Akizungumza katika maadhimisho hayo, Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi
aliyemwakilisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema wafanyabiashara wa
dawa za kulevya ni watu hatari na kwamba, wanaweza kuingilia misingi ya
kiutawala, hivyo Watanzania hawana budi kuipiga vita kwa nguvu zote.
Alisema iwapo biashara hiyo haitadhibitiwa
kikamilifu na kuachwa ikaendelea moja ya athari zitakazojitokeza ni
kuingiliwa kwa misingi ya utawala na ongezeko kubwa la rushwa.
Kauli hii inaonyesha kuwa Serikali imekata tamaa
katika mapambano ya dawa za kulevya nchini. Tulitarajia Serikali
ingetangaza mafanikio ya mapambano hayo, siyo takwimu tu za tatizo. Kwa
mfano kama Lukuvi anakiri kwamba biashara hiyo inawagusa watendaji wa
Serikali, basi watajwe na wachukuliwe hatua hadharani.
Hali hiyo inajitokeza wakati kukiwa na ongezeko la Watanzania wanaokamatwa kwa kujihusisha na biashara hiyo.
Kwa mfano katika kipindi cha mwaka 2008 hadi 2012,
watuhumiwa 10,799 walitiwa mbaroni kwa kujihusisha na biashara hiyo
nchini, huku Watanzania 240 wakikamatwa katika nchi za Brazil, Pakistan
na Afrika Kusini na baadhi wamefungwa.
Taarifa ya Serikali inaonyesha pia kuongezeka kwa
tatizo hilo hadi ilipofika mwaka 2010 ambapo kilo 914 za dawa za kulevya
aina ya heroin, zilikamatwa na kikosi kazi cha kuzuia uharamia nchini.
Tumeshuhudia pia viashiria vya matumizi ya dawa za
kulevya nchini hasa kwa wasanii wa muziki na michezo mingine. Ni hivi
karibuni tu kulikuwa na kifo cha utata cha msanii Albert Mangwair
aliyefia nchini Afrika Kusini huku ikidaiwa kuwa alikuwa na ‘mzigo’
tumboni.
Kifo chake kilifuatiwa na msanii mwingine wa muziki wa kizazi kipya, Langa Kileo ambaye naye aliathirika na dawa hizo.
Msanii mwingine aliyeathirika na dawa za kulevya
na sasa anapatiwa matibabu kwa ufadhili wa Rais Jakaya Kikwete ni Rehema
Chalamila.
Kama hiyo haitoshi, tumeshuhudia hukumu ya miaka
15 aliyopewa mwanamichezo wa ndondi, Petro Mtagwa na watu wengine watatu
waliokamatwa na dawa za kulevya aina ya Heroin nchini Mauritius.
Hao pamoja na wengine wengi wanaonyesha kuwa janga
hili ni kubwa mno. Hata hivyo nina wasiwasi na hatua zinazochukuliwa na
Serikali yetu.
Ni kweli kwamba kuna kikosi maalumu cha Jeshi la Polisi cha
kupambana na dawa za kulevya. Lakini hatuoni hatua kali zikichukuliwa
kwa wahusika kama nchi nyingine.
Zipo baadhi ya nchi ambazo mtu akikamatwa, ama
anashtakiwa na kupata kifungo mara moja, nchi nyingine watu wanahukumiwa
kunyongwa hadi kufa. Hiyo yote ni kuonyesha jinsi wenzetu walivyo
makini na mapambano hayo. Lakini nchi yetu, tunasikia tu watu
wanakamatwa, lakini mwenendo wa kesi zao hausikiki tena.
Ninamaanisha kwamba hatuna hatua kali kwa wahusika hao. Nadhani kuna haja ya sheria za kudhibiti dawa za kulevya zingepitiwa upya ili kuongezwa makali.
Ninamaanisha kwamba hatuna hatua kali kwa wahusika hao. Nadhani kuna haja ya sheria za kudhibiti dawa za kulevya zingepitiwa upya ili kuongezwa makali.
Kama takwimu zinaonyesha kuwa uingizaji umekuwa
mkubwa na watu wanakamatwa, huwa wanapelekwa wapi? Dawa zilizokamatwa
zinapelekwa wapi?
Mambo haya yote yanapaswa kufanyika kwa uwazi ili kutoa onyo kwa wengine wanaoweza kushawishika kujiingiza kwenye biashara hiyo.
Hatua nyingine ambayo Serikali ingetilia mkazo ni
kwa wasanii na wanamichezo ambao kwa kiasi kikubwa wanaonekana
kuathirika ni kuweka walau kanuni za kuwadhibiti.
Baraza la Sanaa Tanzania (Basata) linapaswa
kuwasajili wasanii wote nchini na ikiwezekana kuwapima mara kwa mara
kama wanatumia dawa za kulevya, kama vinavyofanya vyama vya michezo kwa
wachezaji.
Wasanii wanaokutwa na hatia wachukuliwe hatua kali
ikiwa pamoja na kifungo gerezani na kufutiwa usajili wa kufanya kazi za
sanaa nchini. Tusingoje hadi vijana hawa waathirike ndiyo waanzishiwe
matibabu.
Hatua nyingine ambayo ni ya kutibu ni Serikali
kufadhili au kuanzisha vituo vya kuwatibu walioathirika. Hatua hii isiwe
kwa watu maarufu tu, bali hata wa hali ya chini ili kuwakwamua katika
janga hilo.
Hatua hizi zinapaswa kuchukuliwa mapema huku Serikali pia ikiimarisha ulinzi kwa njia zinazotumika kuingiza dawa hizo.
Mwananchi
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment