MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, leo inatarajia kutoa uamuzi wa kumpa au kutompa dhamana Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Wilfred Lwakatare na Ludovick Joseph wanaokabiliwa na kosa la kula njama kutaka kumuua kwa sumu Mhariri Mtendaji wa gazeti la Mwananchi, Denis Msaki.

Hatua hiyo ilitangazwa jana na Hakimu Mkazi wa mahakama hiyo, Alocye Katemana, baada ya Wakili Mwandamizi wa Serikali, Ponsian Lukosi, kuikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuwa imekuja kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Katemana alisema uamuzi wa dhamana ya Lwakatare na mshirika wake, itatolewa leo baada ya kupitia maombi ya dhamana yaliyowasilishwa na mawakili wa Lwakatare, Peter Kibatara na Abdalah Safari Mei 13, mwaka huu mbele ya Hakimu Mkazi, Sundi Fimbo, wakati hakimu huyo alipokuwa likizo.

Katika maombi hayo ya dhamana yaliyowasilishwa Mei 13, mawakili wa Lwakatare walidai kuwa kosa la kula njama linadhaminika kwa mujibu wa sheria.

Hata hivyo Wakili wa Serikali, Prudence alililipinga ombi hilo kwa madai kuwa shauri hilo lipo hatua za uchunguzi, kilichopo mahakamani ni jalada la tuhuma zinazowakabili washitakiwa ambazo zipo katika hatua za uchunguzi na kwamba tuhuma hizo mwisho wa siku zitafunguliwa kesi rasmi Mahakama Kuu, kwani ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza, hivyo mahakama hiyo haiwezi kutoa dhamana kwa kesi ambayo haipo.

“Na kwa mazingira ya shauri linalomkabili Lwakatare hapa Mahakama ya Kisutu, lipo katika hatua za uchunguzi na bado DPP hajafungua kesi rasmi Mahakama Kuu, sasa tunashangaa mawakili wa washitakiwa wanawasilisha ombi la dhamana leo hii katika mahakama hii wakati maamuzi ya Mahakama ya Rufaa yapo na bado hayajatenguliwa,” alisema.

Machi 20 mwaka huu, Lwakatare na wenzake walifunguliwa rasmi kesi Na. 6/2013 ya tuhuma za ugaidi ambapo kosa la pili, tatu, na la nne yalikuwa hayana dhamana, hivyo Mei 8 mwaka huu, Jaji Kaduri aliyafuta makosa hayo kwa maelezo kuwa hajaona kama kuna maelezo ya kutosha ya kuwafungulia mashitaka ya ugaidi.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments:

 
Top