Katibu Mkuu wa Bavicha, Deogratias Munishi 
BARAZA la Vijana wa CHADEMA (Bavicha) limemtaka Rais Jakaya Kikwete kuacha kulalamika kuhusu dawa za kulevya zinazopitishwa kwenye viwanja vya ndege kwa kuwa ameshindwa kushughulikia majina ya wafanyabiashara hiyo aliyowahi kukiri kuwa nayo.
 
Katibu Mkuu wa Bavicha, Deogratias Munishi, alitoa kauli hiyo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, kwamba Rais Kikwete alinukuliwa kuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na ule wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) vinavyotumika kupitishia dawa hizo.

Alisema Bavicha imefedheheshwa na kauli hiyo ya mkuu wa nchi, kwa kuwa haina mashiko wala haisaidii katika kupambana na biashara hiyo haramu.

“Bavicha inaona kauli hii ya Rais Kikwete ni dhihaka kwa vijana wa taifa hili ambao ndio waathirika wakubwa wa dawa za kulevya kwani haina dhamira pana ya kudhibiti uingizwaji wa dawa hizo.

“Ikumbukwe kuwa tangu rais atamke kuwa anayo orodha ya wafanyabiashara wa dawa za kulevya hakuna hatua zozote alizochukua dhidi ya watu hao, zaidi taifa limeendelea kuathirika na biashara hiyo haramu.

“Bavicha inajiuliza kulikoni mkuu wa nchi anaayakumbatia majina ya wanaoliangamiza taifa bila kuchukua hatua zozote? Je, anawaogopa? Ama ni maswahiba zake kiasi cha kuona aibu kuwachukulia hatua?

Kutokana na hali hiyo, Bavicha inamkumbusha Rais Kikwete kwamba, inachafua taswira yake kama kiongozi wa nchi pia kushusha hadhi ya Ikulu kwa kuwa inaonekana ni kituo cha kuhifadhi wahalifu.

Alisisitiza kuwa Bavicha inamtaka Rais Kikwete kutambua kuwa maneno bila matendo katika kupambana na dawa za kulevya nchini  hakusaidii bali kunaendelea kupalilia uharamia huu, hivyo imefika wakati wa kuwataja hadharani wale wote anaowafahamu  wanaojihusisha na biashara hii kisha awachukulie hatua.

Juzi Rais Kikwete alinukuliwa akisema kwamba haridhishwi na kasi ya kupambana na dawa za kulevya katika viwanja vya ndege hapa nchini.
Chanzo: Tanzania Daima
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top