Na Stephen Maina
Katiba hii ni ya kihistoria tofauti na zile zilizotangulia ambazo zimekuwa zikifanyiwa marekebisho bungeni bila wananchi kujua kinachoendelea kwani hawakushirikishwa kuzitunga.

Hivi karibuni Mjumbe wa Tume ya Marekebisho ya Katiba (jina limehifadhiwa) aliwahi kuhojiwa na mwandishi wa makala haya kuhusu matarajio ya Watanzania kuhusu Katiba Mpya na matumizi ya Kiswahili.
Naye alisema: “Nawataka wajumbe wa Bunge la Katiba watakaokwenda Dodoma kutumia lugha sahihi inayoeleweka kwa wananchi, badala ya kuchanganya lugha. Wajumbe wasichanganye lugha ‘Kiswanglish’ kama ilivyotokea katika mikutano mingine ya kitaifa hata bungeni.
Hali hii inajitokeza sana siku hizi katika vikao mbalimbali vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kiswahili ndiyo lugha rasmi ya Bunge hilo lijalo na tungependa wabunge wazingatie hilo, maana tunaona baadhi ya mawaziri na wajumbe wengine wakichanganya lugha.”
Kauli aliyoitoa mjumbe huyu ni ya kupigiwa mfano kwani ametoa ya rohoni. Ni mzalendo kwelikweli, kwani ameweka mbele masilahi ya Watanzania wote. Hawa wajumbe wanawawakilisha Watanzania 45 milioni, ambao wana haki ya kujua hatima ya nchi yao kwani yatakayoamriwa katika Bunge hilo la Katiba yatamgusa kila mwananchi.
Katiba hii ni ya kihistoria tofauti na zile zilizotangulia ambazo zimekuwa zikifanyiwa marekebisho bungeni bila wananchi kujua kinachoendelea kwani hawakushirikishwa kuzitunga.
Matumizi ya lugha fasaha na sanifu ya Kiswahili wakati wa mijadala ya Bunge la Katiba ni jukunu la kila mjumbe. Kwa wale wenye matatizo kidogo kwa maana ya wasomi walioathiriwa na lugha za kigeni wajitahidi kujiandaa zaidi kabla ya kuzungumza. Wajitayarishe kwa kutumia kumbukumbu za kuwaelekeza ni nini cha kuzungumza, wakitumia mwongozo uliowekwa. Wenzetu wasomi wanatumia maneno ‘talking notes’ kama kiongozi cha mazungumzo.
Maandalizi ya aina hii yatawawezesha wajumbe kutumia lugha ya Kiswahili bila hofu, akiamini kuwa wasikilizaji watafaidika na hoja zake.
Mjumbe huyu wa Bunge Maalumu la Katiba ametoa rai ya kuachana na tabia ya kuchanganya lugha katika mazungumzo ambayo imeshamiri kwa Watanzania, wasomi walio wengi.
Hili ni suala lililoguswa na wengi kwamba wabunge wakiwamo mawaziri huchanganya maneno na hata vifungu vya maneno ya kigeni wanapochangia hoja bungeni. 
Inawezekana wanafanya hivyo kwa kukosa maneno ya Kiswahili yanayofaa, lakini wanakera zaidi wanapozungumza. Kwa mfano anaweza kusema;
“Wananchi wa jimbo langu hawana ‘idea’ ya mradi huu wa umwagiliaji ambao ‘donors’ wametoa zaidi nusu ya fedha zote.”
Wako baadhi ya wasikilizaji wataelewa kilichotamkwa bungeni, lakini kwa jumla ni makosa kutumia maneno kama ‘idea’ na ‘donors’.
Kwa utafiti wangu mdogo nimegundua kuwa hatakuwapo Mjumbe wa Bunge la Katiba mwenye elimu chini ya kidato cha nne.

Hiki ni kidato ambacho Kiswahili kilifundishwa kama somo, kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne, baada ya kumaliza darasa la kwanza hadi la saba kwa shule za msingi ambapo Lugha ya kufundishia ni Kiswahili.
Iweje wewe Mtanzania uliyepitia mfumo huu wa elimu yetu uanze kujidai kutumia maneno ya Kiingereza kwenye mazungumzo yako, tena yaliyo rasmi na ambayo yatahifadhiwa katika mfumo wa kiteknolojia wa ‘Hansard’.
Namwomba Spika wa Bunge la Katiba ashirikiane na wajumbe kutunga kanuni za bunge hilo zitakazoweka wazi kuwa lugha ya majadiliano ni Kiswahili fasaha na sanifu na atakayejaribu kutumia lugha mseto, atolewe nje, kwani hayuko hapo kwa manufaa ya Watanzania, bali yake binafsi.
Mwisho, ningetoa ushauri kwa Taasisi ya Taaluma ya Kiswahili (TATAKI), ambayo imetunga Kamusi ya Kiswahili Sanifu waweke katika mfumo katika Tovuti, kuonyesha misamiati na istilahi zilizosanifiwa ili wajumbe wa Bunge la Katiba waweze kupata tafsiri, maana na matumizi ya maneno ya Kiswahili.
Wajumbe watapata fursa ya kutumia lugha ya Kiswahili kwa kujiamini na wenzetu watakaokuwa wanafuatilia majadiliano kutoka katika vyombo vya habari nje ya nchi watakuwa na kumbukumbu za uhakika kwa vizazi vya sasa na vile vijavyo.
0754 861664 0716 694240
Mwananchi

TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top