Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Pandu Ameir Kificho amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa muda wa Bunge Maalumu la Katiba.
Kwa ushindi huo, Kificho atakuwa na kazi kuandaa
kanuni ambazo zitatumika kwa ajili ya kumchagua mwenyekiti wa kudumu wa
Bunge hilo na kusimamia vikao vyake.
Muda wa mwenyekiti huyo wa muda utamalizika Ijumaa
baada ya wajumbe kupitisha kanuni za kuendesha Bunge hilo na kumchagua
mwenyekiti na makamu wake.
Akitangaza matokeo hayo, Katibu wa Bunge, Dk
Thomas Kashililah alisema Kificho alichaguliwa kwa kura 393 sawa na
asilimia 69.13 na kumshinda mpinzani wake Profesa Costa Mahalu aliyepata
kura 84 sawa na asilimia 14.79. Kura saba ziliharibika.
Wengine waliojitokeza kuwania nafasi hiyo ni Magdalena Rwebangira, Sadifa Juma Hamisi na David Mbatia.
Hata hivyo, Mbatia ambaye awali alitambulishwa
kuwa ni James Mbatia alienguliwa kutokana na kutokuwa na sifa na Sadifa
kujitoa muda mfupi baada ya kujieleza mbele ya wajumbe wa Bunge hilo.
Kabla ya kuanza kwa uchaguzi huo, Dk Kashililah na
Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad walimteua mmoja wa
wajumbe wa Bunge hilo, Oliver Luena kuwa mwenyekiti msimamizi wa
uchaguzi huo.
Uchaguzi huo ulioanza saa tisa alasiri hadi saa
moja usiku, ulikabiliwa na changamoto kadhaa baada ya upigaji kura
kuharibika kutokana na idadi ya wajumbe waliopiga kura kuongezeka kutoka
548 hadi 568 wakati wa kuhesabu.
Hali hiyo ilimlazimu Luena kuagiza uchaguzi huo
urudiwe kauli ambayo ilizua mjadala mkali kwa baadhi ya wajumbe kupinga
kurudiwa baadhi wakitaka urudiwe na wengine kupinga.
Mbunge wa Mtera (CCM), Livingstone Lusinde alitaka
uchaguzi huo usirudiwe kwa sababu hatua hiyo ingechukua muda mrefu bila
sababu za msingi huku Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed
akitaka uamuzi huo kufanywa kwa kura na Mbunge wa Hai (Chadema), Freeman
Mbowe akitaka urudiwe. Mbunge wa Viti Maalumu, Sabrina Sungura
(Chadema) alitaka kura tisa zilizozidi kugawanywa kwa wagombea watatu wa
uenyekiti badala ya kurudia uchaguzi.
Katika ufafanuzi wake, Mbowe alisema uchaguzi huo
ni wa kihistoria hivyo ni vyema ukarudiwa ili kuweka kumbukumbu sahihi
za Bunge.
“Uchaguzi huu ni wa kihistoria, hivyo lazima
urudiwe ili historia isije ikatuhukumu. Tuhakikishe waliopo ndani ya
ukumbi ndiyo wanaopiga kura,” alisema Mbowe.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
Kauli hiyo ya Mbowe iliungwa mkono na Luena ambaye alisema
katika uchaguzi lazima idadi ya wajumbe iwiane na idadi ya kura
zitakazopigwa.
Pamoja na ufafanuzi huo, kuliibuka majibizano
mengine ya jinsi ya kurudia uchaguzi huo na Dk Kashililah alitangaza
utaratibu wa wajumbe kufika mbele ya meza kuchukua karatasi za kupigia
kura na wakati huohuo watakuwa wakihesabiwa idadi yao. Kazi hiyo
ilichukua dakika 35.
Kuomba kura
Awali, wakati wagombea hao wakiomba kura, Kificho
aliulizwa swali na Mbunge wa Mkanyageni (CUF), Mohamed Habib Mnyaa
kuhusu elimu yake lakini badala ya kujibu swali hilo alianza kueleza
kuhusu madeni aliyonayo.
“Mheshimiwa Kificho umetueleza kuwa una uzoefu wa
miaka 18 lakini hujatueleza kuhusu elimu yako, tungependa kufahamu
kuhusu hilo,” alisema Mnyaa.
Akijibu swali hilo, Kificho alisema, “Kwa sasa
sina takwimu kuhusu madeni yangu,” kabla ya kushtuka na kutaka kurudiwa
kwa swali hilo.
Baada ya kulielewa swali hilo, Kificho alisema
kuwa ana stashahada ya sheria ambayo aliipata katika chuo cha IDM Mzumbe
ambacho hivi sasa ni Chuo Kikuu cha Mzumbe.
Mbunge wa Chakechake (CUF), Musa Haji Kombo
alimuuliza Kificho: “Umetueleza uzoefu wako, sasa nauliza swali, kama
nikikupigia kura utasikia raha?”
Katika majibu yake Kificho alisema, “Ndiyo maana tangu mwanzo niliwaomba kura za ndiyo.”
Akizungumzia uchaguzi huo, Mwenyekiti wa CUF,
Profesa Ibrahim Lipumba na Mjumbe wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT),
Ezekiel Oluochi kwa nyakati tofauti walisema kuwa ni wazi mazingira hadi
ushindi wa Kificho yalikuwa yameandaliwa.
Mwananchi
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment