Hatima ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, ambao ni wanachama
wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuendelea kushiriki vikao vya
Bunge au kutoendelea inatarajiwa kujulikana leo.
Wakati wajumbe hao, wengi wao kutoka vyama vya
upinzani wakitarajiwa kuamua ama kususa au kubaki ndani ya vikao, kuna
uwezekano wa kuteuliwa baadhi yao katika Kamati ya Uongozi kutokana na
majadiliano yaliyofanyika jana baina ya pande hizo mbili.
Majadiliano ya kamati hiyo, yalifanyika kutokana
na kujiuzulu kwa Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahimu Lipumba baada ya
kuteuliwa na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta.
Habari za uhakika kutoka ndani ya kikao cha
uongozi wa Ukawa jana zilieleza kuwa baada ya mjadala, viongozi
walikubaliana kutosusia Bunge hilo.
“Ingawa wajumbe wengi walitaka tuondoke sote leo
(jana) baada ya kuchoshwa na ukandamizaji unaofanywa na CCM, lakini
tumeamua kwanza kesho (leo) kuendelea na Kikao, alisema mmoja wa wajumbe
hao.
Mjumbe huyo alisema kwa mazingira ambayo CCM
wameyajenga katika Bunge hilo, si rahisi tena wajumbe wa Ukawa kuendelea
na Bunge , kwani ni wazi maamuzi mengi yatakayopita ni ya CCM.
“Kama wenyeviti wa kamati zote za Bunge ni zao,
kamati za kanuni, uandishi wa rasimu ni zao huwezi kupitisha hoja ndio
sababu wengi wetu wanataka tuondoke,” alisema mjumbe huyo.
Hata hivyo, katika kikao cha Uwaka, Mjumbe Tundu
Lissu alionekana kuwataka wajumbe kutochukua maamuzi ya haraka kutokana
na hali ambayo inajionesha bungeni kwani kunaweza kufanyika mabadiliko
ya kanuni.
Kaimu Katibu Mkuu wa Ukawa, Julius Mtatiro baada
ya kuulizwa jana kutokana na maamuzi hayo ya Ukawa alikataa kukanusha
wala kukubali kwa maelezo kuwa yatatangazwa rasmi katika kikao cha
jioni.
“Tumemaliza kikao cha uongozi cha Uwaka, sasa maamuzi tutayafikisha tena kwa wajumbe ili nao waamue,” alisema Mtatiro.
Mjumbe mwingine wa kamati ya uongozi wa Uwaka,
Emmanuel Makaidi alisema, baada ya kikao chao kama viongozi, walitarajia
jana jioni kuwaeleza maamuzi wajumbe wengine.
Wakati huohuo, Baadhi ya wajumbe kutoka Ukawa,
huenda leo wakateuliwa katika kamati ya uongozi ya Bunge hilo, baada ya
kukamilika mabadiliko ya kanuni.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
“Tumejadili suala la uteuzi kama tunaweza kuongeza wajumbe
kutoka huko Ukawa, nadhani kesho tunaweza kufikia maamuzi kwani hakuna
ambaye anapenda Bunge hili kuwa na mivutano,” alisema mmoja wa wajumbe
wa Kamati ya Uongozi.
Suala la Kamati ya Uongozi ya Bunge la Katiba
kusheheni sura za vigogo wa CCM jana liligeuka ‘habari kubwa’ ya Bunge
hilo baada ya wajumbe kuhoji uhalali wake bila kuwa na uwiano mzuri wa
pande mbili za Muungano, vyama vya siasa wala makundi maalumu.
Vile vile uteuzi wa wajumbe watano kuingia katika
kamati hiyo uliofanywa na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta nao
ulihojiwa kwamba haukuzingatia uwiano huo wa kitaifa.
Mwanyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba
alikoleza mjadala huo baada ya kukataa uteuzi wake kuwa miongoni mwa
wajumbe wa kamati hiyo, akisema, “Sitaweza kuingia katika kamati ya
uongozi na sipo tayari kutumiwa kama chambo.”
Kujitoa kwa Lipumba kulipokea kwa ndelemo kutoka
kwa baadhi ya wajumbe, ambao walisema kuwa ni uamuzi wa hekima
uliofanywa na mtu makini.
Kabla ya Lipumba kujitoa, baadhi ya wabunge
akiwamo Kangi Lugola (CCM), Habib Mnyaa (CUF), John Mnyika (Chadema),
Mchungaji Peter Msigwa (Chadema) na Vicent Mzena (201) walioomba
mwongozo na kuonyesha kutoridhishwa na uteuzi au muundo mzima wa kamati
hiyo.
Profesa Lipumba, aliweka wazi kuwa hataki kutumiwa na hayuko tayari jina lake litumiwe kwa maslahi ya CCM.
Awali, Mwenyekiti Sitta alitangaza majina ya
wajumbe watano wanaoungana na wenyeviti waliochaguliwa juzi kuunda
Kamati ya Uongozi wa Bunge.
Kamati hiyo ndiyo yenye majukumu ya kutengeneza ratiba na miongozo mingine ya uendeshaji wa Bunge hilo.
Walioteuliwa ni Profesa Lipumba (CUF), Mary Chatanda (CCM), Fakharia Shomari (CCM), Hamid Abuu Juma (CCM) na Amon Mpanju (201).
Aliomba kutoa maoni yake, Lipumba alisema,
“Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kukuheshimu sana, lakini naomba niseme
kuwa sitaingia katika kamati hiyo kwani nikiingia nitakuwa chambo cha
kusema kiongozi wa upinzani yupo humo,” alisema Lipumba.
Aliongeza: “Mimi siyo Mwenyekiti wa Ukawa (Umoja
wa Katiba ya Watanzania) kama ulivyosema, kama nia ilikuwa ni hivyo basi
angechaguliwa Mheshimiwa Mbowe (Freeman) ambaye ni Mwenyekiti wa
Ukawa.”
Akijibu hoja hiyo, Sitta alisema ni hiyari ya mtu kukubali au
kuukataa uteuzi ambao amepewa na kuwa kufanya hivyo hakuwezi kuchukuliwa
kuwa ni kosa kwa aliyekataa.
Muungano kwanza
Katika hatua nyingine, Mjumbe wa Bunge, Ezekiel
Olouch amewasilisha hoja binafsi ya kutaka Bunge kuanza kujadili hoja ya
muundo wa Muungano kabla ya mambo mengine ili kupata mwafaka wa pamoja.
La sivyo, Oluoch amependekeza ikishindikana
kuafikiana ni busara Bunge kuahirishwa na kurudi kwa wananchi ili wapige
kura ya maoni juu ya Muundo wa Muungano na ikitokea maoni yakawa
tofauti na rasimu, Tume ya Warioba ibadilishe rasimu yake.
“Tukishindwa kuelewana katika hili, tumuombe Rais
avunje Bunge, turudi nyumbani kusubiri kura ya maoni ya wananchi, kisha
turudi hapa kuendelea na mchakato wa Katiba,” alisema Olouch.
Akizungumza na Mwananchi jana, Olouch alisema
hakuna namna yoyote ya kuanza mjadala wa Rasimu ya Katiba, bila kupata
muafaka juu ya muundo wa Muungano.
“Tayari nimepeleka hoja binafsi juu ya hili,
hatuwezi kuanza kujadili rasimu bila kujadili kwanza vifungu 64 kati ya
271 vya rasimu vinavyozungumzia muundo wa serikali tatu. Bila muafaka
kwa suala hili, sidhani kama tunaweza kufika mbali katika kupitia
vifungu vya rasimu,” alisema.
Hoja ya Oluoch imeungwa mkono na mhadhiri
mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Chris Peter Maina
aliyesema rasimu yote ya Katiba imebebwa na muundo wa serikali tatu,
hivyo watakaopendekeza muundo wa serikali mbili wanatakiwa kutambua kuwa
idadi kubwa ya mambo yaliyomo katika rasimu hiyo yatabadilika.
“Kazi ya Bunge la Katiba siyo kubadilisha kila
kitu, kazi yao ni kuiboresha rasimu ya Katiba. Tatizo ni kwamba
wanadhani wao wanaweza kubadili kila kitu,” alisema.
Aliongeza kuwa wajumbe wa Bunge hilo wanatakiwa
kutambua kuwa wajumbe wakibadilisha tutapata Katiba mbaya na sidhani
kama wanaotaka serikali mbili wanalijua jambo hili.
“Ukichomoa nati moja sehemu, ni wazi kuwa kitu
husika hakitakaa kama kilivyokuwa awali ni lazima kitapwaya. Ni lazima
wakubaliane na hilo na hoja zilizomo kwenye rasimu,” alisema Profesa
Maina.
Chanzo: Mwananchi
0 comments:
Post a Comment