Rais Barack Obama wa Marekani  amewasili nchini leo tayari kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ambapo amelakiwa na mwenyeji wake Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.

Baada ya kuwasili akitokea Afrika Kusini ,Rais Obama alipigiwa mizinga 21 na vikosi vya jeshi la wananchi wa Tanzania na kisha kukagua gwaride na kuangalia vikundi  vya ngoma na burudani mbalimbali kutoka Tanzania.

Rais Obama ameambatana na mkewe Michelle Obama na watoto wao huku msafara wake ukiwa na ujumbe wa watu 700 wakiwemo viongozi,wafanyabiashara,wataalam wa kada mbalimbali na waandishi wa habari.

Wananchi wa jiji la Dar es Salaam na viunga vyake wamejitokeza kwa wingi katika barabara ya Nyerere na barabara nyingine alizopitia  Rais Obama na msafara wake kwa lengo la kumkaribisha.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na ofisi ya mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam inaonesha kuwa Rais Kikwete atakuwa na mazungumzo na mgeni wake Ikulu ambapo pia amemuandalia dhifa ya kitaifa.

Hapo Kesho Rais Obama anataraji kuhitimisha ziara yake ya siku mbili kwa  kutembelea Mitambo ya kufua umeme ya kampuni ya Symbion kabla ya kuondoka na kurejea nchini Marekani.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top