusu ya wananchi waliotoa maoni yao kuhusu Muungano walitaka uwepo wa serikali tatu.

Kati ya wananchi 38,000 waliotoa maoni yao kuhusu muungano visiwani Zanzibar, 19,000 walizungumzia suala la muundo, huku zaidi ya nusu wakitaka marekebisho ya kikatiba yatakayowezesha uwepo wa serikali tatu.

Warioba alisema kwa upande wa Bara asilimia 61 ya waliotoa maoni juu ya Muungano walipendekeza muundo wa serikali tatu.

Hata hivyo wiki iliyopita Rais Kikwete wakati akizindua Bunge alisema muundo wa serikali tatu hautekelezeki na akasisitiza msimamo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ni serikali mbili.
Chanzo: Tanzania Daima
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top