Naibu katibu mkuu wa chama cha Wananchi (CUF) Bara, Julius Mtatiro.

Elimu ya uraia  na ushirikishwaji wa wananchi ni mbinu zilizotajwa kuwa muafaka zaidi katika utatuzi wa migogoro ya mgawanyo wa rasilimali zinazopatikana hapa nchini.

Naibu katibu mkuu wa chama cha Wananchi (CUF) kwa upande wa Tanzania Bara, Julius Mtatiro, amesema Jumapili wiki hii wanataraji kutoa elimu kwa wananchi juu ya faida za matumizi ya gesi asilia hapa nchini.

Naibu Katibu Mkuu huyo amesema msimamo wa CUF  kwa wananchi ni kutofanya vurugu bali kuhimiza demokrasia yenye uwazi kama njia muafaka ya kutatua migogoro inayojitokeza katika jamii.

Bwana Mtatiro amesema wanaamini ushirikishwaji wa wananchi wa mikoa ya Lindi na Mtwara ulikuwa mdogo ndiyo sababu kuu ya kujitokeza kwa vurugu na uvunjifu wa amani.

Katibu huyo amesema CUF inajiandaa kukusanya maoni ndani ya wiki mbili na kuyapeleka kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete kupendekeza juu ya utatuzi wa suala hilo.

Hata hivyo serikali kupitia kwa Waziri mkuu Mizengo Pinda imekwishafanya mazungumzo na wananchi wa Mtwara kuhusiana na mipango ya ujenzi wa bomba la kusafirisha gesi mpaka Dar es Salaam.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top