Gaudensia: “Kwa hiyo umeacha makusudi ili kunithibitishia kuwa ulikuwa ukitembea na wanawake ovyoovyo?”

Reina: “Siyo kutembea ovyoovyo, kwani wewe ulitegemea muda huo wote ningekuwa bila mwanamke? Acha utani kabisa, hata wewe kule Dodoma mimi nitajuaje kama siku zote hukuwa na wanaume? Tena nyie wanafunzi wa Udom kwa wabunge ndiyo zenu.”

Baada ya kuzungumza hivyo, Gaudensia alianza kufanya usafi kwa kuchukua kondomu zote, zile zilizotumika na ambazo hazikuwa zimetumika kisha akaenda kuzichoma moto. Hata hivyo, maisha hayakuwa na amani kabisa, vitimbi viliendelea kuchukua nafasi.

Kuna wakati Gaudensia alipigiwa simu na wanawake wa Reina kumtukana lakini hakuwajibu, alinyamaza na hata mume wake aliporejea nyumbani wala hakumuuliza. Alichojali yeye ni kujenga ndoa ya yake, aliamini upo wakati mume wake atabadilika na maisha yatakuwa mazuri.

Uvumilivu wake ulifika ukingoni siku moja baada ya kukuta karatasi kwenye suruali ya mume wake alipokuwa anafua nguo. Ile karatasi ilikuwa imeandikwa “WANAWAKE AMBAO NIMESHAWADUU”. Gaudensia akashtuka, akahesabu majina na kukuta yapo 71.

Gaudensia akagundua kuwa miongoni mwa wanawake hao, wapo marafiki zake wawili ambao alisoma nao Chuo cha Uhasibu, Kurasini, Dar es Salaam. Kwenye orodha hiyo kulikuwa na wahudumu wa baa na machangudoa. Ilimuuma sana.

Reina aliporudi nyumbani, ilikuwa usiku wa manane, kwa hiyo akamuacha alale, asubuhi alipoamka akamuonesha ile karatasi na kumuuliza sababu ya kuandika na kuihifadhi. Bila kutarajia, Reina aligeuka mbogo. Alimkaripia kwa kumchunguza kisha akaanza kumpiga.

Alimpiga na kumuumiza vibaya, baadaye alizimia. Reina bila kujali kama mkewe hana fahamu, aliita gari na kuchukua kila kitu, aliamua kuhama nyumba. Hata hivyo, mmoja wa vijana waliokuwa wanabeba vitu, aliingiwa na huruma, kwa hiyo baada ya kushusha vitu, alikwenda kituo cha polisi kutoa taarifa.

Polisi walifika pale chumbani na kumkuta Gaudensia bado hana fahamu, walimbeba mpaka Hospitali ya Mkoa wa Arusha, Mt. Meru ambako alihudumiwa na kurejewa na fahamu. Polisi wamlitia nguvuni Reina lakini baada ya Gaudensia kupona, alikana kupigwa na Reina.

Hakutaka mume wake aingie kwenye matatizo. Pamoja na imani hiyo lakini Reina hakumjali na alimpiga marufuku kufika nyumbani kwake alipohamia na alikataa kabisa kumuelekeza. Ilimuuma sana Gaudensia, aliomba japo nauli ya kurudi Dar kwa wazazi wake lakini alinyimwa.

Ilibidi Gaudensia ampigie simu mama yake na alipomsimulia mateso aliyonayo, haraka sana alimkatia tiketi ya ndege na ile anafika Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere, mama yake alimwambia: “Mwanangu ni sawa kuvumilia lakini umetukosea sana, uvumilivu wako ni kama vile huna kwenu, kwa nini mwanaume akunyanyase kwa kiwango hicho na wewe uwe kimya?”

Dunia ina kawaida ya kurejesha majibu haraka, miezi sita baada ya Gaudensia kutimuliwa na Reina, tayari alikuwa ameshapata kazi nzuri katika Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), tayari alishajijenga sawasawa, akanunua kiwanja akiwa na ndoto za kujenga nyumba ndani ya miezi 10 inayofuata.

Reina alishafukuzwa kazi wakati huo, mambo yalishaharibika, wazazi wake hawakutaka kumuona. Mtaani alionekana kama kibaka kwa jinsi alivyochakaa. Maisha yalimdanganya, akarudi kwa Gaudensia kuomba msamaha. Itaendelea wiki ijayo.
GPL 
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top