Kingunge Ngombale Mwiru
Akiwa msemaji wa
mwisho katika semina maalum ya kupata uzoefu wa michakato ya katiba,
mzee wetu huyu (namheshimu sana) aliibua vifijo, nderemo na hoihoi pale
alipomhoji mwanasheria mkuu mstaafu wa Kenya na Seneta wa sasa Busia
Mhe. Amos Wako kuhusu umuhimu wa katiba katika kukuza uchumi wa Afrika.
Mzee Kingunge alieleza kuwa haya MAKATIBA kibao yana "role" gani katika
kuinua uchumi wa nchi husika, akitolea mfano wa nchi kama Vietnam,
Malaysia, Singapore n.k ambazo ziliwahi kuwa sawa kiuchumi na Tanzania
lakini leo wenzetu wako mbali mno. Mzee wetu anahoji baada ya miaka
hamsini nchi zetu hizi ni masikini sana.
Mzee Kingunge anasema
hata Rasimu ya Katiba ya Jaji ya Warioba ya juzi imejaa masuala ya
mitandao ya uongozi na kugawana madaraka tu, anasema hakuna kipengele
kinachoelekeza uchumi wa nchi zetu uendeje, usimamiweje, baada ya miaka
hamsini uwe wapi n.k.
Anahoji uzoefu wa mwanasheria Amos Wako katika katiba hizi!
Amos Wako amemjibu kwa kifupi, kwamba Katiba ni msingi mkubwa sana wa
kujenga uchumi Imara, lakini pia amemkumbusha kuwa kupitisha katiba ni jambo
moja, na kuilinda, kuifuata na kuitekeleza ni jambo lingine.
Amesisitiza kuwa katiba lazima ifuatwe, na viongozi na wananchi wote
wahakikishe inafuatwa vinginevyo haitakuza uchumi.
Kwa mtizamo
wangu, Amos Wako amesahau jambo moja muhimu, kwamba uchumi wa nchi
nyingi za Afrika unakuwa duni mno kwa sababu viongozi wenye dhamana,
marafiki zao na ndugu zao na wanamtandao wao wanatenda na kufanya kila
wawezalo kukwapua kila faida inayotokana na jasho la wananchi na kujaza
matumbo ya mitandao yao.
Leo pana viongozi kibao wana mabilioni
ya fedha katika akaunti za nje. Wazee wetu kama kina Andrew Chenge
(Mwanasheria Mkuu mstaafu wa Tanzania) alipata mgao wa dola milioni
mbili katika kashfa ya ununuzi wa rada ya bei kubwa kupita mfano,
alipoulizwa kuhusu mapesa hayo(sawa na milioni elfu mbili za Tanzania)
alijibu kuwa hivyo ni Vijisenti tu.
Mzee Kingunge mwenyewe
anayehoji ati kwa nini nchi za Afrika Kiuchumi zinazidi kuwa hoi, ni
juzi tu kwa miaka kadhaa kampuni yake ilikuwa na kashfa kubwa ya
kukusanya ushuru stendi ya mkoa bila kutoa gawiwo la haki na
linalostahili kwa serikali.
Tathmini ilionesha kuwa, karibu
fedha zote ambazo kampuni yake inakusanya zinalimbikizwa kwa faida ya
kampuni. Hata tenda yenyewe ya kutoza ushuru aliipata kwa njia zisizo
halali na palikuwa na mvutano mkubwa sana juu ya uhalali wa kampuni hiyo
kukusanya ushuru ambao haieleweki hadi leo ulikuwa unakwenda wapi. Kwa
kiasi kikubwa kupewa tenda ile kulihusishwa na yeye kuwa karibu na mfumo
wa serikali.
Leo Kingunge yuleyule anahoji kwa nini nchi zetu ni
masikini mno. Hakumbuki kampuni yake ilitafuna fedha ngapi ambazo
wananchi walilipa ushuru Ubungo stendi na anasahau kuwa ikiwa jambo hilo
lingetendwa kwa haki fedha zile zingeweza kurudi na kujenga barabara,
shule, maji safi, madawa hospitalini, pembejeo kwa wakulima n.k.
Mzee wetu Kingunge anasahau kuwa fefha hizo ambazo kampuni yake ilizitia
kapuni zingeweza kabisa kutosha kuondoa sehemu ya umasikini mkubwa
unaoikabili nchi yetu. Kwa bahati mbaya sana, baada ya
miaka hamsini ya uhuru ambao yeye alikuwa sehemu yake na miaka hamsini ya uongozi wa CCM ambapo naye amekuwa kiongozi, miaka hiyo yote imepita na kuisha, na leo ndiyo Mzee wetu anakuja kumuuliza kijana mdogo tu kama Amis Wako, amsaidie kujibu swali la WHY AFRICA IS POORER DESPITE THE PRESENCE OF MAKATIBA LUKUKI!
miaka hamsini ya uhuru ambao yeye alikuwa sehemu yake na miaka hamsini ya uongozi wa CCM ambapo naye amekuwa kiongozi, miaka hiyo yote imepita na kuisha, na leo ndiyo Mzee wetu anakuja kumuuliza kijana mdogo tu kama Amis Wako, amsaidie kujibu swali la WHY AFRICA IS POORER DESPITE THE PRESENCE OF MAKATIBA LUKUKI!
Kwa mtizamo wangu, ni bora Jaji Warioba ambaye
amewahi kuwa sehemu ya matatizo ya nchi hii, anapotoka hadharani na
kutoa SULUHU ya baadhi ya matatizo hayo, kuliko Mzee Kingunge ambaye
amekuwa sehemu ya matatizo kwa miaka hamsini na leo hii bado anatuuliza
sisi vijana kwa nini nchi zetu ni masikini.
Mzee Kingunge
Ngombale Mwiru anapaswa kukumbuka kuwa vijana wa sasa tunasoma na
tunafanya uchambuzi mkubwa sana, hatuwezi kudanganyika kwa falsafa
zisizoeleweka. Ukweli ni kuwa Afrika ina utajiri mkubwa, Tanzania ni
tajiri hasa, ila utajiri wote huo unaporwa na kikundi cha watu wachache
na wawekezaji bila kuacha faida yoyote kwa mwananchi wa kawaida.
Imefika wakati sasa katiba za Afrika zilinde kwa nguvu zote rasilimali
za nchi husika na ziweke utaratibu maalum wa kiuwajibikaji ambapo kila
serikali inayokuja madarakani itawajibika moja kwa moja na kwa uwazi,
kuhakikisha kuwa rasilimali, nguvu kazi na maliasili za Afrika
zinatumika kwa kuwanufaisha wananchi moja kwa moja badala ya kuendelea
kuwanenepesha VIONGOZI WACHACHE na mitandao yao.
J. Mtatiro
0 comments:
Post a Comment