WAKATI Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Celina Kombani, amekataa kutaja nyongeza ya mishahara ya kima cha chini kwa madai kuwa ni siri, imebainika kuwa mishahara hiyo imeongezeka kwa sh 30,000 tu.

Nyongeza hiyo inafanya kima cha chini cha mishahara ya watumishi wa umma, kufikia sh 200,000 kutoka sh 170,000 za mwaka wa fedha uliopita 2012/2013.

Baadhi ya wabunge walio kwenye Kamati ya Kudumu ya Katiba, Sheria na Utawala iliyokuwa ikijadili kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, waliliambia gazeti hili kuwa kima cha chini cha mshahara kimeongezeka kwa sh 30,000.

Hata hivyo, wakati akifanya majumuisho ya wizara yake jana, Waziri Kombani licha ya baadhi ya wabunge kumtaka atangaze kiwango kilichoongozeka, alisema kuwa hawezi kufanya hivyo kwani mshahara wa mtu ni siri.

“Kuhusu masilahi ya watumishi wa umma. “Hapa msinilazimishe kima cha chini, hapana. Hata sisi wabunge tunapoona kwenye magazeti yakitangaza mishahara yetu, hatufurahi kwa sababu mshahara ni siri yako,” alisema Kombani.

Waziri alirejea kauli yake juzi wakati akiwasilisha mwelekeo wa bajeti ya wizara yake kwamba kwa mwaka wa fedha 2013/2014 serikali imetenga sh trilioni 4.7.

Kiasi hicho ni kwa ajili ya nyongeza ya mishahara na kugharamia mishahara kwa watumishi wa Serikali Kuu, Serikali za Mitaa na Wakala wa Taasisi za Serikali.

Kwa mujibu wa Waziri Kombani, kiasi hiki cha sh trilioni 4.7, pia kitatumika kugharamia ajira mpya 61,915, upandishwaji vyeo na nyongeza za kawaida za mishahara za mwaka, pamoja na nyongeza za mishahara kuanzia Juni 2013.

Mwaka wa fedha uliopita 2011/12, serikali ilitenga sh trilioni 3.7 ambapo mshahara wa kima cha chini uliongezeka kwa sh 20,000 na kufanya kima cha chini kupanda kutoka sh 150,000 hadi sh 170,000.

Hata hivyo Waziri Kombani aliwataka watumishi kuwajibika kwani wapo wanaolalamikia kutaka nyongeza ya mishahara, lakini hawataki kuwajibika.

Waziri Kombani alisema serikali imeandaa operesheni maalumu ya kufanya uhakiki wa vyeti vya watumishi wote nchini ili kubaini walioingia kazini kwa kutumia vyeti vya kughushi.

Alisema wapo baadhi ya waliotumia vyeti vya marehemu na wengine ndugu zao ambao pia wameajiriwa katika majina mawili ya watu wanaofanana.

Wakati serikali ikiongeza mishahara kwa kiwango kidogo, Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi (TUCTA), limekuwa likipendekeza kima cha chini kiwe sh 300,000 na katika mwaka huu wa fedha, imependekeza kima cha chini kiwe sh 400,000 ili kukabiliana na gharama za maisha zilizoongezeka mara dufu.
Chanzo: Tanzania Daima
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top