Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa.
OFISI  ya Msajili  wa  Vyama Vya Siasa  nchini imevitaka  vyama vya siasa kutii agizo la  kutoanzisha kambi za mafunzo ya kulinda amani maarufu kwa jina la mgambo kwa minajili ya kujilinda.



Kauli hiyo imetolewa na Rajab Juma kwa niaba ya Msajili wa Vyama vya Siasa Nchini, John Tendwa kufutia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) kutangaza hivi  karibuni kuwa kinakusudia kuanzisha kambi za mafunzo ya kujilinda kwa vijana  wake  nchi nzima.



Taarifa ya ofisi hiyo imedokeza kuwa  Katiba ya nchi imempa jukumu  kila mwananchi kulinda amani na usalama wa nchi,pia kujilinda yeye mwenyewe na mali zake kwa kutoa taarifa katika vyombo vya dola pale anaposikia au kuona mtu anataka  kufanya au anafanya   uhalifu au amemdhuru mtu.



Amesema suala hilo lilitangazwa na Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe na kuandikwa katika vyombo vya habari kabla ya chama hicho, kuwasiliana na taasisi  husika ikiwemo ofisi hiyo ili kupata ushauri kuwa jambo wanalotaka kufanya ni sahihi .



Bwana Rajab amesema  Katiba ya nchi  na katiba za  vyama vya siasa, hazina maana kila mwananchi au kikundi cha watu kufanya  mafunzo ya kijeshi au ukakamavu ili kufanikisha jukumu hili.



Bwana Rajab amesema kuwa kama CCM  wanakiuka sheria ni jukumu  vyama vingine au Mtanzania yeyote,kutoa taarifa na ikiwezekana na ushahidi katika taasisi husika, ikiwemo Ofisi ya Msajili wa  Vyama Vya Siasa ili suala hilo lishughulikiwe kisheria.



Taarifa ya msajili imefafanua kuwa Jukumu la vikundi kama hivyo  ni kutoa taarifa kwa vyombo vya dola na si kupambana na wahalifu au watu wanaotaka kuwadhuru kwani wenye jukumu la kupambana na wahalifu ni vyombo  vya ulinzi na usalama ambavyo vipo kisheria, mojawapo ikiwa ni Jeshi la Polisi.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top