Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana.
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana,
amemkacha Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA),
Dk. Willibrod Slaa.
Wawili hao walitarajiwa kukutana kwenye kipindi kipya kiitwacho
‘Uzalendo’, kinachotarajiwa kuanza kurushwa wakati wowote kuanzia mwezi
ujao katika kituo cha televisheni cha ITV.
Taarifa za Kinana kumkimbia Dk. Slaa katika mdahalo huo zilisambazwa jana katika mitandao mbalimbali ya kijamii nchini.
Taarifa hiyo na vyanzo vyetu vingine vya habari, vilieleza kuwa
viongozi hao walialikwa na ITV kwa ajili ya mdahalo ambao ungerekodiwa
na baadaye kurushwa na kituo hicho.
Kwa mujibu wa habari hizo, viongozi hao walipewa mwaliko wa kuhudhuria
kipindi hicho siku kumi zilizopita na wote kuthibitisha ushiriki wao,
lakini Dk. Slaa jana alifika katika studio za kituo hicho na kukutana na
Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, badala ya Kinana.
Akizungumza kwa simu na gazeti hili jana, Dk. Slaa alisema: “Ni kweli
tulikuwa tumealikwa kwenye mdahalo pale ITV (leo) jana saa 3, nilipofika
nilikutana na Nape, nikamsalimu nikajua kuwa alikuwa amemsindikiza
Kinana, lakini nilipomuuliza mwendesha kipindi kwamba Kinana yuko wapi,
alisema amepata udhuru hivyo hajafika.
“Nilimwambia Nape wewe si saizi yangu, sitaweza kuongea katika kipindi
hiki kama Kinana hayupo, hivyo kipindi hiki kiahirishwe hadi Kinana
atakapokuwa na nafasi ya kuja,” alisema Dk. Slaa.
“Haiwezekani mwenzangu akaahirisha ghafla kuja kwenye kipindui halafu
nisipewe taarifa na badala yake nikatumiwa Nape, Nape si saizi yangu,”
alisisitiza Dk. Slaa.
Taarifa zaidi zinasema kuwa baada ya kuahirishwa kipindi hicho, Nape
na Dk. Slaa walisalimiana na kuagana. “Naamini siasa si uadui, niliongea
na Nape nikamuuliza Kinana yuko wapi, alisema alikuwa amepata udhuru,
akanipigia simu nije,” alisema.
Akizungumza na gazeti hili kuhusu suala hilo, Nape alisema alikwenda
ITV badala ya Kinana, kuangalia maudhui ya kipindi hicho ili aweze
kushauriana na Kinana na kuamua kuja au la.
“Mimi ndiyo msemaji wa chama, katibu mkuu hawezi kualikwa mimi nisiwe
na taarifa, mimi ndiyo napaswa kwenda na nilikwenda nilipokutana na Dk.
Slaa tukaelezwa, Dk. Slaa alishauri kuwa inafaa kualika watu wenye
hadhi zinazofanana, yaani makatibu, hivyo mimi niliondoka nikamwacha Dk.
Slaa, nadhani alirekodiwa kwa kuwa walisema wanaweza kurekodi mtu mmoja
mmoja na katibu mkuu wetu anaweza kwenda siku nyingine kurekodi,”
alisema Nape.
Kinana mwenyewe alipotafutwa kwa simu yake ya mkononi kuzungumzia
suala hilo, hakuweza kupatikana kwani simu yake iliita bila kupokewa.
0 comments:
Post a Comment