Mke  wa Rais  wa Marekani,  Mama  Michelle Obama, amempongeza  Mke wa Rais  Mama  Salma  Kikwete  kwa kazi  kubwa anayoifanya  ya kutoa elimu bure  kwa watoto wa kike ambao ni yatima  na wanaoishi katika mazingira hatarishi .

Mama Obama  alizitoa pongezi hizo wakati wa majadiliano baina yake na Mama Laura Bush kwenye mkutano wa   Wake wa Marais Wa Afrika uliofanyika katika hoteli ya Serena  jijini Dar es  Salaam.

Mama Obama alisema kuwa wake Wa Marais wana kazi kubwa ya kuhakikisha kuwa wanawasaidia  wanawake na watoto hasa katika upatikanaji wa elimu na mahitaji mengine muhimu.

Akiongea wakati wa ufunguzi wa mkutano huo Mama Kikwete alisema kuwa wake wa Marais waliohudhuria mkutano huo wanawawakilisha wanawake wa Afrika ambao wanahitaji kusaidiwa katika mambo ya afya,  elimu na ujasiriamali.

Mama  Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA)  alisema kuwa katika mkutano huo washiriki watapata nafasi ya kubadilishana ujuzi wa kazi  na kutembelea hospitali ya Kansa ya Ocen Road, kituo cha Mabinti na hospitali ya CCBRT ambako watajionea jitihada kubwa zinazofanywa na watanzania za kuisaidia jamii inayowazunguka.

Alisema kuwa baada ya kumalizika kwa mkutano huo anaamini kuwa washiriki watarudi katika nchi zao na kuweza kukubaliana na Serikali zao pamoja na wadau wao wengine kuwekeza zaidi kwa wanawake ili kuimarisha Bara  la Afrika.

Mkutano huo wa siku mbili   uliandaliwa na Taasisi ya Rais mstaafu wa Marekani, George Bush, na kuhudhuriwa na baadhi ya Wake wa Marais wa Afrika na Mke wa Waziri mkuu mstaafu wa Uingereza, Cherie Blair.

Mada kuu ilikuwa wekeza kwa wanawake imarisha Afrika lengo likiwa ni kuimarisha upatikanaji wa Afya  kwa wanawake, upatikanaji Wa elimu na uchumi katika Afrika.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top