Mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Godfrey Mgimwa
Pingamzi lililowekwa juzi na mgombea wa Chadema dhidi ya
mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Godfrey Mgimwa limetupiliwa mbali
baada ya mgombea huyo wa CCM kuwasilisha nyaraka mbalimbali
zinazothibitisha uraia wake kwa msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Kalenga,
Pudenciana Kisaka.
Msimamizi wa uchaguzi, Pundenciana aliliambia
gazeti hili jana kuwa, alipokea vielelezo kutoka kwa mgombea wa CCM
vinavyothibitisha uraia wake baada ya kumwandikia barua ya kumtaka
kufanya hivyo.
Alisema kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, mgombea
anapowekewa pingamizi anaarifiwa kwa barua, akitakiwa kuwasilisha
vielelezo huku aliyeweka pingamizi akitakiwa kuwasilisha vielelezo
vinavyomtaka athibitishe madai yake.
“Mgombea wa CCM Mgimwa alileta vielelezo vyake na
wa Chadema ameleta barua lakini hakuwasilisha vielelezo alivyokuwa
amedaiwa, kwa hatua hiyo nimeshatoa majibu ya madai yao na hayo mnaweza
kuyapata kwa wagombea wenyewe,”alisema.
Akithibitisha kutolewa kwa uamuzi huo, Mratibu wa
Chadema, Frank Mwaisumbi alisema, “Ni kweli tumepata majibu ya mgombea
wa CCM kupitia kwa msimamizi wa uchaguzi, hatujaridhika nayo,” alisema.
Mgombea wa Chadema aliwasilisha pingamizi lake
Februari 19 akitoa madai matano, likiwamo la kuwa na shaka na uraia wa
mgombea wa CCM walipodai si Mtanzania.
Akizungumza na waandishi, mgombea ubunge kupitia
CCM, Godfrey Mgimwa alisema ameshangazwa na tuhuma za kudaiwa yeye si
Mtanzania wakati amezaliwa katika Hospitali ya Mkoa wa Iringa na kusoma
Shule ya Msingi Wilolesi iliyopo mkoani hapa.
Huku akionyesha vielelezo vya kuthibitisha uraia
wake, Mgimwa ambaye pia ni mtoto wa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la
Kalenga, Marehemu Dk William Mgimwa alisema, asingekuwa raia wa Tanzania
asingekuwa na hati ya kusafiria ya Tanzania kwa kuwa nchi hii ina uraia
wa nchi mmoja.
Mgimwa alifafanua kuwa, baada ya kutoka Shule ya
Msingi Wiloles ya mjini hapa alijiunga na Shule ya Sekondari ya Azania
ya Dar es Salaam na baadaye alikwenda St Marys kabla ya kujiunga na
elimu ya chuo ngazi ya Shahada ya Kwanza Uingereza.
Kwa upande wake Kaimu Katibu wa CCM mkoani hapa,
Hassan Mtenga alisema ameshangazwa na taarifa hizo za Chadema kumwekea
pingamizi mgombea huyo akidai si za kweli na wameonyesha hofu dhidi ya
mgombea wao.
Naye Katibu wa Iringa Vijijini, Amina Mahimbo
alikanusha kauli ya Chadema kuwa wanachama 25 waliomdhamini mgombea wa
CCM si wazawa wa Kalenga na kusema wote walitoka katika jimbo hilo ambao
ni viongozi na wanachama wa Jimbo la Kalenga. Uchaguzi mdogo wa Jimbo
la Kalenga mkoani hapa, unatarajiwa kufanyika Machi 16 ukiwashirikisha
wagombea kutoka vyama vitatu.
Mwananchi
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI
Mwananchi
0 comments:
Post a Comment