Latest News

KATIKA kuadhimisha miaka 49 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Rais Jakaya Kikwete kwa kutumia madaraka aliyopewa chini ya ibara ya 45(1) (d) ya Katiba ya Jamhuri ametoa msamaha kwa wafungwa 4180.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwenye vyombo vya habari jijini Dar es Salaam jana, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi, alisema kuwa wafungwa watakaofaidika na msamaha huo ni waliokuwa wanatumikia kifungo kisichozidi miaka mitano na kwamba watakuwa wameshatumikia robo ya vifungo vyao.

Watakaonufaika wengine ni wale ambao walihukumiwa kifungo kinachozidi miaka mitano ambao wamepunguziwa moja ya sita ya vifungo vyao zaidi ya punguzo la kawaida, wagonjwa wenye magonjwa kama ukimwi, kifua kikuu na kansa.

Wamo pia wafungwa wazee wenye miaka 70 au zaidi, wafungwa wa kike walioingia na mimba gerezani pamoja na wale walioingia na watoto wanaonyonya na wasionyonya.

Dk. Nchimbi alibainisha kuwa wanufaika wengine ni wale wenye ulemavu wa mwili na akili na ambao walihukumiwa na kuwepo gerezani kwa ridhaa ya Rais Kikwete.

Aidha, alieleza kuwa msamaha huo hautahusisha wafungwa waliohukumiwa kunyongwa, wanaotumikia kifungo cha maisha, wanaotumikia kifungo kwa makosa ya kujihusisha na biashasra ya madawa ya kulevya, kupokea au kutoa rushwa.

Wengine ni wanaotumikia kifungo kwa makosa ya unyang’anyi na unyang’anyi wa kutumia silaha, kupatikana na silaha au risasi, kunajisi, kubaka na kulawiti, waliopatikana na hatia ya kuwapa mimba wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ambao walitenda makosa hayo wakiwa na miaka 18 na zaidi.

Wakati huo huo, Rais Kikwete jana aliwaongoza maelfu ya Watanzania katika sherehe hizo za Muungano, zilizofanyika kitaifa katika Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam.

Rais baada ya kuwasili uwanjani alipigiwa mizinga 21 na kisha kukagua gwaride na kupokea heshima ya majeshi ya ulinzi na usalama yaliyopita mbele yake kwa mwendo wa pole na kasi.

Kisha zilifuata buradani mbalimbali kama vile halaiki ya watoto 2695, ngoma za asili na maonesho ya vikosi vya ulinzi ambavyo vilirusha ndege za kivita na mafunzo hewani.

Akizungumzia Muungano huo, mmoja wa wanazuoni Profesa Mwesiga Beregu, alisema Watanzania wana kila sababu ya kujivunia kwani ni wa pekee katika bara la Afrika.

Prof. Beregu alipinga dhana ya baadhi ya watu kuwa muungano hautakiwi akisema kuwa wenye mawazo hayo si wengi.

“Wakati wa mchakato wa Katiba tulipopita Zanzibar kwa kweli sijakutana na watu kama hao, kama wapo wanaotaka kuuvunja Muungano basi watakuwa ni wachache,” alisema Baregu ambaye pia ni mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Naye mwananchi, Edna Sitta, alisema Muungano huu unawanufaisha zaidi Wazanzibari ambao wana uwezo wa kujipatia hata ardhi Tanzania Bara bila vikwazo wakati hali hiyo ni tofauti kwa wabara kumiliki ardhi Zanzibar.

Tatu Ali (86) mkazi wa Temeke, alisema Muungano huu hauna matatizo bali watu wanatakiwa kuwa na uvumilivu pia na kujiepusha kupenda makubwa ambayo mara kadhaa yamekuwa yakijenga taama.

Viongozi mbalimbali walihudhuria sherehe hizo wakiwemo marais wastaafu, Alhaji Alli Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa, Amani Abeid Karume, Waziri Mkuu Mizengo Pinda, mawaziri wakuu wastaafu na wengineo.

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top